Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi kwa mwaka wa fedha 2016/2017.

Hon. Joseph Michael Mkundi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Ukerewe

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi kwa mwaka wa fedha 2016/2017.

MHE. JOSEPH M. MKUNDI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kupata fursa hii. Kwa kuwa ni mara yangu ya kwanza kuchangia bajeti, natumia fursa hii kuwashukuru sana wananchi wa Jimbo la Ukerewe kwa kunituma katika chombo hiki muhimu. Mchango wangu utajikita kwenye maeneo matatu yote lakini kwa mazingira tofauti.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nikianza na eneo la kilimo, wamesema wachangiaji wengi hapa kwamba kwa mazingira tuliyonayo na kwa kuamini kwamba kilimo ni uti wa mgongo wa uchumi wa nchi hii, ni muhimu sana tukahusisha utafiti halafu ndiyo tukapanga mipango yetu ili kuboresha mazingira ya kilimo na kwa maana hiyo hali ya uchumi wa wananchi wetu.
Hata kama tutafanya research, tukaandaa mipango, bila kuitekeleza bado haitakuwa na msaada mkubwa sana kwa maendeleo ya nchi yetu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naishauri Serikali, wakati tunapokuwa tunapanga mipango hususan kupitia Bunge hili, basi tuitekeleze kwa namna tunavyoipanga hasa kama Serikali itatoa pesa kwa kiwango kile ambacho Bunge linakuwa limepitisha.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nina changamoto nyingi sana; kwa mfano, kwenye eneo la Ukerewe bahati mbaya sasa ardhi ya Ukerewe imechoka na Serikali mwaka juzi iliahidi kwamba ingeleta watu kwa ajili ya kufanya research ili sasa ione namna gani itafanya; kwa sababu Ukerewe tulitegemea zaidi zao la muhogo, lakini zao lile sasa linakumbwa na matatizo mengi likiambatana na kuchoka kwa ardhi. Mpaka leo hakuna utafiti wowote uliofanyika kwenye eneo lile ili kuwezesha wananchi wa Ukerewe ambao sasa imekuwa kila wakati wanakabiliana na upungufu wa chakula, waweze kukabiliana na jambo hili.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, wakati wa ku-wind up labda Waziri angeweza kusema ni wapi ambapo amefikia juu ya jambo hili. Bahati mbaya zaidi, mwaka 2015 ilikuwa Ukerewe wapate mgao wa voucher za pembejeo; na kimsingi kwa mazingira ya mvua, ilitakiwa at least mwezi Septemba voucher hizi ziwe zimekuja ili wakulima wapate pembejeo na vifaa vilivyokuwa vinatakiwa, lakini mpaka mwezi Novemba vitu hivyo havikuwa vimetolewa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, bahati mbaya sana ni kwamba wananchi wali-reserve baadhi ya maeneo ili kwamba baada ya kupata zile pembejeo waweze kutumia maeneo hayo. Hawakuweza kuyatumia na mpaka sasa maeneo yale yamebaki bila kutumika pamoja na uhaba wa ardhi uliopo kwenye eneo la Ukerewe.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, suala la voucher za pembejeo, wamesema Wabunge wengi hapa, ni jambo muhimu sana na kwa eneo kama Ukerewe ardhi ni chache, ardhi imechoka, kuna tatizo kubwa sana la upungufu wa chakula, ni lazima Serikali itilie mkazo na ione umuhimu wa jambo hili.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tuna wataalamu wa kilimo kwenye maeneo yetu, lakini bahati mbaya sana kwenye bajeti tunazo zipanga Serikalini pesa haitoki kushuka kwenye maeneo yale kuweza kusaidia wataalam kufanya na kutekeleza majukumu yao. Tumetoa miongozo, kwa mfano, Serikali imetoa miongozo kwamba wataalam waende kwenye maeneo ya vijiji kutembelea wakulima, lakini pesa zile zinazoweza kuwawezesha wataalam hao kwenda kwenye maeneo ya wakulima hazitoki. Tuchukulie kwa mfano Ukerewe, Idara ya Kilimo OC kwa mara ya mwisho wamepata mwezi Februari mwaka 2015. Wakati huo huo wanawaelekeza wataalam hao waende vijijini kusisitiza mambo ya kilimo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hebu Serikali iwe serious na jambo hili ili kwamba wakati tunapoandaa mipango, tunapokuwa tunatoa maelekezo ya kutekeleza sera, basi tupeleke rasilimali fedha ili wataalam wetu wafanye majukumu yao kwa mujibu wa maelekezo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hilo, Ukerewe pale ili kukabiliana na hili tatizo la njaa tuna mabonde pale ambayo tungeweza kuyatumia kwa ajili ya kilimo cha mpunga. Tuna bonde kwa mfano la Mihogwezi, tuna bonde la Muhande, tuna bonde Ilangala labda Mheshimiwa Waziri atakapokuja wakati ana-wind up atoe maelezo kwamba ni wapi kwa mfano kuna bonde la Mihogwezi. Tume-invest pale!
