Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa mwaka wa Fedha 2018/2019 - Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa na Ofisi ya Rais, Utumishi na Utawala Bora

Hon. George Malima Lubeleje

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mpwapwa

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa mwaka wa Fedha 2018/2019 - Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa na Ofisi ya Rais, Utumishi na Utawala Bora

MHE. GEORGE M. LUBELEJE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi ili nami niweze kuchangia hoja hizi mbili. Kwanza niwapongeze Waheshimiwa Mawaziri wote wawili, niwapongeze Watendaji wote wa Wizara hizi mbili kwa kazi nzuri. Nchi hii ina utawala bora, ndiyo maana tumetulia, ndiyo maana tuko hapa Bungeni tunafanya vikao bila wasiwasi nchi imetulia na good governance ni kwa sababu ya political stability. Kwa hiyo, nataka kukuhakikishia kwamba ni Vyombo vya Usalama ndiyo vinafanya kazi nzuri, ndiyo maana tunatembea hata saa nane za usiku.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la kwanza ni mapato ya Halmashauri. Sifa ya Halmashauri yoyote ile ni mapato, kukusanya mapato ya ndani, kama Halmashauri haikusanyi mapato ya ndani haina sifa ya kuitwa Halmashauri ya Wilaya. Kwa hiyo, wakati wa Kamati tuliwaeleza Wakuu wa Mikoa, Wakurugenzi Watendaji wajitahidi kukusanya mapato ya ndani wasitegemee zaidi ruzuku maana ipo siku moja Serikali ikisema kwamba ruzuku tunafuta, Halmashauri zitashindwa kujiendesha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili, niongelee suala la migogoro katika Halmashauri. Bahati nzuri mimi nimekuwa Diwani na Mwenyekiti wa Halmashauri miaka 15, kuna migogoro mingine inasababishwa na Wakurugenzi, Diwani ni haki yake kulipwa posho kila mwezi, lakini Madiwani wanakaa miezi miwili, mitatu, minne bila kulipwa posho hapo mgogoro lazima utakuwepo tu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mgogoro mwingine ni kutokufahamu majukumu ya Madiwani. Tuliokuwa Madiwani zamani tulipelekwa Hombolo kwa ajili ya mafunzo ya mwezi mmoja, lakini hawa Madiwani wa siku hizi hawapelekwi na hivyo hawajui mipaka yao; mipaka ya Watendaji na mipaka ya Madiwani. Kwa hiyo, ombi langu kwa Mheshimiwa Waziri wa TAMISEMI, muwapeleke mafunzo angalau wiki mbili hawa Madiwani waweze kujua mipaka yao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ni posho za Madiwani. Posho za Madiwani wanazolipwa, mwaka 2002 wakati Mheshimiwa Mizengo Pinda akiwa Waziri wa TAMISEMI aliunda Tume ya kushughulikia maslahi ya Madiwani na Tume ile iliongozwa na mimi mwenyewe na ikaitwa Tume ya Lubeleje. Kwa hiyo, mpaka leo wanapata kiwango kilekile.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, namwomba Mheshimiwa Waziri majukumu ya Madiwani wa zamani na sasa ni tofauti. Zamani Madiwani ukiamka asubuhi unakwenda kwenye kikao ukitoka kwenye kikao unarudi nyumbani unapumuzika. Siku hizi mradi ukianza wa shule mradi wa zahanati lazima Diwani ushinde pale. Kwa hiyo, namwomba sana Mheshimiwa Waziri ajitahidi sana angalau wawaangalie waongeze posho kidogo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, halafu jambo lingine baada ya kuongezwa hii posho kidogo, Madiwani walikopa benki, wengi walikopa CRDB, walikopa NMB, sasa bahati mbaya sana kuna Wakurugenzi hawakati zile fedha na kupeleka kwenye haya mabenki. Kwa hiyo, mgogoro mkubwa sana, vyombo vya fedha NMB na CRDB wanaanza kuwafuata Madiwani kwamba ninyi ndiyo mliokopa lakini mishahara yao imeshapelekwa Halmashauri, hawalipwi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ni kuhusu mishahara ya watumishi, Mheshimiwa Waziri wa Utumishi, wakati umefika ndugu zangu tuangalie watumishi wanafanya kazi katika mazingira magumu sana, maisha na gharama zinapanda kila kukicha. Sasa ufinyu wa bajeti sidhani na sitegemei kuna mwaka mmoja Serikali hii itasema sasa tuna fedha za kutosha, hakuna! Kwa hiyo, tuwafikirie Watumishi wanafanya kazi ngumu sana, sifa ya Tanzania wanaleta watumishi kwa kufanya kazi nzuri.(Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ni kucheleweshwa kwa fedha za miradi ya maendeleo. Sasa Mheshimiwa mmoja amesema kwamba sisi ambao tunahudhuria vikao kwenye Halmashauri tusilalamike. Hii ni ruzuku ya Serikali Kuu na sheria inatamka kwamba Serikali Kuu ni lazima isaidie Halmashauri itoe ruzuku. Wabunge tunakaa hapa miezi mitatu kupitisha bajeti ya Serikali, lakini bahati mbaya sana fedha ambazo zinaidhinishwa hapa hazifiki zote.

Mheshimiwa Mwenyekiti, juzi wakati tunachambua bajeti ya Wakuu wa Mikoa, Wakuu wa Mikoa wengi mpaka hadi Februari, 2018 fedha ambazo wamepokea ni kati ya asilimia 51, 48, 60 lakini fedha nyingine hazifiki kwenye miradi. Kwa hiyo, ukitembelea Halmashauri nyingi kuna viporo vingi sana zahanati hazikamilishwi, vituo vya afya havikamilishwi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, namshukuru sana Mheshimiwa Waziri wa TAMISEMI kwa kuniletea shilingi milioni 500 kwa ajili ya kukamilisha Kituo cha Afya cha Mima. Kazi inakwenda vizuri bado kuna Kituo cha Afya cha Mbori ambacho ujenzi wake bado kabisa na kile kituo kikishakamilika kitahudumia Kata Nne; Kata ya Kimagai, Kata ya Lupeta, Kata ya Matomondo na Kata ya Mlembule. Kwa hiyo, naomba milioni 500 zipelekwe tena Mbori kwa ajili ya kukamilisha kituo kile.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ambalo nataka nimalizie, ni suala la upungufu wa watumishi. Serikali inasema ombeni vibali, Wilaya ya Mpwapwa tuna upungufu wa Watumishi wa huduma Idala ya Afya zaidi ya 150, tumeleta juzi kuomba kibali watumishi 150, tumepewa watumishi sita tu. Kuna Kada zingine zile ambazo ni ndogondogo mziachie Halmashauri ziajiri badala ya kuomba kibali Utumishi ndiyo tuwaajiri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema haya nakushukuru sana kwa kunipa nafasi hii. Niwapongeze sana Mawaziri na Watendaji wao wanafanya kazi nzuri, ila wajitahidi sana kutembelea Majimbo yetu kwa sababu ukitembea kwenye Majimbo ndiyo unaona changamoto za kila Mbunge.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana, naunga mkono.