Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo

Hon. Amina Saleh Athuman Mollel

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo

MHE. AMINA S. MOLLEL: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi hii ya kuweza kuchangia. Awali ya yote namshukuru Mwenyezi Mungu kwa kuniwezesha kuwa hapa, pili naomba nifafanue na kuweka taarifa sahihi kwenye Hansard. Nilimaanisha saa tatu asubuhi mpaka saa nne na nusu kipindi cha maswali na majibu ndiyo lilikuwa lengo langu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pili kama sijaenda mbali zaidi naomba nizungumzie kidogo alichozungumzia mwenzangu aliyemaliza kuongea. Katika habari lengo kuu la tasnia ya habari ni kuelimisha, kuhabarisha na kuburudisha. Kwa hiyo katika TV kuna vipindi vya kuelimisha, kuna vipindi vya kuburudisha na kuna vipindi ambavyo vinajumuisha kwenye michezo, burudani lakini vya kuhabarisha ni kama habari. Kwa hiyo, allipozungumzia kuhusu taarifa ya habari dakika tatu, taarifa ya habari unakuta ni nusu saa na inajumlisha matukio yote hayo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika taarifa ya habari, habari nyingine kwa mfano habari kubwa kama ya Rais itakwenda dakika tatu mpaka dakika tano, lakini habari nyingine zitakwenda dadika moja moja au dakika mbili na kama kuna tukio maalum la Rais wanachofanya ni kusema kwamba kutakuwa na kipindi maalum na katika kipindi hicho maalum wanarudia hiyo taarifa katika kuelezea. Kwa hiyo, nataka tu kuweka ufafanuzi huo kwa sababu TBC hawana nafasi ya kuja kujadili hapa na kwa sababu na mimi pia ni mwanataaluma na nimetoka huko.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo napenda pia nimshukuru Mwenyekiti wa Bunge wa Michezo, Mheshimiwa Ngeleja na Kamati yake kwa ujumla kwa kuniteua kuwa Msemaji wa Timu ya Bunge, kwa hili nashukuru sana na mimi nasema kwamba kipele kimepata mkunaji na mimi nitakikuna sawasawa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo nianze na maswali kwa Mheshimiwa Waziri atakapokuja ku- windup aje kutufahamisha. Mheshimiwa Waziri timu yetu imekwenda kushiriki mashindano ya Jumuiya ya Madola kule Australia. Taarifa nilizonazo mpaka hivi sasa ni kwamba miongoni mwa wachezaji waliokwenda huko mmoja ametoroka kambini na amezamia huko nchini Australia. Jina lake nimelipata anaitwa Fathiya kutoka Ukonga.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba Mheshimiwa Waziri atakapokuja ku-windup atufahamishe kwamba hizi taarifa je, zina ukweli wowote kwamba huyu mchezaji ametoroka kambini na kuzamia huko nchini Australia? Pia nataka kujua kwamba kama ni kweli ametoroka ni vipi mahusiano yetu kati ya Tanzania na Australia, hili haliwezi kututia doa kwa sababu sisi tunafahamu Tanzania ni miongoni mwa nchi ambazo zimekuwa zikipokea sana wakimbizi, lakini siyo Watanzania kutorokea kama huyu mwenzetu alivyofanya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hilo kwa sababu dakika ni chache, moja kwa moja niende kwa maslahi ya Waandishi wa Habari. Tunafahamu kwamba tuna mhimili mitatu, Mihimili wa Bunge, Mahakama na Serikali lakini tasnia ya Habari pia ni mhimili ambao tunauhesabu kama mhimili wa nne, lakini waandishi wa habari wamekuwa wakifanya kazi katika mazingira magumu sana. Wengi wao hawalipwi ipasavyo na hata katika ile mikataba yao, ukienda kwa mfano anapofanya miaka miwili hakuna chochote kinachoingizwa katika mifuko.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano mifuko kabla haijavunjwa sasa hivi na kuwa mifuko miwili; tunafahamu kulikuwa kuna PPF na mifuko mingineyo, ilikuwa haipelekwi huko. Kwa hiyo, Mheshimiwa Waziri naomba atakapokuja atufahamishe hapa ni vyombo gani ambavyo vimekuwa haviwalipi Waandishi wa Habari ipasavyo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Waandishi wa Habari wanafanya kazi kubwa sana. Popote pale ulipo Waandishi wapo na ndiyo wanaowahabarisha wananchi, matokeo yake hawapati hiyo mishahara kwa hiyo, naomba Mheshimiwa Waziri atakapokuja atufahamishe amechukua hatua gani.

Mhshimiwa Mwenyekiti, pia, nivipongeze vyombo ambavyo vimekuwa mstari wa mbele katika kuwalipa na hasa mimi nitolee mfano Azam, nawapongeza sana TBC, lakini pia, hata ITV.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia, namwomba Mheshimiwa Waziri atakapokuja aje atueleze, mwaka jana nakumbuka mwenzangu ambaye sasa hivi ni Naibu Waziri alishika shilingi kwa ajili ya kutaka wakalimani katika taarifa za habari. Naomba kufahamu mchakato huo umefikia wapi?

