Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Ofisi ya Waziri Mkuu

Hon. Susan Anselm Jerome Lyimo

Sex

Female

Party

CHADEMA

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Ofisi ya Waziri Mkuu

MHE. SUSAN A.J. LYIMO: Mheshimiwa Mwenyekiti, mosi, nitoe pole kwa Mheshimiwa Spika na kumshukuru Mungu kwa ajili yake.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nichukue fursa hii kutoa pole nyingi sana kwa viongozi wangu Wakuu wa CHADEMA akiwemo Mwenyekiti Taifa, Katibu Mkuu na Manaibu Makatibu Wakuu na wajumbe wa Kamati Kuu waliopata misukosuko mingi wakati wakitetea demokrasia ya Taifa letu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kipekee nimpongeze na kumtia moyo Mheshimiwa Sugu (Osmond Mbilinyi), Mbunge wa Mbeya Mjini anayetumikia kifungo katika Gereza la Mbeya. Naamini haya yote yatapita kama upepo uvumapo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimesoma zaidi ya mara mbili hotuba ya Waziri Mkuu kuna maeneo mengi hayana ukweli na hayana uhalisia wa yanayotokea hapa nchini. Nikianza na mafanikio ya Awamu ya Tano kujenga ari ya uzalendo, kudumisha amani, utulivu na mshikamano. Jambo hili limenishangaza kwa kuwa uzalendo msingi wake mkuu ni upendo na uelewano na ndiyo maana uzalendo haujengwi kwa kampeni bali kwa mahusiano mema na hivyo huja automatically. Vilevile hatuwezi kuwa na mshikamano au umoja kama kuna chuki, ubabe, matumizi mabaya ya dola kama ilivyo sasa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakubaliana na kuwa ulinzi na usalama dhidi ya upinzani umeimarishwa sana na ndiyo sababu kila leo ni wapinzani kukamatwa na polisi au kuripoti polisi na mahakamani. Mbaya zaidi hata walipopata dhamana ile siku ya Alhamisi Kuu eti gari za magereza zikawa mabovu wakati Kisutu Mahakamani magari mengi yalikuwepo bila kazi yoyote.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hali hii ilipelekea viongozi hawa kuendelea kusota Segerea gerezani. Pia hata wafungwa na mahabusu waliokuwa wapelekwe Mahakama Kuu na nyinginezo walikosa kufika. Hii ni kinyume kabisa na huu ni ukiukwaji wa haki za binadamu na haki za mfungwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kauli hii imerejewa tena ukurasa wa 10 pale anapozungumzia masuala ya siasa baada ya miaka 26 ya Vyama Vingi nchini kuwa ni jukumu la kila chama kunadi sera zake. Najiuliza unanadi vipi sera wakati mikutano ya hadhara imezuiwa? Huku chama tawala kikifanya kupita Mwenyekiti wake wa Chama kwa kofia ya Urais huku wengine kina Mheshimiwa Mbowe, Mheshimiwa Mbatia, Mheshimiwa Zitto, Mheshimiwa Cheyo na kadhalika ambao ni Wenyeviti wa Vyama Taifa wakikosa fursa hiyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, natambua Wabunge na Madiwani kuruhusiwa kufanya mkutano ndani ya maeneo yao lakini ni wazi lengo la uanzishwaji wa vyama vingi na kazi ya vyama ni mikutano kwa ajili ya kupata wanachama. Hivyo ni ombi na rai yangu kuwa zuio hili liondolewe na kufuata Sheria ya Vyama vya Siasa ya 1992 iko wazi kwamba vyama vya siasa vitanadi sera zake sasa vitanadi vipi wakati Mheshimiwa Rais ameweka zuio?

Mheshimiwa Mwenyekiti, unahamasishaje ujenzi wa demokrasia kwa wananchi wote kukiwa na ubaguzi ulio wazi? Ni jambo la ajabu sana kwamba katika awamu hii ubaguzi wa wazi wazi umetamalaki kinyume kabisa na tunu muhimu tulizoachiwa na Baba yetu wa Taifa. Tumemsikia Mheshimiwa Rais akisema hawa wamenipa kura msiwabomolee hata kama wamejenga ndani ya eneo la barabara au sehemu za vyuo na taasisi za Serikali huku wengine wakibomolewa tukiamini hawakumpa kura. Imani yangu ni kuwa unaposhinda wewe ni kiongozi wa wote.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la mshikamano kama nilivyosema unafanywa kwenye misingi ya upendo na umoja na ndiyo tunu muhimu kwa Taifa lolote vinginevyo tutakuwa tunajidanganya tukisema kuna mshikamano na amani. Niliposikia Wajumbe wa Kamati ya Viwanda na Biashara wakitaka kwenda kumtembelea mjumbe mwenzao Mheshimiwa Godbless Lema gerezani Arusha na zoezi hilo likakwama na baadaye Mwenyekiti na Makamu wake kuachia nafasi zao kutokana na sababu hiyo sikuamini kabisa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ila sasa naamini kwa kuwa Kamati yetu ya Huduma na Maendeleo ya Jamii tulipokwenda kutembelea miradi ya maendeleo tulipofika Mbeya na kufika kwa RC na kwa kuwa ilikuwa weekend tulidhani ni busara kwenda kumtembelea Mheshimiwa Sugu, lakini cha ajabu hakuna Mbunge hata mmoja wa CCM aliyeambatana nasi jambo lililonithibitishia kuwa haiyumkini lililotokea Kamati ya Viwanda na Biashara ni kweli.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na hayo, kama kweli tungekuwa na mshikamano tuliouzoea Mheshimiwa Lissu angetembelewa na Wabunge wote bila kujali itikadi katika kipindi kirefu alipolazwa Nairobi Hospital. Katika hali hii ni wazi hatuwezi kusema tuna mshikamano kama viongozi. Ni ushauri wangu kuwa ni muhimu kutembea kwenye maneno yetu bado hatujachelewa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa masikitiko makubwa Ofisi ya Msajili ambayo kimsingi ndiye mlezi wa vyama vyote vya siasa, imekuwa ama kwa makusudi ama kwa kujua na hasa ukizingatia Jaji ni msomi na ameapa kulinda Katiba yetu, cha ajabu anakubaliana na zuio la mikutano huku chama tawala kikifanya mikutano inayoongozwa na Rais ambaye ni Mwenyekiti wa Chama cha Mapinduzi. Nilitegemea Mheshimiwa Jaji Mutungi angekemea hili lakini amekuwa akiandika barua vyama vya upinzani kujieleza pale ambapo wanatimiza majukumu yao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu uwezeshwaji wa wananchi, ni ushauri wangu kuwa elimu kuhusu mikopo itolewa kwa wakopaji ili wasije kunadiwa mali zao kwa kushindwa kurejesha. Vilevile kuna tuhuma nyingi kuwa mikopo hii inatolewa kiitikadi na hivyo wasio wanachama wa chama tawala wanatengwa. Naomba kama ni kweli jambo hili liachwe mara moja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, UKIMWI bado ni tishio na hivyo ni muhimu sana sisi kama Taifa tuwe na vyanzo maalum vya fedha kwa ajili ya UKIMWI kwa kuwa bado fedha/dawa kwa asilimia mia moja tunategemea wafadhili wa nje. Ni muda muafaka sasa ule mfuko ulioimbwa muda mrefu utaanza basi uanze.