Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

Hon. Kasuku Samson Bilago

Sex

Male

Party

CHADEMA

Constituent

Buyungu

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

MHE. KASUKU S. BILAGO: Mheshimiwa Naibu Spika, ugonjwa wa tezi dume umeonekana kuongezeka sana nchini. Tatizo kubwa ni operation zinazofanyika, lazima mgonjwa afanyiwe mara mbili. Aidha, hata wanaofanyiwa operation wengi wanakufa.

Ushauri wangu madaktari waongezewe ujuzi nje ya nchi na ikibidi vifaatiba vya kisasa vipatikane kuokoa wanaume hawa.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu ajira ya watumishi sekta ya afya; Mkoa wa Kigoma una upungufu wa watumishi wa afya wapatao asilimia 70 hali ambayo inatishia uhai wa watu wa Kigoma. Aidha, nchi nzima kuna upungufu mkubwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, ushauri wangu Serikali ichukue hatua za makusudi kuajiri watumishi hao ila kila zahanati iwe na CO/CA, vituo vya afya viwe na daktari mmoja na CO , hii itasaidia kupunguza vifo vya akina mama wajawazito na watoto.

Mheshimiwa Naibu Spika, suala la matibabu ya wazee; sera ya wazee kutibiwa bure bado inasuasua sana kwani sehemu nyingi wazee hawa hawapati matibabu bure. Aidha, vitambulisho vimekuwa shida kupatikana. Ni vyema vitambulisho vikatolewa kwa wazee hawa wenye umri wa miaka 60+.

Mheshimiwa Naibu Spika, ushauri wangu ni kuwa Wizara iwasiliane na TAMISEMI ili wazee wote wapewe vitambulisho ili wapate matibabu bure. NB: Vitambulisho vitolewe bure.

Mheshimiwa Naibu Spika, miradi ya Engender Health na Bloomberg; miradi hii iko Mkoa wa Kigoma na inatarajiwa kufikia ukomo/mwisho Aprili, 2019. Huduma nyingi zinazofanyika Mkoani na Wilaya zote ni huduma ya mama, baba na mtoto. Mfano, vituo vitano kila Wilaya vilivyojengwa vimewekewa vifaatiba vya kisasa lakini hakuna wataalam wa vituo hivyo hasa Jimbo la Buyungu (Kakonko). Ni aibu kwa Serikali yetu kupewa msaada wa majengo na mfadhili kisha Serikali inashindwa kuweka/kuajiri wataalam wenye ujuzi wa kutosha.

Mheshimiwa Naibu Spika, ni ushauri wangu kuwa vituo hivi vipewe vipaumbele na Wizara itafute ufadhili utakaosaidia miradi hii iendelee kutoa huduma (sustainability).

Mheshimiwa Naibu Spika, kinga ni bora kuliko tiba; Wizara ya Afya ijiimarishe kwenye kampeni ya kinga ili iepuke kutumia fedha nyingi za tiba. Kampeni ya kutumia tv, redio, michezo/maonesho/sanaa na kadhalika, vipindi kama chakula bora (kuleni chakula bora, mboga, samaki, maziwa na kadhalika), kampeni ya kunawa mikono baada ya kutoka chooni, kuchemsha maji; mabwana na mabibi afya wafanye kazi kukagua usafi majumbani (karo, vyoo safi na kadhalika).