Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano

Hon. Bupe Nelson Mwakang'ata

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano

MHE. BUPE N. MWAKANG’ATA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa nafasi ili nami niweze kuchangia katika Wizara hii ya Ujenzi. Awali ya yote, namshukuru Mwenyezi Mungu kwa kutujalia uzima, nasi kuweza kuchangia katika Wizara hizi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nichukue fursa hii kumpongeza Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli kwa kazi kubwa anazozifanya. Mwenye macho haambiwi tazama; na mnyonge mnyongeni, lakini haki yake mpeni. Mheshimiwa Dkt. Magufuli Mungu yupo pamoja nawe, pamoja na Serikali yako, pigeni kazi. Watanzania wote wako nyuma yenu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nampongeze pia Waziri wa Ujenzi, Mheshimiwa Profesa Mbarawa pamoja na Naibu Mawaziri wake wote wawili kwa kazi kubwa wanazozifanya. Hakika Wizara hii wanaitendea haki. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nijielekeze sasa kwenye suala la Uwanja wa Ndege wa Sumbawanga. Kwanza kabisa naishukuru sana Serikali kwa kutenga fedha. Nimeona katika ukurasa wa 154 zimetengwa fedha karibu shilingi bilioni 12 kwa ajili ya Uwanja wa Sumbawanga wa Mkoa wa Rukwa. Pamoja na shukrani hizi, bado nina hoja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, watu wanaouzunguka uwanja, wananchi wa Mkoa wa Rukwa walifanyiwa tathmini ya muda mrefu. Tumepiga kelele sana; Mheshimiwa Aeshi, Mbunge wa Jimbo la Sumbawanga Mjini amepiga kelele sana hapa, lakini bado wananchi wale hawajalipwa. Bajeti ya mwaka 2017 pesa zilitengwa, lakini wananchi hawakulipwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na mambo yote Serikali inayofanya, naomba sana katika fedha hizi zilizotengwa kipaumbele kiwe kuwalipa kwanza wale wananchi. Wanatia huruma sana wale wananchi. Wengine wamekufa wameacha watoto yatima.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nyumba zile hawawezi tena kuchukulia mikopo, zimebaki tu zimewekwa X. Katika hii fedha iliyotengwa, pamoja na kwamba Serikali inakwenda kujenga uwanja, lakini ichukue kipaumbele kwanza cha kuwalipa wale wananchi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naipongeza Serikali yangu na Mheshimiwa Waziri kwa kununua ndege. Ni kazi kubwa sana waliyofanya Serikali, lakini pamoja na ununuzi wa ndege naipongeza sana Serikali yangu ya Chama cha Mapinduzi. Tunaomba Mkoa wa Rukwa hizi Bombardier nasi tupate angalau route kwa wiki hata mara moja, Bombardier ishuke pale Rukwa, wananchi wafurahie matunda ya Rais wao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nijielekeze sasa kwenye suala la barabara. Naipongeza sana Wizara, inafanya mambo mengi makubwa, lakini bado barabara ya kutoka Sumbawanga Mjini kwenda Kala. Ile barabara imekatika kabisa, yaani wananchi sasa hivi magari yakifika pale kwenye daraja wanapeana zamu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, bado barabara ya kutoka Katongolo kwenda Namansi, imekatika; barabara ya kutoka Marongwa kwenda Kasura Junction imekatika; na barabara ya kutoka Nkana – Kala imekatika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mkoa wa Rukwa Jimbo la Nkasi Kusini kwa Mheshimiwa Mipata hali ni mbaya sana. Mheshimiwa Mipata amekuwa akihangaika sana kutafuta hata pesa za dharura, lakini imeshindikana. Tunaomba watuangalie, watoe hata pesa za dharura ili kutengeneza hizi barabara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara zimekatika kabisa.

T A A R I F A . . .

MHE. BUPE N. MWAKANG’ATA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nimeipokea kwa mikono miwili, tena namshukuru sana kwa kunisaidia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hizi barabara yaani tuna hali mbaya sana. Ninavyosema hivi, Mheshimiwa Mipata ameomba pesa ya dharura mpaka sasa hivi bado hajapata majibu. Wananchi kule wanampigia simu, wanapiga simu kwa Wabunge wote lakini hakuna majibu. Tunaomba sana angalau TARURA au Wizara itoe pesa za dharura ili barabara hizi na haya madaraja yajengwe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nijielekeze sasa kwenye mtandao. Wilaya ya Nkasi tunashukuru Serikali ilituletea mtandao katika Kata ya Wampembe, lakini bado Kata za Kala, Sintari, Ninde, wananchi wanapanda kwenye mti, hasa wanawake usipovaa bukta sasa unapandaje kwenye mti ili ukaongee na simu? Wanakwenda kwenye milima, vichuguu kwenda kuongea na simu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaomba Wizara hii iliangalie hili suala watuletee mtandao kwenye hizi Kata. Wanawake tunashindwa sasa kupanda kwenye ile miti maana miti mingine ni mirefu, mtandao unapatikana juu kabisa. Kwa hiyo, suala hili lichukuliwe kwa umuhimu wake. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niongelee barabara za hapa Dodoma. Sisi tunaokaa Area D, barabara zinazotoka kwenye yale maghorofa wanayokaa Wabunge zimeharibika sana kiasi kwamba wakati mwingine tunaweza tukapata ajali hapa hapa mjini. Tunapita hii njia ya kwenda Morogoro tunakatisha kwenye vichochoro mpaka tukafike kule Area D Sengia unakuwa umepata shida sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaomba wangetufungulia japo kwa muda tuwe tunakatisha pale kwenye uwanja ule wa ndege ambao wamefunga, sisi Wabunge tuwe tunapita kwa muda kwa sababu tunavyopita kwenye vichochoro tunaweza tukakabwa. Vile vichochoro tunapita kwenye nyumba za watu, kwenye milango. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia zile nyumba za TBA zimechoka, TBA hawazifanyii ukarabati. Sisi tunaoishi kwenye zile nyumba tunapata shida. TBA waje watufanyie ukarabati zile nyumba, tunalipa kodi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni hayo, nashukuru sana na naunga mkono hoja.