Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

Hon. Shabani Omari Shekilindi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Lushoto

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

MHE. SHAABANI O. SHEKILINDI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nimpongeze Waziri Ummy pamoja na Naibu Waziri wake pamoja na timu yote kwa ujumla kwa kazi kubwa wanayoifanya ya kuwatumikia Watanzania bila kuchoka. Mwenyezi Mungu atawalipa ujira wao huo.

Mheshimiwa Naibu Spika, Jimbo la Lushoto kuna Kituo cha Afya kimoja tu ambacho kipo Mlola na kituo kinahudumia zaidi ya kata nane, na hii imepelekea mrundikano wa wagonjwa. Hivyo basi niiombe Serikali yangu tukufu ipandishe hadhi Zahanati ya Makanya kuwa Kituo cha Afya kwani hii itapunguza mrundikano wa wagonjwa na kuokoa vifo vya wananchi hasa vifo vya mama na watoto.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna changamoto kubwa sana ya gari la wagonjwa katika Kituo cha Afya Mlola. Niiombe Serikali yangu katika bajeti hii mtutengee pesa kwa ajili ya kununua gari la wagonjwa kwani tunapoteza wananchi wengi hasa akina mama wajawazito pale wanapohitaji usafiri kwenda katika Hospitali ya Wilaya na kama unavyojua miundombinu yetu ya barabara sio mizuri kabisa. Kwa hiyo kunahitajika gari la wagonjwa ambalo ni kwa ajili ya kubebea wagonjwa tu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kama nilivyosema kuwa Jimbo la Lushoto kuna kituo cha afya kimoja lakini wananchi wamejitolea na kuanza kujenga vituo vya afya viwili ambavyo ni Kituo cha Afya Gare na Kituo cha Afya Ngwelo. Hivyo basi, naomba safari hii Serikali ivitengee pesa ambazo zitatosha kumalizia vituo hivyo ili kupunguza msongamano katika Hospitali ya Wilaya na ni pamoja na kuendelea kuokoa vifo vya mama na mtoto ukizingatia vituo hivi vipo mbali na Hospitali ya Wilaya.

Mheshimiwa Naibu Spika, zipo changamoto za vifaatiba katika Hospitali ya Wilaya ya Lushoto ambavyo ni ultra sound, x-ray machine ni ndogo haina uwezo. Kwa hiyo, inaharibika mara kwa mara hii imepelekea wagonjwa wengi kukosa huduma na kupata usumbufu wa kwenda na kurudi na ukizingatia wagonjwa wengi wanatoka mbali. Kwa hiyo, niiombe Serikali ipeleke vifaa hivyo ili kuokoa vifo vya wananchi ambavyo vinaweza kuzuilika.

Mheshimiwa Naibu Spika, suala zima la watumishi katika kada ya afya, niiombe Serikali ipeleke watumishi wa kutosha katika zahanati zetu pamoja na vituo vya afya pamoja na Hospitali ya Wilaya. Wananchi wengi wamejenga zahanati kwa nguvu zao mpaka nyingine zimeisha, lakini watumishi ni shida mpaka zahanati hizi kuelekea kuwa magofu na hii inapelekea kuwavunja nguvu na kuwakatisha tamaa. Naomba Serikali iajiri watumishi haraka iwezekanavyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, ni ukweli usiofichika kuwa katika vituo vyetu vya afya na katika hospitali zetu za wilaya chanjo ya kichaa cha mbwa ni gharama, na siyo gharama tu pia haipatikani. Kwa hiyo, niiombe Serikali ipeleke chanjo hiyo ya kichaa cha mbwa katika hospitali zetu pamoja na vituo vya afya mpaka kwenye zahanati ili kuokoa wananchi wanaopata ajali ya kung’atwa na mbwa. Tumekosa na kupoteza wananchi wengi waliopata ajali hizo za kung’atwa na mbwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, dawa muhimu hazifiki kwenye zahanati zetu vituo vya afya pamoja na hospitali ya wilaya, kwa mfano dawa za kisukari hizi ndio kabisa. Mimi kama Mbunge nimepata malalamiko mengi sana hasa kwa wale wazee ambao wanatibiwa bure. Niishauri na kuiomba Serikali yangu ipeleke dawa hizi muhimu hasa katika zahanati, vituo vya afya na katika hospitali zetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, mwisho naunga mkono hoja kwa asilimia mia moja.