Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

Hon. Mariamu Nassoro Kisangi

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

MHE. MARIAM N. KISANGI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi nami niweze kuchangia. Kwanza namshukuru Mwenyezi Mungu kwa kuniweka salama na kuweza kuwa na afya njema kwa siku ya leo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza kwa umuhimu mkubwa napenda nimpongeze Mheshimiwa Rais wangu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Makamu wa Rais, Mheshimiwa Waziri Mkuu kwa utendaji wao mwema uliotukuka. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, napenda nitoe shukrani za dhati kwa Chama cha Mapinduzi - Mkoa wa Dar es Salaam kwa jinsi walivyopata shida, walivyohangaika na uchaguzi na hatimaye tukampata Mbunge mahiri, Mheshimiwa Mtulia wa Kinondoni. Kwa kweli ni jambo la kutukuka katika Mkoa wetu wa Dar es Salaam. Chama cha Mapinduzi kimepata nyongeza ya Mbunge, sasa tuko fifty-fifty. Ahsanteni sana akina mama wote wa Mkoa wa Dar es Salaam kwa jinsi mlivyowajibika katika kupata nyongeza ya Mbunge. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa naomba niende kwenye Wizara ya Afya. Napo napenda nimpongeze Mheshimiwa Waziri, Naibu Waziri, Makatibu Wakuu na watendaji wote wa Wizara ya Afya kwa kazi kubwa wanayoifanya kuwahudumia wananchi wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ni ukweli usiopingika huduma za afya katika Mkoa wa Dar es Salaam zimeimarika kwa kiwango kikubwa sana. Napenda niipongeze Serikali kwa jinsi ilivyoimarisha huduma ya afya ya mama na mtoto katika Mkoa wa Dar es Salaam. Nawapongeze sana Mheshimiwa Mkuu wa Mkoa, timu yake, Wakurugenzi na Wakuu wa Wilaya zote za Mkoa wa Dar es Salaam jinsi wanavyoshirikiana katika kuhakikisha wanaboresha huduma za afya ya mama na mtoto katika Mkoa wa Dar es Salaam. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, napenda nitoe shukrani za kipekee kwa Kampuni ya Armson Groups ambayo imeweza kutujengea Hospitali za Afya ya Mama na Mtoto katika Hospitali ya Amana, lakini wanatarajia kwenda Mwananyamala na Temeke pia. Nampongeza sana mfadhili huyu na ninamwambia fungu lako utalikuta kesho kwa Mwenyezi Mungu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, napenda nizungumzie juu ya huduma hizi zinazotolewa na Serikali, zizingatie idadi ya watu. Jimbo la Mbagala lina takribani idadi ya watu 1,100,000 lakini mpaka sasa hivi hospitali iliyopo ya Zakiem imezidiwa. Najua juhudi za Serikali wanataka kuboresha Hospitali ya Maji Matitu, lakini naiomba Serikali iiongezee pesa iwe hospitali kubwa. Idadi ya watu imezidi Mbagala na watu wanaongezeka kila siku. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia naiomba Serikali iangalie eneo la Mbande. Kama ilivyo wanafunzi wa shule, madarasa hayatoshi kila siku, lakini na idadi ya watu inakuwa ni wengi, akina mama ni wengi, huduma inayotakiwa ya afya kule ni kubwa. Wakati tunaangalia maeneo gani tupeleke huduma tuzingatie na idadi ya watu. Akina mama wa Mbande na wananchi wa Mbande ambako wanakutana na Mkoa wa Pwani na Wilaya ya Ilala, pamoja na kazi kubwa iliyofanywa na Serikali ya kuweka ile Hospitali ya Chanika, lakini bado hawa watu wa Mbande wanakuja Zakhiem na Temeke hivyo. Naiomba Serikali iangalie hilo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia niende kwenye Hospitali ya Mloganzila. Hospitali hii ni kubwa na nzuri, naipongeza sana Serikali, lakini bado ina upungufu wa madaktari na wauguzi. Wale ukifika pale unaambiwa mgonjwa wako huruhusiwi kumhudumia. Weka uji, weka maziwa hapo, lakini unakuta wodi nzima ina ma-nurse watatu, wagonjwa 50. Watawanyweshaje huo uji? Hata iweje, lazima kuna wengine watakosa huduma hiyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, kinachonishangaza, lengo la Serikali katika kuanzisha ile Hospitali ya Mloganzila ni kwenda wanafunzi wanaojifunza udaktari na wanaojifunza uuguzi, wakajifunzie. Sasa wale wanafunzi, hivi hakuna wanafunzi wa practical? Wanafanya nini? Kwa nini wasiungane na wale ma-nurse na madaktari katika kusaidia wagonjwa? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kweli madaktari wale na wauguzi wana kazi. Kunywesha kila mmoja umnyweshe na haruhusiwi ndugu yeyote kubaki pale, hili ni tatizo. Naiomba Serikali iangalie, kama imeshindwa kabisa, waache hata ndugu mmoja aweze kutoa huduma kwa mgonjwa wake. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba sasa Serikali nayo iimarishe vitengo vya mifupa katika hospitali za wilaya na mikoa ili kusaidia mzigo mzito utakaoenda MOI - Muhimbili. Naomba Hospitali ya Muhimbili wangalie gharama… (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. MARIAM N. KISANGI: Mheshimiwa Naibu Spika, kuna tatizo la ucheleweshwaji wa bili kwa wagonjwa. Hilo ni tatizo kubwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja, mengine nitayaleta kwa maandishi.