Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano

Hon. Dr. Shukuru Jumanne Kawambwa

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Bagamoyo

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano

MHE. DKT. SHUKURU J. KAWAMBWA: Mheshimiwa Naibu Spika, namshukuru na kumpongeza Mheshimiwa Waziri kwa hotuba nzuri na utekelezaji mzuri wa Ilani ya CCM. Pia nawapongeza Mheshimiwa Naibu Waziri, Makatibu Wakuu na watendaji wote kwa utendaji kazi mzuri.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika ukurasa 81 wa hotuba ya Mheshimiwa Waziri ametujulisha kuwa mkataba wa Bandari ya Bagamoyo utasainiwa Juni, 2018. Naipongeza sana Serikali kwa hatua hii. Sisi wa Bagamoyo tunahamu sana Waziri atuambie lini ujenzi utaanza? Pia atujulishe lini fidia zilizobaki takribani shilingi bilioni 12 zitalipwa? Pia lini wananchi 687 wanaopisha bandari ambapo wamethibitishwa kupunjwa fidia zao watalipwa? Kukamilisha malipo ya fidia yatasaidia kuliweka eneo la bandari kuwa huru ili likabidhiwe kwa mwekezaji.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu makazi mapya ya wananchi wa vijiji vya Pande na Mlingotini wanaopisha mradi wa bandari, wananchi hawa waliahidiwa na Serikali kupitia EPZA kuwa watapewa makazi mbadala (barua ya EPZA ya tarehe 20.01.2014 ambayo nimekabidhi meza ya Spika) Kijiji kizima cha Pande na sehemu ya kijiji cha Mlingotini vinahamishwa. Kaya zipatazo 460 (wakazi 1,670) zitaathirika. Wananchi hawa wanapoamuliwa kuondoka wanaenda kuishi wapi? Wengi fidia zao hazitowezesha kununua ardhi au kujenga nyumba.

Mheshimiwa Naibu Spika, naiomba Serikali itimize ahadi yake. Ahadi hii ni deni! Ikiwa Serikali itashindwa basi nashauri Serikali imuagize mwekezaji kulipia gharama za makazi mbadala kwa wananchi hawa (resettlement). Hizi ni taratibu za kawaida duniani kwa viwango vya utawala bora. Ni imani yangu mwekezaji atakubali kwa vile hata China na Oman wanawapa wananchi wao makazi mbadala kwa ujenzi wa miradi mikubwa.

Kuhusu ujenzi wa barabara ya Bagamoyo – Saadani - Pangani – Tanga katika ukurasa 129 wa hotuba ya Mheshimiwa Waziri ameahidi ujenzi wa barabara tajwa na kwamba kwa mwaka wa fedha 2018/2019 ujenzi utaanza kwa kilometa 50 Tanga – Pangani. Naomba kumjulisha Mheshimiwa Waziri tuliopigania barabara hii ni pamoja na wananchi wa Bagamoyo na Mbunge wao! Naomba Waziri aweke wakandarasi wawili, mmoja aanze Tanga na mwingine aanze Bagamoyo kilometa 25 kila upande. Hii itaharakisha kazi na Tanga na Bagamoyo. Tulishafanya hivyo kwa miradi ya Manyoni – Tabora, Tunduma – Sumbawanga na kadhalika kipindi hicho mimi nikiwa Waziri. Naomba sana Mheshimiwa Waziri atusaidie jambo hili.

Mheshimiwa Naibu Spika, namshukuru Mheshimiwa Rais kwa ahadi ya ujenzi kwa kiwango cha lami barabara za Bagamoyo mjini kilometa tano na atutengee fedha mwaka huu 2018/2019 kuendelea utekelezaji wa ahadi ya Rais.
Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja.