Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi kwa mwaka wa fedha 2016/2017.

Hon. Oran Manase Njeza

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbeya Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi kwa mwaka wa fedha 2016/2017.

MHE. ORAN M. NJEZA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana. Nami napenda kumpongeza Waziri wa Kilimo na Naibu wake na timu nzima ya Wizara ya Kilimo kwa kazi kubwa wanayoifanya na kukabiliana na changamoto zilizopo.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kweli kama walivyosema wenzangu, hii Bajeti ya Kilimo haijakaa vizuri. Asilimia 0.9 ya bajeti nzima ya Serikali kuipeleka kwenye kilimo, nafikiri hatuitendei haki Sekta hii ya Kilimo. Niliangalia vizuri sana Bajeti ya Mheshimiwa Waziri Mkuu ambayo ilikuwa na mabadiliko makubwa sana. Aliibadilisha kutoka asilimia 15 ya maendeleo mpaka asilimia 70 ya maendeleo. Sasa tulitegemea mabadiliko kama hayo yangekuwepo vilevile kwenye sekta hii muhimu ya kilimo.
Mheshimiwa Naibu Spika, suala la uzalishaji na tija ya kilimo linasababishwa sana na ufinyu wa bajeti ya kilimo. Ukiangalia, kama sisi tunaotoka kwenye maeneo ambayo ni ya kilimo, kwenye Wilaya ya Mbeya tunalima karibu mazao yote ya biashara na mazao ya chakula. Kabla ya mwaka 2010, Wilaya ya Mbeya ilikuwa ni mojawapo ya wazalishaji wakubwa sana wa pareto Tanzania na Afrika, lakini kwa leo hii zao hilo limeporomoka sana. Sababu kubwa ya kuporomoka kwa zao hilo ambalo lina soko zuri sana duniani ni ufuatiliaji na ubora na usimamizi mbovu.
Mheshimiwa Naibu Spika, soko halina uhakika kabisa! Watu waliopewa majukumu ya kulisimamia Soko la Pareto leo hii wameweza kuweka mnunuzi mmoja wa pareto na huyo mnunuzi ambaye ni mwekezaji ndio ana Kiwanda cha Pareto. Unategemea mkulima atafaidika namna gani kwa monopoly ya namna hii?
Mheshimiwa Naibu Spika, pareto ilipokuwa na wanunuzi wengi, wakulima walipata sh. 2,400/= kwa kilo. Leo hii wakulima wanapata sh. 1,500/=. Bei ya huko kwa wenzetu nchi nyingine ni sh. 4,000/= kwa kilo. Sasa unategemea maajabu gani kuitoa nchi hii katika huu umaskini wakati umaskini unazalishwa na sisi wenyewe? Angalia hiyo tofauti ya sh. 1,500/= na sh. 4,000/=. Ukiweza kuibadilisha tu hiyo, ni kwamba uchumi wetu utakuwa umebadilika kwa zaidi ya asilimia 200.
Mheshimiwa Naibu Spika, nami namwomba Waziri na nashukuru alikuwa amelifanyia kazi suala hili, lakini inavyoelekea kuna matatizo kwenye Bodi ya Pareto. Uliagiza kuwa wakutanishwe wanunuzi wadogo na yule mwekezaji (PST) pamoja na wakulima, lakini mpaka leo, licha ya kwamba Waziri Mkuu vilevile alisimamia suala hilo, hawajakutana na hawataki kuwakutanisha hawa watu.
Mheshimiwa Naibu Spika, sasa kama tuna bodi tunazozisimamia, hazipokei maagizo kutoka juu, tunategemea nini? Nafikiri Mheshimiwa Waziri inabidi uangalie ni namna gani utalishughulikia hili suala. Hali hii inakatisha tamaa wakulima, nami mwenyewe kama ni mkulima, nasikitika kuona wakulima wa Mbeya wanapata sh. 1,500/= na soko huko nje wanapata sh. 4,000/=, kisa ni utendaji mbovu wa Bodi ya Pareto. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, ukiangalia huu uzalishaji wetu, tulikuwa tunaongoza duniani; nchi zetu hizi tatu za Afrika Mashariki ikiwemo Kenya, Rwanda na Tanzania. Tulikuwa tunazalisha zaidi ya asilimia 70 ya pareto inayozalishwa duniani. Leo hii baada ya haya matatizo, kisiwa kidogo cha Tasmania huko Australia ndiyo kinazalisha zaidi ya asilimia 70 ya pareto na wenzetu kule wanapata zaidi ya sh. 4,000/= kwa kilo.
Mheshimiwa Naibu Spika, nafikiri tuanze kuangalia ni namna gani tunasimamia sera zetu na strategic objectives tulizonazo ili tukishazitatua hizo, nafikiri badala ya kuongeza maeneo ya kilimo, tuangalie ni namna gani haya maeneo yetu tuliyonayo sasa hivi yatatoa mazao yetu ya kilimo kwa tija zaidi na kabla ya kuongeza maeneo ya kilimo.
MHE. ORAN M. NJEZA: Mheshimiwa Naibu Spika, ukiangalia kule kwangu, Wilaya ya Mbeya…
NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Njeza muda wako tayari!
MHE. ORAN M. NJEZA: Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja kwa asilimia mia moja. Ahsante.