Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

Hon. Innocent Sebba Bilakwate

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kyerwa

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

MHE. INNOCENT S. BILAKWATE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuchangia Wizara hii muhimu. Kwanza nimshukuru Mwenyezi Mungu ambaye amenipa afya na nguvu kuendelea kuwatumikia wananchi wangu wa Jimbo la Kyerwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, nichukue nafasi hii kuendelea kumpongeza Jemedari wetu Mheshimiwa John Pombe Magufuli pamoja na Waziri Mheshimiwa Ummy Mwalimu, Naibu Waziri na watendaji wote wa Wizara ya Afya kwa kazi nzuri wanayoifanya, hakika Serikali yetu imejipanga kuhakikisha inaboresha huduma za afya.

Mheshimiwa Naibu Spika, wako watu wengi wanabeza mara hakuna kilichofanyika sasa mimi ngoja niwaambie baada ya kuwasemea wananchi wangu wa Jimbo la Kyerwa ni nini kimefanyika Kyerwa. Wakati naingia hapa Bungeni nilikuwa nina kituo cha afya kimoja ambacho huduma zake hazikuwa nzuri kituo cha Nkwenda leo kimeboreshwa akina mama wanapata huduma ya upasuaji. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mwaka jana nimepokea shilingi milioni 700 kwa ajili ya Kituo cha Afya Mlongo, hiyo ni kazi nzuri inayofanywa na Serikali ya John Pombe Magufuli. Mwaka huu kwenye bajeti ya TAMISEMI nimepokea bilioni moja na milioni mia tano (1,500,000,000) kwa ajili ya hospitali ya Wilaya, nani kama John Pombe Magufuli?

Mheshimiwa Naibu Spika, hizi ni kazi nzuri zinazofanywa na Serikali ya John Pombe Magufuli, wenye macho wanaona na wenye masikio wanasikia. Pamoja na kazi hizi zinazofanyika bado tunazo changamoto za watumishi, niendelee kuiomba sana Serikali yetu, Kyerwa watumishi wa afya ni wachache sana, ninaomba tunapotoa mgao kama Serikali na Kyerwa muiangalie. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niipongeze Serikali kwa ajili ya huduma za matibabu ya kibingwa, kwa kweli tumepiga hatua nzuri sana. Mimi nimefika pale Muhimbili kwenye Hospitali ya Jakaya Mrisho Kikwete ya Moyo, kwa kweli wanafanya kazi nzuri sana inatia moyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, mambo haya tulikuwa tunasikia yanafanyika nje, lakini leo tunaona yanafanyika Tanzania, nimpongeze Daktari wetu Profesa Janabi, lakini na madaktari wengine ambao wanaboresha huduma za afya. Ninachoiomba Serikali yangu sikivu tujitahidi kama tunavyofanya maamuzi magumu kwenye mambo mengine, hebu tufanye maamuzi magumu kuboresha huduma za afya kwa upande wa matibabu ya kibingwa ili tuweze kuokoa pesa nyingi zinazoenda nje ya Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mwaka huu nilimpeleka Mzee wangu India, Watanzania ni wengi wanaotibiwa India na wanatumia gharama kubwa sana. Kama mtu mmoja tuliweza kutumia zaidi ya milioni 30 kuna mama mmoja alikuwa anafanyiwa upasuaji pale Hospitali ya Apollo anahitaji zaidi ya dola 30,000 hizi pesa zote tukiboresha huduma za afya zitaingia Tanzania na tutaongeza kipato cha Wizara ya Afya. Ninaiomba sana Serikali iongeze vifaa, iongeze nguvu ninaamini tunao wataalam wengi sana lakini tatizo bado vifaa havitoshi kuweza kuboresha huduma hizi.

Mheshimiwa Naibu Spika, niongelee suala la upatikanaji wa madawa. Kwa kweli Serikali inafanya kazi nzuri, tumetoka bilioni 30 leo tunaongelea bilioni 200, ni kazi kubwa inayofanyika kwa kweli tuna kila sababu ya kuipongeza Serikali yetu kwa kuhakikisha inaboresha huduma za afya na Watanzania wanakaa sawa. Ninachoomba Mheshimiwa Ummy tumeona ukiongea na wadau mbalimbali hili jambo na lenyewe iwe ni sehemu ya kufanya maamuzi magumu ili tuweze kuwa na viwanda vya madawa hapa Tanzania na hii itasaidia, hizi pesa nyingi zinaenda nje lakini zingebaki ndani zingeweza kuboresha huduma za afya na ninaamini tutapiga hatua kubwa sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, niongelee suala la Bima ya Afya, hili suala ni jambo ambalo ni muhimu Watanzania hawawezi kuwa na pesa ya kujitibu, lakini tunapokuwa na bima ya afya itasaidia. Niiombe sana Serikali iongeze nguvu na waendelee kuwahamasisha Watanzania kila mmoja awe na bima ya afya, hii itasaidia sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo nakushukuru sana, naunga mkono hoja.