Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa mwaka wa Fedha 2018/2019 - Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa na Ofisi ya Rais, Utumishi na Utawala Bora

Hon. Zainab Mndolwa Amir

Sex

Female

Party

CUF

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa mwaka wa Fedha 2018/2019 - Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa na Ofisi ya Rais, Utumishi na Utawala Bora

MHE. ZAINAB M. AMIR: Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote nami napenda kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunipa afya njema ya kuweza kuchangia katika ofisi ya TAMISEMI na ofisi ya Utumishi na Utawala Bora.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaipongeza Wizara ya TAMISEMI kwa kazi nzuri inayoifanya. Naipongeza kwa juhudi kubwa anazozifanya Mheshimiwa Jafo katika Wizara yake, hususani katika kazi zake zinazoonekana dhahiri katika kujenga vituo vya afya pia katika kujenga zahanati, na pia namshukuru sana kwa kupandisha Hospitali yetu ya Temeke kuwa Hospitali ya Rufaa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninachokiomba na kushauri Serikali; Hospitali ya Wilaya ya Temeke imepandishwa hadhi kuwa Hospitali ya Rufaa lakini hospitali ile inachukua wagonjwa kutoka Wilaya za karibu hususani Mkuranga na Wilaya ya Kigamboni.

Nakuomba Mheshimiwa Waziri, najua kuna utaratibu unafanya kuboresha zahanati zilizokuwa Mkuranga pamoja na Kigamboni; naomba wakati unafanya utaratibu huo uitupie macho Hospitali ya Temeke. Hospitali hii wodi zake zile kweli ni chakavu na ni za siku nyingi. Nakuomba sana uipe kipaumbele, uiboreshe, kwa sababu wananchi wa Mkuranga wakipata transfer ni lazima waende Tumbi na Tumbi ni mbali sana kutokana na jiografia yake kwa hiyo wanachotakiwa ni kuwaleta Temeke. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wakati Mheshimiwa Jafo unaandaa mazingira nakuomba sana Hospitali yetu ya Wilaya ya Temeke ambayo sasa hivi ndio itakuwa ni hospitali ya rufaa iboreshwe, majengo yake yawe ya hadhi ya rufaa. Kwa sababu eneo ni dogo nashauri Wizara angalau zile wodi namba moja, namba mbili , namba tatu majengo yake yawe ya ghorofa ili iweze kukidhi idadi ya wagonjwa. Pia si majengo tu kuna vifaa muhimu pia vinatakiwa hospitali vifaa kama x- ray mmejitahidi, lakini vifaa vingine ni vile vidogo vidogo lakini tunaona si vya muhimu. Katika wodi za wagonjwa lazima kuwe na vikabati vya kuhifadhia chakula. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Waheshimiwa ukifika Hospitali ya Temeke sasa hivi kuna matatizo, unapompelekea mgonjwa wako chakula unaweka chini chakula hakuna vikabati vya kutosha kwa hiyo naomba sana katika kuboresha hizo hospitali na vifaa vingine ambavyo mnaviona ni vidogo vinahudumia wananchi, vinahudumia wagonjwa wote ni muhimu sana katika hospitali zetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kuchangia katika Hospitali ya Rufaa ya Muhimbili. Ni ukweli usiopongika kwamba Hospitali ya Muhimbili inachukua wagonjwa wengi kutoka mikoa mbalimbali Tanzania Bara na Visiwani. Serikali imejitahidi katika kujenga vyumba vya upasuaji na kuongeza wodi, lakini kuna changamoto moja inayoikabili hospitali ya muhimbili naona watu wengi hawaioni, lakini sisi wakazi wa mjini Dar es Salaam tunaiona. Si wagonjwa wote wanaoletwa katika Hospitali ya Muhimbili wana wenyeji katika Mkoa wa Dar es Salaam. Wanapopewa rufaa wakifika pale emergence na kukabidhi wagonjwa wao huwa wanaambiwa kwamba mgonjwa wako ameshapatiwa kitanda, kwa hiyo yeye aondoke.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wengine hawana ndugu wala jamaa Dar es Salaam. Tunaiomba Wizara angalau itenge jengo maalum ambalo litasaidia wale wasindikizaji ambao wanakuja kuleta wagonjwa wao waweze kupata eneo la kijisitiri na kusubiri matokeo ya wagonjwa wao kama ni vipimo na kuwahudumia. Kuna huduma nyingine haziwezi kufanywa na daktari, haziwezi kufanywa na nesi. Nurse hawezi akamlisha mgonjwa, kufua nguo za mgonjwa na labda mgonjwa akiwa amejisaidia, ni mtu wa karibu mno anatakiwa azifanye zile huduma.

Kwa hiyo, naomba sana Mheshimiwa Jafo, Hospitali ya Muhimbli ipatiwe eneo maalum ambalo litakalokuwa na wahudumu watakaoweza kukaa na kuwaona wagonjwa wao jinsi wananvyoendelea na vipimo na kuweza kuwasaidia katika mambo mbalimbali. Kama ikiwezekana wawe na hata identy card ya kuonesha kwamba huyu mgonjwa wake yuko Sewa Haji au yuko Kibasila. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ili iweze kusaidia hata wale walinzi wetu wawapo katika maeneo ya ulinzi naomba sana hospitali zetu; nitolee mfano Hospitali ya Mwananyamala; naitolea mfano; ukipeleka mgonjwa hospitali ya Mwananyamala na Mwenyezi Mungu akamtanguliza mbele ya haki akitoka wodini, anapopelekwa chumba cha maiti ili kumtoa kila siku ni 20,000. Akikaa siku 10 ni shilingi 200,000, akifia nyumbani na kuletwa ndani kwenye mortuary ya hospitali unakuta anakuwa-charged shilingi 30,000. Sisemi utofauti wa malipo ninachosema yule ni Mtanzania halisi ambaye wakati wa uhai wake alikuwa analipa kodi na kodi hiyo ilikuwa inalipwa na Serikali inakusanya, iweje Mtanzania huyu amekufa na ametibiwa na ndugu zake kwa gharama nyingi sana maiti mnaitoza malipo? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nawaombeni kama inawekana, kwa ushauri wangu nawaomba mtoe yale malipo ya maiti. Nadhani pale mimi ninatolea mfano tu, kuna hospitali nyingi naona Waheshimiwa Wabunge sidhani kama mmefanya uchunguzi, ukiweka maiti yako hospitali si kama unaweka kwa sababu hutaki kumzika, huenda unasubiri ndugu na jamaa; kwa kweli gharama ni kubwa sana. Huyu maiti wa Tanzania ni Mtanzania alikuwa analipa kodi.

Naomba sana Mheshimiwa Jafo uliangalie kwa makini katika bajeti yako, muondoe haya malipo ya kumtoa maiti wetu katika hospitali hizi za Serikali, iwe huduma kama huduma nyingine. Kwa sababu inaonekana kama tumekosa sehemu nyingine ya kukusanya mapato, tutafute eneo lingine Serikali si kwenye maiti, tuwaonee huruma wafiwa na tumuonee huruma pia marehemu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuzungumzia pia Hospitali ya Mkoa wa Morogoro. Hospitali ya Mkoa wa Morogoro chumba chake cha kuhifadhia maiti kipo nje ya uzio wa hospitali na kiko karibuni sana na shule ya sekondari ya Morogoro.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi nilisoma pale miaka ya 1980, ni kero sana ile mortuary, iko karibu na madarasa kiasi kwamba ndugu waliofiwa na ndugu yao wakati wanakuja kuchukua marehemu wao wanahisia mbalimbali wengine hulia, wengine huja pale labda kuaga kwa mapambio na mwalimu anapofundisha darasani hakuna usikivu. (Makofi)

Naombeni Mheshimiwa Jafo wakati unapanga bajeti yako uliangalie kwa jicho la huruma wanafunzi wa Morogoro Sekondari wanapata tabu kwa kuwepo chumba cha maiti karibu na madarasa. Naomba ulifanyie kazi kwa sababu hili ni tatizo kubwa ingawa Mheshimiwa Abdul-Azizi ataniunga mokono ni Mbunge wa Morogoro na anaona tatizo hili, yeye alisoma Forest, mimi nimesoma Morogoro miaka ya 1980 lakini tatizo ni kubwa sana. Hata wakati mnafanya mtihani mwalimu unakuta anaweka stop watch kwa sababu wangoje zile kelele zipungue, nawaombeni muhamishe ile mortuary ilipo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine napenda kuchangia kwenye utawala bora, muda hautoshi mambo ni mengi. Kuna baadhi ya Wakuu wa Mikoa na Wakuu wa Wilaya wanawaweka ndani kwa masaa 24 wananchi wetu bila sababu na wakati mwingine sababu zenyewe hazijulikani, anakuambia wewe kaa ndani. Sasa nataka Serikali inijulishe, je, kama kuna sheria hii ni makosa gani ambayo Mkuu wa Mkoa au Mkuu wa Wilaya anatakiwa amuweke mtu ndani kwa masaa 24?

Mheshimiwa Mwenyekiti, ikibainikwa kwamba amemuweka kimakosa, je, Mkuu wa Mkoa au Mkuu wa Wilaya atachukuliwa hatua gani? Maana sasa hivi hatuelewi, hata sheria kila mtu anachukua mamlaka mikononi. (Makofi)

Nakuomba Mheshimiwa George Mkuchika unijibu swali hili, ni sheria gani inawaruhusu wakuu wa mikoa na wakuu wa wilaya kuwaweka ndani wananchi na baadae anawatoa? Je, ikibainika kwamba hana kosa lolote je, Mkuu wa Mkoa au Mkuu wa Wilaya atachukuliwa hatua gani? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hawa ndugu tuliwarudisha juzi wa darasa la saba, wengine wamefariki, je, Serikali ina mpango gani kwa wale ndugu ambao jamaa zao wamefariki; na hapa juzi tumetangaza kwamba waterejeshwa, je, stahiki zao zitakuwaje? (Makofi)

Kwa hiyo, naomba wakati wa kutoa maelezo tufahamishwe, kwamba stahiki za wela ambao wamepoteza maisha wengine kwa presha tu baada ya kusimamishwa, je, stahiki zao zitapatika vipi? Kwa sababu wameondoka mbele haki wameacha familia na juzi tumesema kwamba warudi makazini na hawapo duniani? Tunaomba Serikali itupe majibu kwa wale ambao wametangulia mbele ya haki na sheria imesema warudi kazini, walipwe mishahara yao tangu pale waliposimamishwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni mengi ya kuyazungumza lakini naomba sana walimu wengi wana matatizo, wengi wamezungumza, na sisi wote tumepita kwa walimu lakini sekta hii hatuipi uzito.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusiana na kuongeza mishahara nashauri walimu wawe wa kwanza, utaona, kwamba utakapowaongezea mishahara walimu wengi, hata kama mtu kapata division one atakuwa interest ya kusoma ualimu. Kama walimu wangekuwa wanalipwa mishahara kama tunayolipwa sisi, wengi na mimi pia ni mwalimu nisingekuwa hapa, lakini kutokana na ualimu kuonekana kama ni kazi dhalili watu wengine wanaacha ile kazi wanaondoka. Kwa hiyo, naomba sana tuwaboreshee walimu mishahara yao stahiki zao ili waweze kufanya kazi kwa weledi. Watakapofanya ya kazi kwa weledi wanafunzi wetu watafaulu vizuri kwa kiwango cha juu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo nashukuru sana, naomba haya yasiishie kwenye vitabu hivi tu, mmeandika mambo mazuri lakini yasiiishie kwenye maandishi. Hii bajeti iliyopagwa itolewe kwa wakati ili muweze kufanya kazi zenu barabara, ahsanteni sana.