Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

Hon. Vicky Paschal Kamata

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

MHE. VICKY P. KAMATA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi na mimi niweze kuchangia hotuba hii iliyoko mbele yetu. Kwanza kabisa napenda nimshukuru Mungu kwa kuniwezesha kusisima tena katika Bunge hili na kuweza kuchangia bajeti.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niungane na wenzangu kumpongeza sana Mheshimiwa Ummy, Waziri wa Afya, Naibu wake, Mheshimiwa Dkt. Ndugulile, Katibu Mkuu na Viongozi wote, Watalaam wetu mbalimbali wa sekta hii ya afya, kwa jitihada kubwa wanazozifanya kuhakikisha kwamba afya ya Mtanzania inazidi kuimarika ili tuweze kufanya kazi na kuleta maendeleo kwenye nchi yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na pongezi hizo naomba pia niwakumbushe Waheshimiwa Wabunge wenzangu jambo moja. Waheshimiwa Wabunge kazi yetu ni kuisimamia Serikali na kuishauri Serikali, nadhani hiyo ndiyo kazi yetu kubwa. Pia naamini kabisa kwamba sisi kuwa ndani ya Bunge hili siyo kwa sababu tuna akili kuliko wale tuliogombea nao tukawashinda, wala siyo kwamba sisi ni bora zaidi ya wale tuliogombea nao tukawashinda isipokuwa ni kwa neema tu. Mungu amepanda sisi tuingie kwa kipindi hiki tufanye hiyo kazi ya kuishauri Serikali na kusimamia siyo kuisifia Serikali au kuibomoa, hapana! Kuisimamia na kuishauri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikitoka kwenye hilo kwa kuwa nimewakumbusha na nashukuru makofi haya ni kwamba kweli mnaungana na mimi kwamba kazi yetu ni hiyo kusimamia na kuishauri, basi tuifanye kwa uaminifu na Mungu wetu atusaidie.