Mheshimiwa Mwenyekiti, wanamuziki wetu tunafahamu kwamba, muziki wa dansi tulikotoka mpaka hivi sasa, lakini kwa mfano kwa hivi sasa kumbi nyingi za burudani zinatakiwa zifungwe saa sita kamili usiku, kama unavyofahamu saa sita kwetu watu wazima ndiyo kumenoga kwelikweli, lakini hawa pia ndiyo ajira yao wanaambiwa kwamba muda huo wafunge. Mpaka wamefikia kuwaweka wasanii ndani kwa mfano mwanamuziki mkongwe King Kikii aliwekwa ndani. Naomba Mheshimiwa Waziri atakapokuja hapa aje kutufahamisha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali langu lingine ni kwamba, Maafisa Utamaduni, tunafahamu wapo chini ya TAMISEMI. Nataka kujua hivi sasa je, ule ufanyaji kazi wao ukoje na Wizara husika kwa sababu, mambo ya sanaa, utamaduni na michezo yako katika Wizara yake, aje kutuambia kwamba, wamefikia wapi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la maadili, naomba Waziri aje kutufahamisha, Mheshimiwa Waziri nimemwonesha katika Night Clubs zetu kumekuwa na mchezo ambao wanahamasishwa labda kama ni mwanamke au mwanaume kucheza na wakati mwingine mpaka kufikia kuvua nguo na kufanya tendo la ndoa na Mheshimiwa Waziri nimemwonesha kilichotokea hivi karibuni. Nataka atakapokuja hapa aje atueleze wamechukuliwa hatua gani na ni mikakati gani ipo kwa ajili ya kuhakikisha kwamba, utamaduni wetu na maadili yetu tunayalinda?

Mheshimiwa Mwenyekiti, Shirika la TBC, naweza kusema ni miongoni mwa mashirika ambayo yana wataalam waliobobea, wakongwe tangu miaka hiyo. TBC tunafahamu popote pale katika shughuli zote za Kitaifa, TBC ndiyo ambao wamekuwa wakitegemewa sana, lakini wakati mwingine tunawalaumu TBC wakati makosa siyo ya kwao. Makosa siyo ya kwao kwa sababu hatujaliangalia ni kwa jinsi gani tunawekeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hili ni shirika la umma, namwomba Mheshimiwa Waziri atakapokuja hapa atueleze ni kwa jinsi gani analiwezesha Shirika la Utangazaji (TBC) ili basi liwe kweli ni Shirika la Umma, liwe kweli shirika ambalo linaweza kufanya majukumu yake na hizi lawama zinazotokea zote ni kwa sababu, tumelisahau.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimeona katika taarifa kwamba, wamesema wanakuja kujenga studio ya kisasa hapa Mjini Dodoma, lakini je, kwa wakati huu ambapo bado wapo Dar es Salaam tunawawezesha vipi? Naomba kwa sababu ndiyo shirika tunalolitegemea sana katika utendaji wa kazi wamebobea. TBC ndiyo ambao wamefunga mitambo ya vyombo vingine vyote, kwa maana kwamba, wamewatoa wataalam TBC na wamekwenda kufunga huko. Kama wanaweza kufunga huko kote kwa nini washindwe wao kufanya vizuri? Ni kwamba, hatujaamua kuwekeza ipasavyo katika Shirika la Utangazaji (TBC). (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naomba sana, leo hii mimi najivunia uwepo wangu hapa ni kwa sababu nimelelewa katika taaluma, nimetoka huko ndiyo maana najivunia uwepo wangu hapa bila kusahau nilipotoka, siku zote tulipotoka ndipo ambapo pameweza kutufikisha hapa. Naipongeza sana TBC na naomba tuwawezeshe ili waweze kufanya kazi kwa ufanisi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nizungumzie Online TV. Nafurahi kwa sababu, vijana wengi wamepata ajira hivi sasa, lakini katika kila kitu kisipowekewa msingi mzuri ni dhahiri kabisa kwamba hata maadili wakati mwingine yanaweza kukiukwa, ndiyo maana hata ukiangalia nyingine zinafanya vizuri sana, lakini sasa utaratibu ambao amekuja nao Mheshimiwa Waziri, nafurahi kwamba, tutaweka sasa zile guidelines na kuwafahamisha vizuri ili wasiweze kwenda kinyume na maadili ya Mtanzania, kwa sababu ile ni njia mojawapo pia ya habari, tuone kwamba ni kwa jinsi gani wanafuata misingi, sheria na taratibu zilizopo katika kuhakikisha kwamba, wanaendelea kuuhabarisha umma. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niongelee kuhusu sanaa na utamaduni. Sipingani na maamuzi ya Serikali katika kuwafungia Wasanii. Hapa kuna sehemu tulikosea kwa sababu haiwezekani mwanamuziki anatoa single yake, ametoa wimbo wake unapigwa halafu wanakuja kumfungia! Hili haliwezekani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tujikumbushe siku za nyuma wanamuziki wengi, wakati huo Redio Tanzania Dar-es- Salaam, walikuwa wakitoa nyimbo zinakuwa edited, baada ya hapo ndiyo zinapigwa. Je, hawa wataalam sasa hivi wako wapi? Tuweke misingi mizuri tuwasaidie wasanii wetu ili wakikiuka baada ya kupewa hiyo misingi mizuri na kulelewa vizuri, hapo ndipo tunaweza tukawahukumu. Kwa hiyo, nawapongeza akina Diamond, nampongeza Monalisa na wengine wote ambao wameweza kupeperusha vizuri bendera ya Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika taarifa pia ya Mheshimiwa Waziri amezungumzia kuhusu Mkataba wa Star Media pamoja na TBC. Nafurahi kwamba, mkataba ule umekuwa renewed hivi sasa na kwamba matakwa yamezingatiwa, lakini sikubaliani na walichosema kwamba kwa miaka yote saba Star Media wamepata hasara! Hii naona kwangu ni aibu kwa kweli.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kumbuka mwaka 2013, TBC na Star Media ndiyo walikuwa wa kwanza kuanza kuuza ving’amuzi, wote ni mashahidi na tunajua…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa mzungumzaji)

MHE. AMINA S. MOLLEL: Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja. Ahsante.