Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano

Hon. Edward Franz Mwalongo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Njombe Mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano

MHE. EDWARD F. MWALONGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Awali ya yote, namshukuru sana Mwenyezi Mungu mwingi wa rehema, mpaji wa yote kwa kutujalia Wabunge wote kuwemo humu ndani na tunaendelea na kazi yetu vizuri. Pia nawapongeza sana watendaji wote wa Serikali, akiwemo Rais wetu na Mawaziri na wote wanaowasaidia kutimiza majukumu yao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikizungumzia suala la ujenzi kwanza kabisa niseme kwamba kwa kweli nasikitishwa sana na jinsi bajeti ilivyowekwa katika Mkoa wa Njombe na hasa katika barabara ya Itoni – Manda. Barabara hii ni miaka mingi sana imekuwa ikiahidiwa itawekewa lami na kipande cha kilometa 50 kimeshaanza kuwekewa lami ndani ya Wilaya ya Ludewa lakini hakisongi mbele.

Mheshimiwa Mwenyekiti, fedha inayotolewa ni ndogo sana kiasi ambacho kazi haiendi na maeneo yale ni ya uzalishaji mkubwa na ndiyo ghala la chakula kwa ajili ya wananchi wa nchi hii. Kwa hiyo, niiombe sana Serikali, hebu iwe serious, tunaposema tunataka kutengeneza barabara ya lami kwa ajili ya kuleta maendeleo katika maeneo yetu, basi iwekwe fedha ya kutosha na kazi iweze kwenda vizuri.
(Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ambalo napenda kuliongelea ni barabara za mijini ambazo TANROADS huwa inajenga. Njombe Mjini ni Makao Makuu ya Mkoa, tumetengenezewa barabara ya lami mita 150. Sasa ukiangalia mobilisation ya vifaa vya lami kwenda wilayani au mkoani kama Njombe halafu vinakuja kufanya kazi ya mita 150 ni upotevu wa fedha. Siyo kwamba tunakataa tusitengenezewe, lakini hebu wabadilishe utaratibu huo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Makao Makuu ya Mkoa barabara haziridhishi kabisa lakini zinakuja kutengenezwa mita 150, mkandarasi anakuja pale kwa ajili ya barabara ya mita 150, anasafirisha grader, roller, escalator, malori na mashine za kumimina lami, anakuja kufanya kazi ya mita 150, hii inasababisha barabara iwe ya ghali sana. Kwa hiyo, niombe sana Njombe tutengenezewe barabara za mjini kwa sababu ni Makao Makuu ya Mkoa na hali ya barabara za mjini ni mbaya sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ni uwanja wa ndege. Nimeona wanasema kwenye viwanja vya ndege ambavyo vimo na Njombe imo. Naomba Mheshimiwa Waziri atakapokuja hapa nataka asema mipaka ya uwanja wa ndege iko wapi? Wananchi wale wanaozunguka uwanja wa ndege wa Njombe wanastahili nini? Wahame, waendelee kuwepo, watawalipwa fidia au wapime nyumba zao zile waendelee kuishi?

Mheshimiwa Mwenyekiti, nasema hivyo kwa sababu siku zote wananchi wale wa Njombe wamekuwa hawaelewi, wanaishi kwenye sintofahamu. Wanashindwa kuendeleza maeneo yao, hawapimiwi na uwanja wa ndege hawatoi taarifa yoyote. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na hayo ule uwanja wa ndege ni pori na unatusababishia vibaka pale mjini.

Niwaombe sana wakija hapa keshokutwa kuhitimisha bajeti yao waseme uwanja wa ndege wameshafyeka majani yote ndani ya uwanja hayapo. Kwanza uwanja wenyewe uko mjini, hawausafishi, wanatusababishia mji uwe mchafu. Vibaka wanatoka pale wanasumbua watu mtaani lakini vilevile wamefanya kama ndiyo dampo kwa ajili ya kutupa uchafu mbalimbali katika uwanja wa ndege. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine, Mheshimiwa Waziri anajitahidi sana kujenga barabara, lakini nimefanya utafiti mdogo, Jeshi la Polisi, Idara ya Trafiki wanabomoa barabara. Wanasimamisha malori mahali ambapo sio mahali maalum pa kusimamisha lori, matokeo yake barabara inamegeka mabega kidogo kidogo, wakiona pameshakuwa na mashimo pamemegeka sana wanahama wanaenda kuanzisha kituo mahali pengine. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naomba Wizara ya Ujenzi wakae na Wizara ya Mambo ya Ndani wakubaliane Police Traffic watasimama wapi na watasimamisha magari wapi kwa sababu hii ni hasara kwa nchi. Kama sehemu za vivuko vya ng’ombe tumeandaa mazingira maalum kwamba ng’ombe wavuke mahali fulani, kwa nini malori yasiandaliwe mahali pa kusimamishwa? Wanaamua tu kwamba leo tusimame hapa, leo tusimame hapa, malori yanasimamishwa yanakwenda kandokando ya barabara yanaharibu barabara. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, yangu ni hayo, lakini naomba sana barabara za Mji wa Njombe ziangaliwe.