Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Katiba na Sheria

Hon. Dr. Advocate Damas Daniel Ndumbaro

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Songea Mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Katiba na Sheria

MHE. DKT. DAMAS D. NDUMBARO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi kuchangia kwenye bajeti ya Wizara ya Katiba na Sheria. Awali ya yote namshukuru Mheshimiwa Waziri na Watendaji kwa taarifa nzuri ya bajeti ambayo wametuletea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pili, nitoe shukrani kwa Mheshimiwa Waziri na watendaji wote wa Shule Kuu ya Sheria kwa kazi nzuri wanayoifanya ya kuchuja wanasheria na kada hii ya sheria ili tuwe na wanasheria wazuri. Pamoja na mambo hayo yote, kuna changamoto nyingi ambazo zinaikabili Shule Kuu ya Sheria.

Kwanza, bajeti finyu. Kwenye bajeti ya matumizi mengineyo, tukumbuke kwamba Shule Kuu ya Sheria inahudumia takribani vyuo vikuu 17 ambavyo vinatoa wahitimu wa shahada ya kwanza ya sheria, lakini bajeti yake ni ndogo katika matumizi mengineyo na haifiki hata asilimia
22. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia kuna tatizo la kisheria. Ukisoma kifungu cha 15 (1)(d) ya Sheria ya Shule Kuu ya Sheria Na. 18 ya 2007, imeanzisha Governing Council ambapo Wajumbe wake, mmoja kati ya Wajumbe ni Mkuu wa Kitivo cha Sheria kutoka Chuo Kikuu cha Dar es Salaam.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa kama nilivyosema, kuna vyuo vikuu 17 vinavyotoa shahada ya kwanza ya sheria, ni kwa nini sheria hii imetoa upendeleo kwa chuo kikuu kimoja kupeleka Mkuu wake wa Kitivo katika Governing Council wakati tuna vyuo vikuu 17. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wakati sheria hii inataungwa mwaka 2007, hivi vyuo vingi vilikuwepo. Kwa hiyo, ni mapendekezo yangu Mheshimiwa Waziri akiona inafaa, itendwe haki jinsi ya kupata mwakilishi wa Vitivo vya Sheria vya Vyuo Vikuu vyote Tanzania badala ya kupendelea chuo kikuu kimojan kwa sababu upendeleo huo ni ubaguzi ambao unapingwa kikatiba kwa mujibu wa Ibara ya 13(4) ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hoja yangu ya pili kwa Wizara hii ni suala la usajili wa vyeti vya kuzaliwa. Katika hotuba ya Mheshimiwa Waziri, ametueleza kwamba ni asilimia 28 tu ya watoto wote wanaozaliwa wanaandikishwa na kupata vyeti. Hivyo tuna upungufu wa asilimia 72. Upungufu huu ni mkubwa sana, tuna kila sababu ya kuwa- address upungufu huu kuhakikisha kwamba kila mtoto anayezaliwa anapata cheti cha usajili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, takwimu zilizopo katika kiambatisho ā€˜Dā€™ ukurasa wa 94 kinatupa mshtuko ambao inabidi Wizara na Serikali iangalie vizuri zaidi. Katika mikoa 26 takwimu zimeonesha kwamba ni mikoa 12 tu ndipo takwimu zake zimeonesha pale. Kuna mikoa 14 haijaonesha ule usajili wa under five years jinsi ulivyofanyika. Katika hiyo mikoa 14, upo Mkoa wa Ruvuma na Jimbo la Songea. Kwa hiyo, hii inaonesha kwamba watoto hawa wa under five years wanakosa haki zao za msingi katika kusajiliwa mara baada ya kuzaliwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kukosa haki huko ni kukiuka Ibara ya 7 ya Tamko la Haki za Watoto Duniani la mwaka 1989, ni kukiuka Ibara ya 14 ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, lakini pia ni kukiuka kifungu cha 6(3) cha Sheria ya Mtoto ya mwaka 2009, Sura ya 13. Ni ushauri wangu kwa Serikali na kwa Wizara kwamba ni muhimu sana kuhakikisha kwamba suala la usajili wa under five years linafanyika nchi nzima ili kuhakikisha kwamba siyo tu tunapata takwimu, lakini pia tunatekeleza haki za watoto hao kama zilivyoelezwa katika nyaraka hizo za kimataifa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia naomba nieleze kuhusiana na ukosefu wa Kituo cha Kimataifa cha Utatuzi wa Migogoro ya Kibiashara. Katika hotuba nzima aliyoelezea Mheshimiwa Waziri Profesa Kabudi, sijaona mahali ambapo ameelezea kuwepo au kuanzishwa kwa Kituo cha Kimataifa cha Utatuzi wa Migogoro (International Commercial Arbitration).

Mheshimiwa Mwenyekiti, tufahamu kwamba mikataba mingi ambayo tunaingia kama nchi, tunalazika kuweka arbitration clause ya kupeleka migogoro yetu ya kibiashara katika nchi mbalimbali duniani, nchi ambazo hatujui mambo yao ya kisheria yakoje, systems zao ni ngumu, matokeo yake tunakuja kupata maamuzi ambayo yanakuja kutuathiri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ili kukabiliana na hilo, ni ushauri wangu kwamba ni vizuri tuwe na Kituo cha Kimataifa cha Utatuzi wa Migogoro hapa nchini ambacho kitasaidia sana kutatua migogoro mingi ya kibaishara na sisi tulazimishe. Nchi jirani kama Rwanda wameanzisha Kigali International Arbitration Center ambayo inakuja kwa juu sana. Tusipokuwa makini itachukua districts zote katika Afrika Mashariki na Kati.

Mheshimiwa Mwenyekiti, na sisi tunapaswa kujipanga kuhakikisha kwamba tunaanzisha kituo hicho ambacho kina faida. Sheria nyingi ambazo tumezitunga za kulinda rasilimali za nchi hii ambazo ni nzuri sana, tunahitaji kuzilinda zaidi kuwa na mifumo ya utatuzi wa migogoro ambayo tunaiamini na inaeleweka. Hivyo, kuanzishwa kwa kituo kama hicho, hakuepukiki. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kituo kama hicho kikianzishwa ni muhimu sana kwa kusaidia wataalam wa ndani kujenga uwezo wao katika utatuzi wa migogoro ya kibiashara ya Kimataifa. Kituo kama hicho kikiwepo hapa ndani kitatuokolea fedha nyingi sana ambazo tunatumia kwenda kutatua migogoro katika nchi mbalimbali. (Makofi)

Hivyo basi, ni ushauri wangu Mheshimiwa Waziri na Wizara nzima waone umuhimu wa kuanzisha kituo kama hicho. Ahsante sana.