Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

Hon. Daimu Iddi Mpakate

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Tunduru Kusini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

MHE. DAIMU I. MPAKATE: Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kuchangia hotuba Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, nianze na upungufu wa vituo vya afya; Halmashauri ya Wilaya ya Tunduru ina jumla ya kata 39 lakini tuna vituo vya afya vitano tu na zahanati 57 kati ya vijiji 167. Hali hii inadhoofisha utoaji wa huduma ya afya kwa akina mama na watoto. Akina mama wajawazito wanalazimika kutembea umbali wa zaidi ya kilometa 10 kufuata huduma za afya. Hivyo, tunaomba Serikali itupie jicho Wilaya hii ya Tunduru kutokana na uchache wa vituo vya afya na zahanati. Jitihada za Halmashauri ya Wilaya zinagonga mwamba kutokana na ukubwa wa eneo pamoja na makusanyo madogo ya mapato ya ndani. Hata hivyo, kuna upungufu mkubwa wa watumishi katika sekta ya afya; zahanati nyingi zina wahudumu si zaidi ya wawili, nyingine zina mhudumu mmoja tu, jambo ambalo linadhoofisha utoaji wa huduma za afya kwa wananchi.

Mheshimiwa Naibu Spika, ahadi ya muda mrefu ya Rais wa Awamu ya Nne Mheshimiwa Jakaya Mrisho Kikwete mwaka 2014 alitoa ahadi ya kujenga kituo cha afya katika Kijiji cha Nalasi chenye wakazi zaidi ya 50,000 katika mgawanyo wa vijiji vinne. Jambo hili limekuwa ni kero kubwa sana, wananchi walijitolea kufyatua tofali na Halmashauri ilitoa shilingi 80,000,000 mwaka 2015 lakini fedha hizo ziliishia kujenga foundation tu, pamoja na uwepo wa matofali yale mpaka leo hakuna kilichoendelea. Halmashauri imejitahidi kutenga shilingi milioni 100 kila mwaka lakini upatikanaji wa fedha umekuwa mgumu sana. Hivyo ninaiomba Serikali kutekeleza ahadi hii ya muda mrefu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu ahadi ya muda mrefu ya gari la wagonjwa; Rais wa Awamu ya Nne alitoa ahadi ya kutoa gari katika Kituo cha Afya Mchoteka mwaka 2014 lakini hadi hivi leo ahadi hiyo haijatekelezwa. Ninaomba Serikali kuona umuhimu wa kutekeleza ahadi hii kwani kituo hiki cha afya kipo umbali wa kilometa 80 kutoka ilipo Hospitali ya Wilaya.

Mheshimiwa Naibu Spika, Kituo cha Afya Mtina kimejengwa mwaka 1970, majengo yake ni machakavu na hakuna wodi ya akina mama na watoto; haina maabara wala theater (chumba cha upasuaji) na kituo hiki kinahudumia Kata nne; Lukumbule, Mchesi, Tumemado na Kata ya Mtina yenyewe; zaidi ya wananchi 80,000 wanahudumiwa katika kituo hiki. Hivyo, ninaiomba Serikali kutoa fedha kuongeza huduma za afya kama ilivyo katika vituo vingine vilivyoongezewa majengo ili kutoa huduma ya malazi, upasuaji na huduma ya maabara.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika Jimbo la Tunduru Kusini kuna Hospitali ya Mission ya Mbesa ambayo inategemewa takribani na wananchi zaidi ya 200,000. Rais wa Awamu ya Nne alitoa ahadi ya kuifanya hospitali hii kuwa Hospitali Teule ya Wilaya lakini mpaka leo ahadi hiyo haijatekelezwa pamoja na kwamba Halmashauri inapeleka watumishi katika hospitali ile ili kusaidia kutoa huduma kwa wananchi kama ilivyo katika hospitali nyingine teule zilizopo maeneo mengine.

Mheshimiwa Naibu Spika, Hospitali ya Wilaya ina gari bovu sana la wagonjwa na ukizingatia Wilaya ile ni kubwa sana, hivyo, tunaomba gari la wagonjwa.