Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano

Hon. Zainab Mndolwa Amir

Sex

Female

Party

CUF

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano

MHE. ZAINABU M. AMIRI: Mheshimiwa Naibu Spika, awali ya yote nampongeza Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, Mheshimiwa Profesa Makame Mnyaa Mbarawa, pamoja na Naibu Mawaziri wake kwa kazi nzuri wanazozifanya katika Wizara hii.

Mheshimiwa Naibu Spika, naishauri Serikali iondoe tozo, malipo kwa wananchi wa Kigamboni wanaotumia vyombo vya moto kupita katika Daraja la Kigamboni (Daraja la Nyerere), ni ghali mno na kipato cha Watanzania na hali ya uchumi ni ngumu.

Mheshimiwa Naibu Spika, wakandarasi wanaojenga barabara za lami chini ya kiwango wawajibike kuzikarabati zitakapoharibika kabla ya muda maalum.

Mheshimiwa Naibu Spika, naishauri Serikali iondoe msongamano katika mizani iliyopo Vigwaza, Mikese na Morogoro. Kwa magari ya abiria (mabasi) yawe na eneo maalum la kupima uzito maana mabasi mara nyingi huenda kwa ratiba maalum, abiria wengine ni wagonjwa, watoto na mabasi hutumia muda mwingi katika mizani hiyo. Pia nashauri barabara zote zilizopo pembezoni mwa milima zijengewe pavements ili kuepuka mmomonyoko wa ardhi na ili zisiharibu miundombinu.

Mheshimiwa Naibu Spika, reli ya Dar es Salaam hadi Tanga ifufuliwe ili kuweza kusaidia mizigo mizito hususani malori kutumia reli ili kuepuka uharibifu wa barabara. Katika barabara kuu zijengwe kalvati ambazo zitakuwa na uwezo wa kuhimili wingi wa maji kipindi cha mvua za masika ili kuepuka maji kupita juu ya barabara na kuharibu miundumbinu. Mfano, barabara ya Dodoma - Morogoro eneo la Mbande hadi Kibaigwa ni eneo korofi sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu uwanja wa ndege wa Morogoro ambao upo maeneo ya Kihonda Bima, uwanja ule uboreshwe ili ndege ziweze kutua usiku na mchana na ukizingatia Morogoro kuna Mbuga za Wanyama za Mikumi na Selous ambazo ni vivutio vikubwa vya watalii, kwa kutumia uwanja huo tutaweza kuwavutia watalii wengi kuja Morogoro.

Mheshimiwa Naibu Spika, naishauri Serikali itoe fedha kwa wakati ili kuwezesha Wizara kufanya kazi kwa muda uliopangwa kujenga miundombinu ya nchi yetu.