Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano

Hon. Eng. Edwin Amandus Ngonyani

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Namtumbo

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano

MHE. ENG. EDWIN A. NGONYANI: Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Waziri, Profesa Makame Mbarawa, hongera sana kwa kazi kubwa na ya kutukuka unayoifanya wewe na timu yako ya Naibu Mawaziri, Makatibu Wakuu, Wakurugenzi na Wakuu wa Taasisi zote. Hakika mnatubeba wananchi, CCM wote chini ya uongozi mahiri wa Mheshimiwa Rais, Makamu wa Rais na Waziri Mkuu. Mwenyezi Mungu aendelee kuwabariki, Amen.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Waziri, naomba tu nikumbushie masuala yafuatayo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, ujenzi wa barabara ya Lumecha – Kitanda – Londo – Kilosa kwa Mpepo hadi Lupiro kwa kiwango cha lami, barabara hiyo inaunganisha Mikoa ya Ruvuma na Morogoro kupitia Wilaya za Malinyi na Namtumbo ambao ni majirani wa asili wanaounganishwa kwa njia ya miguu tangu enzi za Wajerumani na Waingereza waliokuwa wakiitumia kusafirisha manamba kwa ajili ya kilimo cha mkonge katika Mikoa ya Pwani na Tanga. Tunaomba ujenzi uanze Lumecha kuelekea Londona - Lupiro ambapo kuna daraja linalotenganisha Wilaya na Mikoa hiyo miwili na hivyo kutekeleza Ilani ya CCM ya 2015/2020.

Mheshimiwa Naibu Spika, wakati tukisubiri lami iliyoahidiwa na Serikali ya Awamu ya Tano chini ya uongozi wa Rais wetu mpendwa, Mheshimiwa Dkt. John Pombe Joseph Magufuli, tunaomba juhudi za kutoboa na kuchonga kipande cha barabara kuanzia Londo hadi Kilosa kwa Mpepo zingeharakishwa ili barabara hiyo inayounganisha Wilaya ya Namtumbo (Ruvuma) na Wilaya ya Malinyi (Morogoro) ianze kutumika.

Mheshimiwa Naibu Spika, wananchi wanadhani barabara hiyo imetoboka na hivyo inapitika, kumbe bado haijachongwa na kusababisha wanaotamani kuitumia na kuanza kupita kwa gari ama pikipiki kudhurika kama ilivyotokea kwa Padri wa Hanga Monaskeri aliyetumia pikipiki ambayo ilikwama na hatimaye kutembea kwa miguu hadi kifo kilipomfika kwa sababu ya uchovu na njaa ya siku zaidi ya tatu. Nikuombe Waziri mpendwa, Mheshimiwa Profesa Makame Mnyaa Mbarawa, ushirikiane na Katibu Mkuu wako, Engineer Nyamhanga mtusaidie fedha za kukamilisha uchongaji wa kipande hicho cha barabara ili ianze kupitika. Mameneja wa TANROADS Mikoa ya Ruvuma na Morogoro wana dhamira ya dhati ya kuifanya kazi hiyo lakini wanakwamishwa na ukosefu wa fedha za kutosheleza ukamilifu wa kazi hiyo ya kuchonga.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Waziri, nashukuru kwa kumlipa advance payment Mhandisi Mshauri wa upembuzi yakinifu na usanifu wa kina wa barabara ya Mtwarapachani – Likusanguse – Nalasi hadi Tunduru ili ijengwe kwa kiwango cha lami kama ilivyoahidiwa na Waheshimiwa Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete, Rais wa Awamu ya Nne na Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, Makamu wa Rais wa Serikali hii ya Awamu ya Tano waliofanikiwa kupita katika barabara hiyo na kujionea wingi wa wakazi wanaotegemea barabara hiyo na fursa kubwa zilizopo katika maeneo hayo. Ninakuomba Mheshimiwa Waziri uendelee kuwalipa certificates zao za kazi ili kazi hiyo ikamilike mwakani kama ilivyokubalika katika mkataba na ujenzi kuanza kwa wakati. Hivyo, naomba fedha za kutosha zitengwe.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Waziri, naomba ahadi ya kukipeleka Kivuko cha Ruhuhu kihamishiwe eneo la custom katika Kijiji cha Magazini, Wilaya ya Namtumbo ili safari za wakazi wa Namtumbo, Tarafa ya Sasawala na wakazi wa Tunduru Kusini, Nalasina Mbesa wapate kivuko salama cha kuwapeleka katika vijiji vya Wilaya ya Mabhagho nchini Msumbiji kwa shughuli za kijamii na kibiashara. Vilevile kwa wananchi wa Mabhagho kuja Mkoani Ruvuma kwa shughuli za kibiashara na kijamii.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Waziri, nikuombe uiwezeshe TANROADS Mkoa wa Ruvuma kifedha, watekeleze miradi ya barabara zao ikiwa ni pamoja na barabara za Wilaya ya Namtumbo kama vile Namtumbo – Likuyu – Mkuju kunakojengwa Mgodi wa Madini ya Urani, Utwango – Namabengo – Mbimbi – Luegu, Mkonya – Mgombasi – Nangero – Naikesi na Mkongo Nakawale – Matimila – Mleke. Barabara hizo zipo maeneo ya kiuchumi ya Wilaya ya Namtumbo na zinahudumia wakazi wengi wa Wilaya hiyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Waziri, UCSAF na TCRA wanatekeleza majukumu yao vizuri katika eneo langu na ninawaomba tu watekeleze ahadi zao kwa wananchi wa Namtumbo kupitia mimi Mbunge wao.

Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja kwa asilimia mia moja. Nawasilisha.