Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Ofisi ya Makamu wa Rais, Mungano na Mazingira kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

Hon. Abdallah Ally Mtolea

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Temeke

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Ofisi ya Makamu wa Rais, Mungano na Mazingira kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

MHE. ABDALLAH A. MTOLEA: Mheshimiwa Mwneyekiti, nami nimshukuru Mwenyezi Mungu kwa kukupa uwezo wa kunipa nafasi ili niweze kuchangia katika bajeti inayohusu Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira).

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini nianze kwanza kwa kutoa pole kwa wananchi wa Jiji la Dar es Salaam hasa wapiga kura wangu wa Temeke kwa mvua kubwa ambazo zinakwamisha shughuli zao za kila siku kwa namna moja au nyingine. Niiombe pia Serikali baadhi ya maeneo madhara yamekuwa makubwa kwa sababu ya wao kutotimiza wajibu wao vizuri. Kama pale kwenye barabara ya Mandela kwenye mataa ya Serengeti ambapo kuna shule ya sekondari ya Kibasila mifereji ya barabara imeshindwa kubeba maji yale ya mvua matokeo yake maji yote yanakwenda kwenye shule ile. Sasa hivi naambiwa madarasani maji ni ya kiuno.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia kuna barabara ya Jet Lumo - Davis Corner na yenyewe pia Serikali haijaitengea fedha ya kumalizia toka mwaka wa fedha uliopita na mwaka huu wa fedha. Kwa hiyo, mitaro iliyochimbwa mkandarasi hajamalizia, maji yanakwenda kwenye makazi ya watu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tukirudi kwenye hoja mimi nina machache tu na haya machache nayazungumza kwa sababu mara zote yanazunguka kichwani kwangu siyapatii majibu.