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kusema kwamba ni Mjumbe wa Kamati ya Huduma na Maendeleo ya Jamii maarufu Guantanamo na nilipata bahati ya kufanya ziara katika Mkoa wa Mbeya na Iringa ambapo tulikuwa tunakwenda kukagua miradi ambayo ilikuwa imeidhinishiwa pesa kwa bajeti ya 2017/2018.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumetembelea Chuo cha Maendeleo ya Jamii cha Lungemba kilichopo Mufindi – Iringa. Chuo kile kilikuwa kimetengewa milioni 258 kama nakosea nitarekebishwa na Wajumbe wenzangu lakini nina uhakika ni milioni 258 zilitengwa na tukaidhinisha pesa zile ziende kwa ajili ya mradi ule ili hiki Chuo cha Maendeleo ya Jamii huo mradi uweze kukamilika, tuweze kudahili wanafunzi wa kutosha ili waje watusaidie huko maana tunaitaka Tanzania ya viwanda, tunataka Tanzania kufikia uchumi wa Kati kwa kutegemea viwanda.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunawategemea sana hawa Maafisa Maendeleo washuke kule chini kwenye Kata zetu, wafanye hiyo kazi ya kuhamasisha maendeleo, wawe chachu kwa sababu watakwenda kule wakiwa wameelimishwa vya kutosha, wakatusaidie kule chini, kuhamasisha maendeleo kule chini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumeenda kule pesa zile ambazo tumeidhinisha Bunge la Bajeti mwaka jana mwaka wa 2017/2018 pesa hazijakwenda mpaka tulivyoenda kukagua huo mradi na mpaka juzi ambapo tunajadili tena, tunachambua bajeti ya hii 2018/2019, taarifa tulizokuwa nazo mpaka dakika ya mwisho juzi hapa ni kwamba zile milioni 258 hazijakwenda mpaka sasa hivi tunapojadili bajeti nyingine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumeenda Chuo cha Maendeleo ya Jamii Uyole, kiko Mbeya. Chuo hicho kilikuwa kimetengewa zaidi ya milioni 216, tumefika kule pesa hazijakwenda mpaka mwisho sasa tunaingia bajeti nyingine 2018/2019 pesa hazijakwenda.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumekwenda hospitali ya Rufaa ya Mbeya, hii ni hospitali ya Kanda inahudumia mikoa saba, hospitali hii tuliidhinisha kwenye Bunge hili bilioni 200 kwa ajili ya kununua madawa na kazi zingine huko nafikiri na ujenzi wa jiolojia, kitu kama hicho mtanirekebisha wataalam ambao mnajua, lakini bilioni 200 tumeidhinisha kwenye Bunge hili. Mpaka tunaenda kuukagua ule mradi bilioni 200 zilikuwa hazijakwenda na mpaka juzi tunachambua bajeti hii ya mwaka mwingine 2018/2019, pesa zile hazijakwenda.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kazi yetu ni kuisimamia Serikali na kuishauri sasa tunashauri zile pesa ziende hata kama mimi namheshimu sana Mheshimiwa Ummy na naamini wana dhamira ya dhati pamoja na Naibu wake na Katibu Mkuu wanafanya kazi kwa dhati, sasa sisi kama kazi yetu ni kusimamia kweli Serikali, ni kuishauri kweli Serikali, pesa ambazo tunakuwa tumepitisha humu ziwe zinaenda kule kutekeleza miradi ili hata uhalali wetu wa kuwa humu ndani uweze kuwepo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, maana kama tunaisimamia Serikali, tunaishauri, halafu tunaidhinisha pesa haiendi mpaka dakika za mwisho, tunakuja kujadili bajeti tena kwa mwaka mwingine, tunaidhinisha tena pengine hazitaenda tena. Kama zile za mwaka jana hazijakwenda tuna uhakika gani hizi tunazoidhinisha leo zitakwenda? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naomba sana, tusionekane kama rubber stamp, maana huko nje jamani credibility ya Bunge letu inaondoka watu wanafuatilia Bunge, watu wanafuatilia Bunge hili tutake, tusitake na wakija wakaanza kutudhihaki kama akina Pascal Mayala tusiwalaumu kwa sababu wao wanaamini kazi yetu ni kuisimamia na kuishauri Serikali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, tunapoishauri tunatakiwa tuhakikishe kwamba tunaidhinisha pesa mwaka unaofuata au muda unaotakiwa pesa zikiwa zimeshaenda au hazijaenda tuwe na haki ya kuuliza na tujibiwe tu vizuri siyo kwa lengo la kubomoa bali kwa lengo la kujenga. Nimesema kazi yetu ni kuishauri na kuisimamia, siyo kuibomoa wala kusifia siyo kazi yetu hiyo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba sana mimi nitaunga hoja hii mkono bila wasiwasi, lakini naomba tunapoidhinisha pesa ziwe zinaenda na kama kunakuwa kumetokea mabadiliko yoyote ya matumizi basi Bunge hili si ndiyo linatakiwa pia liidhinishe hayo mabadiliko? Kwa hiyo, kama kuna mabadiliko, tuidhinishe sasa hayo mabadiliko kwamba hii pesa haitaenda tena kwenye kile Chuo cha Maendeleo lakini tutaitumia kwenye one, two, three, four iende hivyo, ndiyo hivyo ndugu zangu tutafika, vinginevyo hatutafika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nina imani sana na Mheshimiwa Ummy, nina imani sana na Serikali hii kupitia Wizara ya Afya, naamini kabisa kwamba bajeti hii itapita lakini msisitizo sasa tukubaliane kabisa, tunapopitisha ziende kweli. Naomba pia kwa ajili ya Mkoa wangu wa Geita. Mkoa wa Geita tuna ujenzi wa hospitali ya Mkoa na mpaka sasa hivi jitihada kubwa zimeshafanyika Mheshimiwa Ummy, rafiki yangu anajua. Kwa hiyo, tunaomba hizi pesa ambazo tunazipitisha sasa hivi hapa, ziende ili ile hospitali ikamilike.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia hatuna ma-specialist kwenye hospitali yetu ya Mkoa, tunaye mmoja tu na uhitaji kwa Mkoa wa Geita ni Specialist 24. Wauguzi tunao watatu katika Mkoa mzima, tunahitaji Wauguzi 30. Kwa hiyo, naomba sana Serikali yetu hii sikivu, basi isikie yale ambayo tunayapitisha humu yaende ili tuweze kuufikia uchumi wa kati unaotegemea viwanda.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana.