Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano

Hon. Daniel Edward Mtuka

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Manyoni Mashariki

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano

MHE. DANIEL E. MTUKA: Ahsante.

Mheshimiwa Naibu Spika, na mimi nashukuru kwa nafasi hii fupi, lakini nitajitahidi kujikita kwa harakaharaka kutoa mchango wangu katika Wizara hii ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano.

Kwanza nampongeza Mheshimiwa Rais kwa kazi kubwa anayoifanya, Watanzania wote wanaona. Pia niwapongeze Mawaziri wanaohusika na Wizara hii, Mheshimiwa Profesa Mbarawa na ndugu yangu Mheshimiwa Kwandikwa, tunaona juhudi zao na wanavyochapa kazi kuwatumikia Watanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nitoe shukrani zangu baada ya kutizama kitabu hiki cha bajeti, Jimbo langu la Manyoni tumetengewa fedha katika barabara za Ikungi – Londoni – Kilimatinde; Manyoni – Heka – Ikasi; Heka – Iluma na pia Daraja kubwa la Sanza nalo limetengewa pesa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, labda niombe ufafanuzi tu kidogo hapo kwenye barabara ya Ikungi – Londoni – Kilimatinde. Katika ukurasa wa 221, nimeona kuna barabara kama mbili tofauti, kuna moja imeandikwa Ikungi – Londoni – Kilimatinde na nyingine imeandikwa Ikungi – Kilimatinde. Mimi naona hicho ni kitu kimoja, lakini naona wametenganisha na fedha zimetengwa kwa kila kipande shilingi milioni 60. Kama ni kitu kimoja basi ile pesa msiitoe, iunganisheni tu basi nipate shilingi milioni 120. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nizungumzie mawasiliano ya simu. Wilaya ya Manyoni imekuwa na tatizo kubwa sana la mtandao wa simu, lakini naishukuru Serikali kwa kiasi imejitahidi sana kutujengea mitandao. Niombe kasi ya Kampuni ya Halotel ambao wamepewa tender hii hebu wafanye haraka, ni mwaka mzima sasa kwa mfano sehemu za Asasilo, Mpapa, Sanza na Nkonko minara wameweka tu misingi, hawaja-erect ile minara na kuwasha simu kwa mwaka mzima sasa. Naomba wahimizwe basi wajenge ile minara na kuwasha ili tuweze kuanza kuwasiliana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pia maeneo ambayo hayasikiki kabisa katika jimbo langu ni vijiji vya Hika, Igwamadete, Mangoli, Mafurungu, Simbangulu, Imalampaka, havina kabisa mawasiliano. Ukifika katika eneo hili unakuwa kama uko katika kisiwa. Kampuni ya Halotel tunaomba sana Mheshimiwa Waziri awahimize kwa sababu ndiyo waliopata tender na wamezuia wengine, wafanye haraka basi sisi tunahitaji mawasiliano. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, upande wa reli, nizungumzie kidogo suala la reli ya Singida – Manyoni. Reli hii ilifunguliwa tarehe 24 Oktoba, 1985, ilikuwa kwa ajili ya kusafirisha mazao ya pamba na ngano kule Basuto pamoja na kuwasafirisha abiria na ilianza ku-operate vizuri sana ilikuwa na mabehewa matatu, mabehewa ya abiria mawili na la mizigo moja, ilitusaidia sana kipindi kile. Cha ajabu nilishuhudia tarehe 9 Septemba, 2009 ndiyo ilikuwa safari ya mwisho kusafiri lakini tarehe 12 Septemba, 2009 safari hizi zilisitishwa rasmi tukawa hatuna treni tena. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Waziri anayehusika tunaiomba treni yetu ya Singida kwa sababu mlisema kwamba tumesitisha safari eti kwa sababu ya ujio wa lami na pamba hailimwi tena. Sasa hivi sababu hizo hazina msingi wowote kwa sababu mtu anaposafiri analinganisha gharama za usafirishaji. Sasa hivi tunajenga Daraja la Sibiti, tutapata mizigo kutoka Simiyu na maeneo mengi ya Singida pale, tunalima vitunguu, tunao kuku, tunayo miwa, tuna viazi, tunaomba sana mturudishie treni ile, Mwalimu Nyerere hakukosea kutuletea treni ile. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pia katika ujenzi wa standard gauge, msiisahau hii reli. Ifungueni ianze ku-operate sasa hivi, lakini standard gauge itakapoanza kujengwa reli hii pia ikumbukwe, mtujengee standard gauge, tunahitaji sana hii treni. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nizungumzie ajali zinazotokea sana kwenye mteremko wa Mbwasa pale Chikuyu. Kumekuwa na ajali nyingi sana pale Mbwasa na pale Sekenke. Mimi kama mtaalam wa mambo haya ya ujenzi wa barabara nilipoangalia pale kuna makosa ya design.

Naomba sana Mheshimiwa Waziri atume wataalam pale waende Mbwasa na Sekenke waka-design upya, wanyooshe zile kona maana kuna mteremko halafu kuna kona ghafla. Lori linapo-fail pale huwezi kukata kona ukikata kona ghafla unalipiga ngwala lile lori lazima litaanguka tu.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba waka-design upya ili wanyooshe zile barabara ziteremke pale chini halafu kona isiwe kali sana. Hili linawezekana mimi kama mtaalam nimepita, nimeona kuna uwezekano kabisa wa kufanya marekebisho kuepusha ajali hizi, tunapoteza maisha ya watu wengi.

Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa nafasi hii, ahsante.