Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

Hon. Salma Rashid Kikwete

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Mchinga

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

MHE. SALMA R. KIKWETE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Kwanza naomba nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu. Hatimaye nikushukuru wewe Mheshimiwa Naibu Spika kwa kunipa nafasi ya kuweza kuchangia kwenye Wizara hii ya Afya ambayo ni muhimu sana kwa ustawi na maendeleo ya mwanadamu katika muktadha ufuatao. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, usipokuwa na afya njema huwezi kwenda shule; usipokuwa na afya njema maendeleo hayawezi kufanyika; usipokuwa na afya njema kitu kitakachojitokeza hata uchumi wa Taifa letu utapungua kwa ajili ya kukosa nguvu kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nianze kwa kumshukuru Mheshimiwa Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kazi kubwa na nzuri ambayo anaifanya katika Taifa letu. Sambamba na hilo namshukuru Mheshimiwa Waziri wa Wizara ya Afya pamoja na Naibu wake na watendaji wote wa Wizara hii bila kuwasahau madereva na wahudumu ambao wanafanya kazi nzuri. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naishukuru sana Wizara ya Afya na Maendeleo ya Jamii kwa kutupatia fedha kiasi cha shilingi 1,200,000,000 katika Jimbo la Lindi Mjini. Shilingi milioni 400 zimetolewa kwa ajili ya Hospitali ya Kituo cha Afya cha Mingoyo, lakini shilingi milioni 700 zimetolewa kwa ajili ya Kituo cha Afya cha Mnazi Mmoja. Tunaishukuru sana Serikali.
(Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo, pamoja na mazuri ambayo yameweza kujitokeza, lakini Lindi tuna mambo yafuatayo; hatujajua hatma yetu ya Mkoa wa Lindi kuwa na Hospitali ya Mkoa na Hospitali ya Wilaya. Ukiuliza hivi, unaambiwa Sokoine ni Hospitali ya Mkoa. Wakati mwingine unaambiwa Sokoine ni Hospitali ya Wilaya. Mheshimiwa Waziri, naomba utakapokuja hapa utupe ufafanuzi juu ya jambo hili.

Mheshimiwa Naibu Spika, sambamba na hilo, kama Mkoa wa Lindi na kama ambavyo Hospitali ya Sokoine iko pale, lakini kikubwa Mganga Mkuu wa Hospitali ya Mkoa hana gari la kufanyia huduma. Sizungumzii ambulance, tunazungumzia gari la kufanyia huduma, anatumia gari binafsi kuendeshea shughuli za Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, asilimia 28 tu ndiyo ya wahudumu waliopo ndani ya Mkoa wa Lindi. Tuna upungufu wa asilimia 72. Naomba hili liangaliwe kwa jicho la huruma. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hali ya UKIMWI nchini Tanzania kwa mujibu wa Tanzania HIV Impact Survey ya mwaka 2016/2017, maambukizi ya wanawake ni asilimia 6.5 na wanaume ni asilimia 3.5. Hii hufanya maambukizi Kitaifa ni 5%. Sasa ndani ya Mkoa wa Lindi ni asilimia 0.3. Nawapongeza sana watu wa Mkoa wa Lindi kwa kupunguza kiasi kikubwa cha maambukizi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, maambukizi ya UKIMWI yana vitu mbalimbali ambavyo vinasababisha. Kwa hiyo, tuna wajibu sisi kama Watanzania kuepuka vitu vile ambavyo vinaambukiza ili pesa hizi zitakazopatikana baada ya kutumika kununua madawa na vitu vingine, zitumike katika mazingira ya kufanya shughuli mbalimbali za maendeleo katika nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nazungumzia ARVs ndiyo dawa zinazotumika kufubaisha virusi vya UKIMWI. Sasa hizi dawa ziende kwa wakati kwa kunusuru maisha ya watu hawa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu vifo vya akina mama na watoto; haikubaliki nchi kama Tanzania, mwanamke kufa wakati analeta kiumbe kingine duniani. Tunajua kuna mipango na mikakati mizuri sana iliyowekwa, lakini ni lazima itekelezwe na iwekwe kwa wakati. Kuna magonjwa yasiyo ya kuambukiza kama figo, pressure na kisukari. Ni lazima yawekewe mikakati madhubuti ili kuhakikisha mazingira haya yanakuwa salama katika nchi yetu. Yote haya yanawezekana tu kama bajeti iliyopangwa na Serikali itapelekwa kwenye maeneo husika kwa wakati na ikiwa timilifu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana. Naunga mkono hoja.