Moja, mara kadhaa nimekuwa nikiona vitabu vikiandika kwamba pande mbili za Muungano zilikaa kujadili Muungano. Huwa nafahamu sana upande wa Zanzibar wana Baraza la Wawakilishi, kwa hiyo, huwa linakaa linakusanya kero na linawapa Wajumbe wake kwamba hizi mwende mkazisimamie kwa maslahi ya Zanzibar. Sijui wanaotoka upande wa Tanganyika huwa wanakaa wapi, wanaambiwa na nani kwamba hizi ndiyo hoja za Tanganyika mwende mkazipiganie. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili huwa sielewi kwa nini tunavunja Katiba hasa tunapokwenda kwenye sherehe za Mapinduzi. Kwenye sherehe za Mapinduzi mtakumbuka ukiacha ile ya mwaka 2016 ambayo Mheshimiwa Rais hakwenda alienda Shinyanga, mara zote Mheshimiwa Rais akihudhuria pale tunamvua madaraka yake tunamvalisha Dkt. Ali Mohamed Shein ambaye anapanda motorcade, anapigiwa mizinga 21 lakini Rais wa Jamhuri ya Muungano mwenye hadhi hiyo amekaa pembeni. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hayo mambo mawili ndiyo nilikuwa hasa nataka kuyazungumzia. Sasa nianze na la kwanza. Kwanza nawapongeza sana wenzetu Wazanzibari kwa namna ambavyo wamekuwa wamoja wakiipigania Zanzibar yao. Mara kadhaa tumeona hata wakiwa hapa ndani linapokuwa jambo ni la Zanzibar wanalipigania bila kujali wanatokea upande upi wa kisiasa na ndiyo maana wenzetu wanafanikiwa. Wametujengea picha kwamba sasa hata Serikali inafikiri kushughulikia kero za Muungano ni kwenda kujibu hoja za kutoka upande mmoja tu wa Zanzibar, wanahisi kwamba Tanganyika hakuna kero. Tanganyika kuna kero nyingi, lakini hatuna pa kusemea kwa sababu hakuna chombo ndani ya Tanganyika ambacho Watanganyika watakaa, watasema kwamba kero zetu au tungependa Muungano wetu uwe hivi. Sasa tumekataa kwenda kwenye Katiba Mpya, lakini kwa nini tusitafute mazingira ambapo Watanzania na wenyewe watapata kusema? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, namnukuu Msomi Profesa Palamagamba Kabudi ambaye kwenye hii Serikali ya Dodoma yeye ni Waziri wa Katiba na Sheria, siku moja aliwahi kusema siku moja kwamba kwenye kero za Muungano yeye haofii kero za kutoka Zanzibar kwa sababu nyingi ziko mezani na zinajadiliwa, anapata wasiwasi sana na Watanganyika ambao muda mrefu wamekaa kimya na kimsingi hatujakaa kimya, lakini tunasemea wapi? Hakuna kikao chochote mahali popote Watanganyika wanaweza wakakaa wakasema tunataka haya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ili Muungano huu uwe na tija, bora na imara ni lazima tupunguze manung’uniko kutoka kwenye pande mbili za Muungano. Muungano wenye manung’uniko hauwezi kuwa na afya. Japo kuna taswira zile kwamba watu ambao wanataka kuufanyia marekebisho Muungano ndiyo wanaonekana kama hawapendi Muungano lakini kiukweli hata nyumba yako kama unaipenda sana utakuwa unaifanyia ukarabati ili iendelee kuwa nzuri wakati wote. Kwa hiyo, msiotaka tuujadili Muungano na kujiaminisha kwamba Tanganyika haipo na wala haikuwepo, ninyi ndiyo hamuutaki Muungano kwa sababu bado hitaji la Watanganyika kukaa na kusema linaendelea kuwa la msingi. Sasa ni vizuri hili kama ni jipu Serikali mlimiliki jipu hili ili mpange hata tarehe ya kulipasua, mkiacha wananchi walimiliki watakuja kulipasua siku ambayo ninyi hamjajiandaa kushika usaha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuwafurahisha Watanganyika siyo kuwabana Wazanzibari, ni kuwaacha Watanganyika nao waseme. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuufurahisha upande huu huku, siyo lazima kuwaminya Wazanzibari kwamba labda wakitaka kujiunga na FIFA tuwakatalie, wakitaka kujiunga na IOC tuwakatalie, hapana. Tuwaunge mkono ikiwezekana wapate hata mamlaka kamili lakini na upande huu pia tupate pa kuzisemea kero zetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wa upande huu ambao hutaki niwaite Watanganyika, wa upande huu, kuna mambo ambayo kwa kweli… (Kicheko)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sidhani kama muda wangu unanitunzia maana unani- interrupt sana wakati si lazima niseme Tanzania Bara, nikisema upande huu, huku ni Bara. (Kicheko)

T A A R I F A . . .

MHE. ABDALLAH A. MTOLEA: Mheshimiwa Mwenyekiti, hilo naliacha kama halikufurahishi. (Kicheko)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini cha mwisho nachotaka kusema kwa nini tunayapora mamlaka ya Rais tunapomtaka ahudhurie Sherehe za Mapinduzi? Katiba ya Jamhuri ya Muungano, Ibara ya 33(1) na (2) inamtaja Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kuwa ndiye Kiongozi Mkuu wa nchi hii, ndiye Kiongozi Mkuu wa Serikali na ndiye Amiri Jeshi Mkuu wa Majeshi yote, lakini anapokwenda kwenye Sherehe za Mapinduzi yeye anaingia wa pili na Mheshimiwa Dkt. Ali Shein anaingia mwisho. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, maana yake ni nini? Wakati Mheshimiwa Dkt. Ali Shein anaingia, Rais wa Jamhuri ya Muungano ambaye ndiye mwenye hadhi ya kuwa wa mwisho inabidi asimame kumkaribisha anayeingia, hakuna itifaki ya namna hii duniani hapa. Ingekuwa ni busara kwenye sherehe zile Mheshimiwa Rais asiende, anaweza kwenda Naibu Waziri wa Mazingira akawakilisha Serikali ili Mheshimiwa Dkt. Shein anapoingia awe mkubwa.