Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Ofisi ya Makamu wa Rais, Mungano na Mazingira kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

Hon. Machano Othman Said

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

House of Representatives

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Ofisi ya Makamu wa Rais, Mungano na Mazingira kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

MHE. MACHANO OTHMAN SAID: Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote naomba nimshukuru Mwenyezi Mungu kwa kutujalia uhai na uzima, lakini pia nikushukuru wewe kwa kunipa nafasi hii ya kuchangia hotuba hii ya Mheshimiwa Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunachangia hotuba hii lakini wiki moja ijayo tutakuwa tunaadhimisha miaka 54 ya Muungano wetu. Kwa hiyo, jambo hili ni jema sana kwa leo kulizungumza katika Bunge letu Tukufu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi nitazungumzia mambo matatu. Kwanza nimpongeze Mheshimiwa Waziri wa Nchi kwa kitabu chake hiki kizuri, nikienda katika ukurasa wa sita amezungumzia jinsi ambavyo wamefanya vikao vya kuzungumzia kero za Muungano. Kwa bahati nzuri vikao hivi vimeanza muda mrefu sana na kwa bahati mbaya hapo hapo matokeo ya vikao hivi utekelezaji wake unakuwa mdogo sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pande mbili za Muungano yaani Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar walifikia makubaliano kuhusu ajira za taasisi za Muungano kwamba katika taasisi za Muungano asilimia 21 za ajira zote zitengwe kwa ajili ya Zanzibar kwa watu ambao wana elimu na weledi wa kazi ambazo zitatangazwa kwa upande wa Bara. Ukiacha taasisi za ulinzi kama Jeshi la wananchi wa Tanzania, Polisi na Uhamiaji, taasisi zote zilizobakia hazijatekeleza suala hili.

Naomba Mheshimiwa Waziri akija kufanya majumuisho atuambie ni sababu gani za msingi zaidi ya miaka mitano sasa suala hili halijatekelezwa. Suala hili linaleta kero, manung’uniko kwa watu ambao wana sifa, baadhi ya Wizara wanaziona za Muungano lakini Katibu Mkuu, Naibu Makatibu Wakuu, Wakurugenzi mpaka watumishi wote hamna. Siyo jambo jema na linaleta ukakasi sana katika shughuli za maendeleo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili katika makubaliano ambayo yamefanywa pia pande mbili zilikubaliana kwamba Sheria ya Uvuvi wa Bahari Kuu ifanyiwe marekebisho katika Bunge hili ili iweze kuridhiwa na Zanzibar kwa kupitia Baraza la Wawakilishi. Hadi leo sheria hii haijafanyiwa marekebisho na bado suala la uvuvi wa bahari kuu linaleta tabu na haliwezi kutekelezeka. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ni hili ambalo Mheshimiwa Pondeza alilizungumzia la vyombo vya usafiri au vyombo vya moto. Ni kweli kwamba vyombo kutoka Zanzibar vikija Bara vinatozwa fedha na havipati permit vizuri. Hata hivyo, nalo hili wamekubaliana Serikali mbili kwamba Serikali ya Jamhuri ya Muungano wafanye marekebisho kupitia Wizara ya Mambo ya Ndani kwa kifungu kimoja tu cha sheria ili sheria hii iwe vizuri, lakini mpaka leo bado haijafanyiwa marekebisho. Hili nalo nataka ufafanuzi wa Mheshimiwa Waziri wakati akija kuhitimisha hapa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine katika kitabu hiki imeelezewa kwamba pamoja na kuimarisha Muungano ofisi hii imejenga makazi na Ofisi ya Makamu wa Rais Zanzibar, lakini hadi leo wajenzi wa Ofisi zile hawajamaliziwa malipo yao karibu mwaka wa nne au wa tano sasa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunamuomba Mheshimiwa Waziri nalo hili alione kwamba ni kero pia kwa wale ambao wamejenga ofisi hizi. Ni vizuri kwa Makamu wa Rais kuwa na Ofisi nzuri Zanzibar lakini pia kuwa na staff wazuri Zanzibar ili kuweza kushughulikia masuala haya ambayo ni sehemu ya Muungano wetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika masuala ya Muungano ambayo yamekubaliwa nje ya Muungano ni kutoa fursa kwa upande wa Zanzibar kupata soko kwa Tanzania Bara. Jambo hili utekelezaji wake umekuwa mgumu sana hata bidhaa ndogo ndogo ambazo zinazalishwa Zanzibar kuingia Bara ni jambo gumu sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hili linaambatana na sheria ya kwamba ukianzisha kiwanda Zanzibar lazima upate leseni kutoka Bara yaani BRELA. Kwa hiyo, tunafikiria kwamba ni vyema kwa upande wa Jamhuri wangefikiria kuanzisha wakala ama Ofisi ya BRELA Zanzibar ili Wazanzibar waweze kuanzisha viwanda kukidhi mahitaji ya Zanzibar na kukidhi soko la Tanzania Bara. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ni ahadi za viongozi. Viongozi wetu wa Kitaifa wanatembelea Zanzibar na Bara na kote huko wanatoa ahadi, lakini utekelezaji wa ahadi kwa upande wa Zanzibar unakuwa mgumu na wa muda mrefu. Zipo ahadi tangu Awamu ya Nne ambazo
zimetolewa Zanzibar ikiwemo ahadi ya barabara ya Fuoni mpaka leo bado haijajengwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, tunaomba Mheshimiwa Waziri alichukue hili kwamba ni changamoto katika Muungano wetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini nisilalamike tu pia niwapongeze sana kwa kupitia mradi wa TASAF. Serikali ya Jamhuri ya Muungano imefanya vizuri sana katika mradi huu na kwa upande wa Zanzibar mradi huu unafanya vizuri. Tunaipongeza Serikali ya Jamhuri ya Muungano na tunasema kwamba ni vyema miradi kama hii iwe inapelekwa Zanzibar kwa kiwango kizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, la mwisho kabisa kwa upande wangu mimi ni kuhusu fursa za kibiashara kama nilivyozungumza mwanzo, lakini pia Zanzibar ni sehemu ya kisiwa kwa hivyo shughuli nyingi za kibiashara zinakuwa katika huduma. Huduma za kibiashara ndiyo ambazo zinaingiza fedha nyingi Zanzibar kama mitandao ya kijamii, simu na kadhalika.

Kwa hiyo, fursa hizi zifunguke zaidi ili Zanzibar waweze kufaidika. Wenzangu asubuhi walizungumzia utalii na majengo ya kisasa ya airport na bandari haya ni msingi mkubwa katika uchumi wa Zanzibar. Tunaomba sana Serikali ya Jamhuri ya Muungano iwaunge mkono Serikali ya Zanzibar katika utekelezaji wa miradi hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, naomba kuunga mkono hoja hii na sina mengi zaidi ya hayo.