Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

Hon. Ridhiwani Jakaya Kikwete

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Chalinze

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

MHE. RIDHIWANI J. KIKWETE: Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kumshukuru Mungu na kumtakia rehema, kiongozi wa umma, nimshukuru sana Mheshimiwa Rais, Makamu wa Rais, Waziri Mkuu na wasaidizi wao ukiwemo wewe Mheshimiwa Waziri, Naibu Waziri na wasaidizi wenu kwa kazi nzuri mnayoifanya.

Mheshimiwa Naibu Spika, kazi kubwa imefanyika na inaendelea kufanyika. Pamoja na juhudi nzuri na kubwa ambazo zimekwishafanyika kama ujenzi wa Hospitali ya Mloganzila, upatikanaji wa vifaa na dawa, magari ya kubeba wagonjwa na dawa, lakini ukweli changamoto hasa kwa sisi wenye majimbo ya vijiji tumeendelea kupata taabu na changamoto nyingi sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika Halmashauri yetu ya Chalinze, hitaji la wauguzi na waganga kwa ajili ya kutoa huduma za kitabibu imeendelea kuwa changamoto. Mfano, katika Kituo cha Afya Kibindu kuna daktari mmoja tu; yeye asikilize mgonjwa, achome sindano, agawe dawa na hata pia atoe ushauri nasaha. Hapo sizungumzii wakati anatibu mgonjwa wa malaria au surua akaja mama mjamzito anayehitaji kujifungua.

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na juhudi kubwa, bado tunahitaji kubwa la waganga hasa katika vituo vya afya Kibindu, Miono, Msata, Lugoba, Vigwaza, Ubena na maeneo mengine yanayofanana na shida hii ya Halmashauri yetu ya Chalinze.

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na juhudi kubwa zinazofanyika na zinazofanywa na Halmashauri yetu ya Chalinze ya kujenga nyumba za waganga, natumia nafasi hii kuishukuru Serikali kwa kutupatia fedha kiasi cha fedha halali shilingi milioni 750 kwa ujenzi wa vituo vya afya Lugoba na Kibindu. Licha ya juhudi hizo, ujenzi wa hospitali ya Wilaya ya Chalinze umeendelea kusuasua. Juhudi za Serikali ya Halmashauri ya wilaya ya Chalinze kumalizia zinazofanyika.

Mfano pesa kiasi milioni 50 zimetengwa, lakini ukweli nguvu hii inahitaji mkono wa Serikali kumalizia mapema.

Mheshimiwa Naibu Spika, kukamilika kwa hospitali hii kutapunguza rufaa zinazokwenda Kibaha na Bagamoyo hivyo kupunguza wingi au Lundo la wagonjwa katika hospitali hiyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, hivi karibuni tumeshuhudia zoezi lililoendelea pale Dar es Salaam ambalo kwa ukweli kabisa kumekuwa na uvunjifu mkubwa wa maadili na sheria ambazo zimesababisha hata heshima za watu kuvunjwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa upande mwingine zoezi hili limeibua changamoto ya kuonesha kuwa kuna walakini katika taasisi zetu za kiutendaji. Hapa nakusudia Taasisi au Idara ya Ustawi wa Jamii. Taasisi hii ilikuwa wapi kufanya haya? Je, mfumo gani wanatumia kufanya kazi? Je, kwa nini hawatoi elimu kwa wananchi?

Mheshimiwa Naibu Spika, katika Halmashauri ya Chalinze, miaka 13 iliyopita tulikubaliana kujenga shule za sekondari za kata. Katika makubaliano hayo, ujenzi wa mabweni kwa ajili ya kuwalaza vijana wetu wa kike na wa kiume ulikubaliwa. Matatizo makubwa hasa kwa watoto wa kike wanaoishi kwenye mabweni yamekuwapo kipindi wanapoingia kwenye siku zao za hedhi.

Mheshimiwa Naibu Spika, ni ombi kwa Serikali, kutokana na hali ngumu za maisha za wazazi wetu na hali ya malezi, niombe Serikali ikubali kuondoa kodi kwenye taulo hizi ili kuwezesha lengo la milenia la kumuelimisha mtoto wa kike kutimia.

Mheshimiwa Naibu Spika, Halmashauri ya Chalinze kijiografia ni jimbo pana sana na hata wakati mwingine huchukua umbali mrefu sana toka point moja ya Halmashauri kwenda point nyingine. Umbali huo umekuwa ni kero hasa kutokana na mapungufu ya magari ya kubebea wagonjwa kuwatoa zahanati au nyumbani/vijijini hadi kwenye hospitali au kituo cha afya. Pamoja na hili hakuna gari la chanjo la Wilaya. Tunaomba gari la wagonjwa kwa Kituo cha Afya Lugoba na Kwaruhombo.

Mheshimiwa Naibu Spika, nimalizie kwa kumkumbusha Mheshimiwa Waziri, ombi la Halmashauri kuhusu kuongezewa waganga ili kupambana na mapungufu yaliyopo sasa limeendelea kuwapo. Kwa sasa watumishi waliopo ni asilimia 30 ya mahitaji halisi. Kwa taarifa hadi sasa zipo zahanati ambazo zinaongozwa na wahudumu wa afya na hili limesababisha kushindikana kufunguliwa kwa zahanati mpya zilizojengwa huko Magulumatari, Talawanda na Buyuni Vigwaza.

Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja tukafanye kazi sasa kutatua kero za afya Tanzania na hasa Chalinze.