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali imewekeza pesa zaidi ya shilingi milioni 700, lakini sasa bonde lile liko pale pamoja na pesa zile tume-dump pale, liko vilevile. Sasa Serikali ina mpango gani na bonde hili, pamoja na kutumia mabonde mengine haya ili kwamba tuweze kukabiliana na tatizo la upungufu wa chakula linaloikabili Ukerewe lakini pamoja na maeneo mengine yote. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye eneo la mifugo, wamesema wachangiaji wengi hapa lakini mimi nitaongelea kwenye eneo moja tu. Kuna mchangiaji mmoja amesema tuna chuo ambacho kinafundisha wataalam wetu lakini wataalam hawa hatuwatumii, wako mitaani.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Ukerewe tuna Kata 25, lakini tuna Maafisa Ugani saba pekee. Kwa hiyo, unaweza kuona ni upungufu kiasi gani uliyopo kwa wataalam hawa ambao ni muhimu sana wa ajili ya kuwasaidia wakulima wetu kufanya shughuli hizi katika kiwango kizuri kikawa na tija na kikasaidia jamii kwa ujumla wake. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo lingine ambalo ningependa kuongelea ni eneo la uvuvi. Namshukuru Mheshimiwa Waziri, mara kadhaa tumeonana katika kujadiliana juu ya suala hili la uvuvi na ninashukuru kwa ushikiano wako, lakini bado kuna changamoto ambazo Serikali ni muhimu sana ikazifanyia kazi. Baadhi umezisema kwenye hotuba yako, kwa mfano, suala la tozo nyingi ambazo wavuvi hawa wanakabiliana nazo, ni muhimu sana sheria hii ikaangaliwa upya tozo hizi zikapunguzwa ili wavuvi wafanye shughuli zao kwa tija.
Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile sheria inayoelekeza aina ya nyavu ambazo zinatumika kwenye Ziwa Victoria, ni jambo muhimu sana. Kwa mfano, kwa sheria ile ya mwaka 1983 kama sikosei, inaelekeza uvuvi wa dagaa kwa mfano kwenye Ziwa Victoria kutumia nyavu zenye matundu ya milimita 10.
Mheshimiwa Mwenyekiti, huwezi kupata dagaa wa milimita 10 kwenye Ziwa Victoria. Ile research inawezekana ilifanyika kwa Ziwa Tanganyika, lakini dagaa walioko katika Ziwa Victoria hawakui zaidi ya kiwango kile walichopo ambacho ni kama milimita sita tu. Bahati nzuri ni kwamba dagaa wanavuliwa kwenye kina kirefu, siyo kwa kuvutwa, ni kwa kuchotwa.
Kwa hiyo, huwezi kutegemea kwamba kwa sheria ile mvuvi katika Ziwa Victoria atapata chochote. Ni lazima sheria ile iangaliwe ifanyiwe marekebisho iendane na mazingira halisi ya Ziwa Victoria. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ambalo ni muhimu sana ni suala la usalama kwenye Ziwa Victoria. Watu wameimba sana, wamepiga kelele sana, naomba tafadhali Mheshimiwa Waziri alitilie mkazo, ashirikiane na Wizara nyingine zinazohusika.
Mheshimiwa Mwenyekiti, wavuvi wanataabika sana kwenye Ziwa Victoria. Imagine watu wanafanya shughuli zao kwenye Ziwa Victoria, wamechukua rasilimali zao wakawekeza pale, watu wachache wanaenda wanawanyang‟anya rasilimali, wanawakata mapanga, wanawaua, wananyang‟anya mali zao, siyo jambo jema kuendelea kwenye nchi kama hii ya kwetu. Lazima tuwe serious na jambo hili, tulikomeshe kwa gharama yoyote ile, watu wetu wafanye shughuli zao za kiuchumi wakiwa na amani wapate rasilimali zile wanazozitarajia, waboreshe maisha yao. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine kwenye maeneo yanayotoa madini, kumekuwa na habari ya mrahaba. Hivi katika maeneo yanayozungukwa na ziwa ambapo samaki wanatoka kwenda kwenye viwanda vya kuchakata samaki, hakuna namna yoyote ambayo katika mapato yanayotokana na ziwa, asilimia fulani ya mapato yale yakarudi kwenye maeneo yale kusaidia uharibifu wa mazingira kwenye maeneo yale? Kwa sababu kutokana na shughuli za uvuvi, mazingira yanaharibika sana, jamii inaharibika kitabia, kwa mfano, watoto wanashindwa kwenda shule na matatizo mengine kama hayo. (Makofi)
Kwa hiyo, iangaliwe namna ambayo wakati shughuli za uvuvi zinapofanyika, samaki wanapopelekwa viwandani, basi viwanda vile angalau vitozwe asilimia fulani ambayo itarudi kwenye maeneo yale kuweza kusaidia jambo hilo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante.