Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi

Hon. Katani Ahmadi Katani

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Tandahimba

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi

MHE. KATANI A. KATANI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nami nikushukuru, nikiendelea kwa yale aliyoachia ndugu yangu Khatib, ninalo jambo la kuzungumza juu ya Jeshi la Polisi. Page ya 12 wamezungumzia suala la kuboresha Mfumo wa Upelelezi wa suala la kesi za jinai. Hili jambo ni jambo jema sana kama mfumo utafanya kazi inavyopaswa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna mambo ambayo yanaleta mkanganyiko sana. Tarehe 8 Agosti, 2015 Jimboni kwangu Tandahimba wamechukuliwa watu takriban tisa. Watu wenyewe wengi wao ni Masheikh. Bahati mbaya wamepelekwa Dar es Salaam wameingizwa kwenye kesi ya mauaji tena kesi yenyewe Polisi wanafika pale Oysterbay wanauliza watu hawa tuwape kesi gani. Ndiyo maana mpaka leo kesi ipo mahakamani ushahidi mpaka leo haujakamilika. Haujakamilika kwa sababu yaliyofanyika ni uonevu unaotokana na jeshi la polisi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mfano yupo mtu anaitwa Mbaraka, Mbaraka tarehe ambayo amebambikiwa kwenye kesi ile ya mauaji ya Ikwiriri, hatupendi kuona Polisi wakiuliwa, Mbaraka alikuwa kwenye kikao cha TANEKU Newala, siku ya pili ameshiriki kikao cha kamati ya shule, amelala kwenye msiba, lakini unamkamata mtu unamwambia kwamba amehusika kwenye kesi ya mauaji ya Ikwiriri. Huu ni uonevu wa Jeshi la Polisi ambao hauna mfano kabisa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, haya ni mambo ya ajabu kwa jeshi tunalolitegemea. Naamini IGP Kamanda Sirro anafanya kazi nzuri kwenye kudhibiti uhalifu. Kwenye kuonea watu hawa ambao hawana hatia ni mambo ya ajabu sana, wanalidhalilisha Jeshi letu la Polisi bila sababu za msingi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hawa watu leo wana miaka takribani mitatu au minne na kesi zao zilishawahi kwenda kwa Waziri aliyekuwa wa Sheria kipindi hicho akasema anashughulikia, lakini mpaka leo watu hawa wanakwenda mahakamani wanarudi, ushahidi bado haujakamilika. Ni lini ushahidi utakamilika? Wanawapaje v ifungo Watanzania ambao hawana hatia kwa sababu ushahidi haujakamilika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niwaombe sana, Jeshi la Polisi tunalolitegemea, wanapoamua kufanya kazi zao wafanye kwa weledi. Nami naamini kabisa Jeshi la Polisi wapo watu wana uzoefu, wana uzoefu na upelelezi. Hizi tamaa za fedha, maana matukio haya kwa Mtwara yamekuwa yanafanyika kwa ajili ya tamaa ya fedha. Wapo watu wameuawa, wapo watu wakitoa fedha milioni mbili, milioni tatu wanaachiwa, kama kweli wangekuwa wauaji wasingewaachia basi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, juzi, leo wiki ya pili wamekamatwa watu wangu Tandahimba kule, Kijiji cha Mihambwe. Tandahimba mpaka wetu wa Tandahimba na Msumbiji ni Mto Ruvuma. Tandahimba hakuna tembo, Tandahimba hakuna mali hizo zinazosemwa watu wale wamepelekwa polisi inasemekana kwamba wanauza meno ya tembo. Meno ya tembo Tandahimba yanatoka wapi? Maana siyo Liwale Tandahimba, mwisho wa siku wanatoa 2,500,000 hawana kesi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, haya mambo Jeshi la Polisi wanajidhalilisha bila sababu za msingi. Hata hivyo, inawezekana haya mambo yanafanyika kwa sababu ya vipato vidogo vya Jeshi letu la Polisi. Kama wangekuwa wanawapa mafao yanayofanana, nadhani wasingekuwa na tamaa na fedha hizi ndogo ndogo hizi. Kwa hiyo, niwaombe sana kwenye kuboresha maslahi ya jeshi la Polisi labda watafanya kazi kwa weledi, basi waone namna gani wanapata maslahi yaliyo bora ili watu wetu waweze kufanyiwa mambo yao kwa utu na kwa kutumia haki za msingi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la udhibiti wa uhalifu nchini; nimpongeze IGP na jeshi lake kwa sasa suala la uhalifu limepungua kwa asilimia 90. Mimi nilipongeze sana Jeshi la Polisi nchini. Hata hivyo, kwenye matukio haya wapo wezi ambao wanaiba pikipiki Dar es Salaam, wanapeleka Mtwara, wanapeleka maeneo mengine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, zile pikipiki wanatengeneza kadi feki unapotoa pikipiki Dar es Salaam ina kadi feki ukapeleka Ngara, mtu wa Ngara hawezi kubaini kadi feki. Anauziwa pikipiki yenye kadi feki ambayo ukiangalia document zinaonesha zinafanana na mwisho wa siku anakamatwa mtu wa Ngara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, operation yao wanayofanya kwa ajili ya wezi hawa, naamini kabisa kwamba IGP Sirro wanaweza wakawabaini watu hawa ambao wengi wao wanatoka Dar es Salaam na wizi mkubwa wa pikipiki unafanyika Dar es Salaam. Badala ya kwenda kukamata watu wetu ambao wanateswa mwishoni japo wanasema na waliowauzia pikipiki akina nani? Hata hivyo, wanashindwa kuwakamata waliouza pikipiki wanakwenda kwa watu wa hali ya chini wale, badala ya kuchukua pikipiki wazi-hold, wale watu na wenyewe wanaendelea kuwatesa bila sababu za msingi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nije sasa kwenye suala la mipaka, kwenye Idara za Mheshimiwa Waziri kwa maana ya Wizara yake ya Mambo ya Ndani afadhali Jeshi la Polisi wana vitendea kazi vya kutosha, japo havitoshi kwa kiwango hicho kinachoridhisha, lakini wapo watu wanafanya kazi kubwa ndugu zetu wa uhamiaji. , maeneo ya mipakani ambapo watu wa uhamiaji wapo hawana vitendea kazi, hawana magari, lakini hata OC zao hawazipeleki, watafanyaje kazi watu hawa wa Idara hii ya Uhamiaji? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mkoa wa Mtwara wanajua tunapakana na Mto Ruvuma pale. Watu wa Uhamiaji ni watu ambao wanapaswa wawe na magari kwa ajili doria na vitu vingine kule, lakini leo hawana magari; lakini OC hizi za milioni moja moja tunazosema wakienda kuangalia Uhamiaji wamepeleka lini wataona aibu wenyewe. Waende wakaangalie wataona aibu wenyewe! Wawapelekee OC hizi waweze kufanya kazi kwa ufasaha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimwombe sana Mheshimiwa Waziri kwenye kuboresha maslahi ya ndugu zetu hawa wa Uhamiaji ambao wanafanya kazi kubwa sana. Wanafanya kazi kweli kweli, amepata kuzungumza Mzee Ally Keissy pale kwamba zamani kulikuwa na passport zinapatikana kwa raia ambao hata sio Watanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wapo watu wanatoka Burundi wanafanya ujanja ujanja wanapita Tanzania wanapata documents, wanaenda South Africa ndio wanauza madawa ya kulevya akikamatwa kwa sababu ana document ya Tanzania, anaonekana ni Mtanzania. Uhalifu huu umefanywa katika maeneo mengi wakitajwa Watanzania kumbe sio Watanzania ni Wanyarwanda wengine ni Warundi, wanafanya matukio haya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa ili kuimarisha mifumo hii, Idara yetu ya Uhamiaji ni lazima waipe nguvu ya kutosha, waweze kufanya kazi zao vizuri ili tuweze kuimarisha mazingira haya na kuondoa maneno yanayotajwa Tanzania kumbe sio Watanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niliwahi kumwambia tatizo la Askari wetu wa Usalama Barabarani hususan Tandahimba, lakini hata alipokwenda Waziri Mkuu wananchi wameweza kuonesha mabango pale. Jeshi la Polisi Usalama wa Barabarani kuna tatizo gan? Kwa nini askari wa usalama barabarani apige mtu viboko ndio sheria inavyotaka, ndiyo PGO ilivyoandikwa ndani humo?

Mheshimiwa Mwenyekiti, mara kadhaa yametokea matukio ya Tandahimba zaidi ya matatu au manne hata akisema Mheshimiwa Waziri tuondoke au IGP twende atakuta vijana wamepata ajali kwa sababu DTO anachomeka gari yake anamchomekea bodaboda na sio mara moja au mara mbili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, yametokea matukio zaidi ya mara tatu, mara nne, kwa ajili ya ustahimilivu ya watu kuheshimu Serikali, vinginevyo wangeamua kuchukua sheria mkononi, wao kwa sababu wana silaha za moto wanasema wananchi ndio wenye matatizo, kumbe matatizo mengine yanazalishwa na Jeshi la Polisi lenyewe. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa Tandahimba tatizo kubwa ni DTO peke yake, askari wengine wa usalama barabarani wanafanya kazi kwa weledi, yeye ndiyo anafanya matukio haya ya ovyo na siyo mara moja au mara mbili, Mheshimiwa Mwigulu nimeshamwambia zaidi ya mara tatu jambo hili. Waziri Mkuu amekwenda kwenye ziara Tandahimba amekutana na mabango, bahati mbaya mimi sikuwepo nilikuwa Ubelgiji huko, amekutana na mabango watu wakilalamikia hali hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa kama wanampenda sana DTO wambadilishe hata kituo wachukue Mheshimiwa Mwigulu wapeleke kwake pale, akawafanyie watu wake aone uchungu atakaoupata. Atajua wapiga kura wake wakipigwa, mtu amekosa kuvaa helmet kweli amefanya kosa ni sahihi apigwe viboko na DTO? Ni sahihi achomekewe gari na DTO? Kwa nini DTO wa Tandahimba avunje sheria na Jeshi la Polisi lipo, Waziri anajua bado tunaendelea kukaa naye. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sisi bwana ni wanadamu kweli kweli na tuna utu kweli kweli, wakati mwingine ukionewa sana utakapoamua kunyanyua mguu, aliyenyanyua mguu ataonekana mkorofi. Hatutaki watu wa Tandahimba tufike huko. Najua wana busara za kutosha, IGP yupo anasikia, Waziri nimemweleza jambo hili zaidi ya mara tatu, lakini wameendelea kumwacha yule bwana, aidha kuna jambo wanalitengeneza Tandahimba, aidha utokee ugomvi baina ya polisi na raia kwa sababu wana bunduki wapige watu wa Tandahimba. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niombe sana mtu mmoja asisababishe amani ya watu wa Tandahimba wote. Miaka miwili mfululizo Tandahimba hatufanyi biashara kwa uhuru pale. Watu wanakwenda Newala ambako kuna unafuu Traffic hawatumii nguvu kubwa wanakwenda kununua bidhaa kule, tunaiacha Tandahimba ikididimia pale kwa ajili ya mtu mmoja ambaye anafanya watu washindwe kuingia Tandahimba kwa kutofuata sheria.