Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Ofisi ya Makamu wa Rais, Mungano na Mazingira kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

Hon. Amina Saleh Athuman Mollel

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Ofisi ya Makamu wa Rais, Mungano na Mazingira kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

MHE. AMINA S. MOLLEL: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi nichangie katika Wizara hii. Naomba niende moja kwa moja katika mazingira, niwapongeze pia Waziri na Naibu wake kwa kazi kubwa wanayoifanya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tupo katika msimu wa mvua na katika msimu huu wa mvua tumeshuhudia ni kwa jinsi gani baadhi ya wenzetu walivyoathirika, tunawapa pole. Hata hivyo, haya yote ni kutokana na baadhi ya wenzetu ambao utendaji wao wa kazi uliwezesha kutoa vibali ambavyo havikustahili kutolewa katika maeneo hayo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano, tukienda katika Bonde la Msimbazi kuna baadhi ya wananchi ambao leo hii ukienda wana vibali vinavyowaruhusu kuwepo maeneo hayo. Kama hawa watu wasingetoa vibali hivyo ni dhahiri kabisa mafuriko haya yasingewakumba.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile mazingira yetu tunaharibu sisi wananchi wenyewe. Twende katika mito yetu ambayo kwa namna moja au nyingine tumekuwa tukimwaga taka ngumu lakini sio hiyo tu hata katika mitaro tumeona kuziba kwake ni kutokana na uharibifu wa mazingira unaofanywa na baadhi ya wananchi wenzetu wenyewe. Kwa hapa niwaombe wenzangu wananchi wa kawaida tujue umuhimu wa kuhifadhi mazingira.

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo hii tunaona mafuriko na kama tunavyofahamu katika mafuriko maji mengine yanatoka katika vyoo na takataka mbalimbali zimechanganyika. Baada ya mafuriko kunakuwepo na tahadhari ya ugonjwa wa kipindupindu. Kwa hiyo, ni dhahiri kabisa jukumu hili sio la Serikali peke yake, hata sisi wananchi tunapaswa kuhakikisha kwamba tunashuhudia na kuyalinda mazingira yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Tanzania sera iliyopo sasa ni kuhakikisha kwamba ujengaji wa viwanda, nakubaliana kabisa na naunga mkono, lakini katika viwanda hivyo tuangalie kwamba ni kwa jinsi gani tunahitaji viwanda lakini viwanda ambavyo vitalinda mazingira yetu. Tunafahamu Mataifa makubwa kama Marekani na China ambayo yalikataa kusaini Mkataba wa Kyoto kutokana na uhitaji wa viwanda vikubwa vilivyopo kwao, lakini pia ndio chanzo cha uharibifu wa mazingira. Kwa hiyo na sisi wakati huu tunapoanzisha ujenzi wa viwanda, tuhakikishe kwamba viwanda sio chanzo cha uharibifu wa mazingira.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hivi sasa air pollution ni tatizo kubwa na sio Tanzania tu, maeneo mengi. Kwa hiyo, katika viwanda naiomba Wizara inayohusika kuhakikisha kwamba viwanda hivi vinakuwa sio chanzo cha uharibifu wa mazingira bali vinakuwa ni chanzo cha utunzaji wa mazingira.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumeona tatizo kubwa la ukataji wa miti ni kutokana na uhitaji mkubwa wa mkaa. Hivi sasa Tanzania Mwenyezi Mungu ametujalia tuna gesi, basi tuone ule uharaka wa kuhakikisha kwamba hii gesi inakuwa ni chanzo cha utunzaji wa miti yetu, miti yetu isikatwe na kusiwepo na uharibifu wa mazingira kwa sababu wananchi wengi watakwenda katika utumiaji wa gesi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ili waende katika utumiaji wa gesi tunahitaji gesi kwa gharama nafuu, kwa maana hiyo tutaweza kulinda mazingira yetu, watu na hasa kwa sababu mkaa usipohitajika kwa kiasi kikubwa mjini, ni dhahiri kabisa wale waliopo kule Vijijini hawatoharibu miti yetu, hawatokata miti kwa ajili ya uchomaji wa mkaa. Kwa hiyo, ni uharaka unahitajika kwa hivi sasa kuhakikisha kwamba mazingira, gesi inakuwa ni chanzo cha kuhifadhi misitu, ni chanzo cha utunzaji wa misitu ili wananchi wasiweze kuharibu kwa kiasi kikubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baadhi pia ya maeneo yamekuwa na uharibifu mkubwa na hasa tunavyofahamu wananchi wenyewe ndio chanzo kikubwa. Itumike elimu na kuhakikisha kwamba kwa mfano wanaochimba mchanga maeneo mengi wanakuwa ni chanzo cha uharibifu. Yale maeneo kama tulivyoona Makamu wa Rais alichokianzisha hapa Dodoma, basi elimu hiyo ya upandaji wa miti iendelee katika maeneo mengi kwenye mikoa mingine ili kulinda mazingira yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja ya Waziri. Ahsante.