Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi kwa mwaka wa fedha 2016/2017.

Hon. Daimu Iddi Mpakate

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Tunduru Kusini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi kwa mwaka wa fedha 2016/2017.

MHE. MPAKATE D. IDDI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Kwanza kabisa, naomba nitoe shukurani kwa kuniteua leo kuwa mchangiaji katika bajeti ya kilimo.
Pili, namshukuru Mwenyezi Mungu kwa kuniwezesha leo nikiwa salama kuongea katika Bunge lako kwa mara ya kwanza. Pia napenda niwashukuru wapiga kura wangu wa Tunduru Kusini na Tunduru kwa ujumla walioniwezesha leo kuwa ndani ya Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, bila kukosa fadhila, nakishukuru chama changu, Chama cha Mapinduzi kwa kuniteua kuwa mgombea wa Jimbo la Tunduru Kusini na hatimaye kuhakikisha kwamba ninashinda na leo niko ndani ya Bunge hili. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, tatu, napenda kumpongeza Waziri wa Kilimo kwa hotuba yake nzuri ambayo ameiwasilisha leo. Nami napenda sehemu ya hotuba hiyo nichangie mambo mawili matatu ambayo najua yakirekebishwa, basi utendaji wetu utaendelea vizuri na wakulima wetu watapata manufaa mazuri na kulima zaidi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, moja, ni suala la pembejeo. Namshukuru sana Mheshimiwa Waziri amelieleza vizuri. Kero ya voucher imekuwa ni donda ndugu, kwa kweli lilikuwa linatugombanisha na wakulima wetu; mahali penye kaya 2000, kaya 30 zinapata voucher, matokeo yake inaleta migongano katika vijiji vyetu.
Nashukuru sana kwa kuliona hili, lakini pamoja na kuahidi kwamba pembejeo zitauzwa kama soda, ni vyema Mheshimiwa Waziri uhakikishe kwamba unaweka bei dira, bei elekezi ya hizo pembejeo kama wanavyofanya EWURA ili kila mkulima ajue kwamba katika eneo lake pembejeo itapatikana kwa bei fulani.
Mheshimiwa Mwenyekiti, bila kufanya hivyo, wafanyabiashara ambao ni mawakala watakaosambaza pembejeo zile, watatumia mwanya ule ule kuendelea kuuza bei juu kuliko vile ilivyokusudiwa na Wizara. Naomba sana jambo hili litiliwe mkazo ili kuhakikisha kwamba wakulima wetu wanapata fursa nzuri ya kupata pembejeo kwa bei nzuri na mahali walipo ili kuendeleza kilimo chetu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ambalo ni la muhimu ni suala la umwagiliaji. Ninachojua mimi katika dhana ya umwagiliaji ni kuhakikisha kwamba kilimo kinaendelea through out the year, kwamba mkulima anakuwa analima kifuku na kiangazi, lakini umwagiliaji uliopo sasa katika maeneo mengi, kilimo kile kinakuwa ni kilimo cha umwagiliaji wakati wa kifuku tofauti na kusudio lile la kulima through out the year. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli wataalam wetu wanatakiwa waende mbali zaidi kuhakikisha kwamba ile mifereji inayotengenezwa kwa ajili ya kifuku peke yake, tuone namna nyingine ya kutengeneza mifereji kwa ajili ya kulima kipindi cha kiangazi. Maeneo mengi yaliyotengenezwa kwa ajili ya kilimo hiki yanatumika kifuku badala ya kiangazi kama inavyokusudiwa na dhana yenyewe ya umwagiliaji. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, tatu, naomba nielezee suala mtambuka la ushirika. Kwanza naomba ni-declare interest kwamba mimi ni mmojawapo wa watumishi wa ushirika ndani ya miaka nane katika sekta ya korosho.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Waziri amesema kuhusu kuanzisha commission ya ushirika. Ni kweli ushirika umedorora lakini tunasahau wapi tulipojikwaa, tunaangalia tulipoangukia. Kamisheni hii kwa kweli haina nguvu kwa mujibu wa taratibu za kikazi. Utakuta kamisheni haina watumishi mikoani; kamisheni haina watumishi Wilayani, inategemea watumishi kutoka Halmashauri za Wilaya ambao katika utendaji wa kazi wanawajibika kwa Wakurugenzi wa Wilaya. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kweli hili ni tatizo, utendaji hauendi sawasawa kama kamisheni ilivyokusudia kwa ajili ya kufufua ushirika. Mbaya zaidi, hata hao watumishi waliokuwepo katika Halmashauri, hawatoshi kusimamia ushirika. Ni hali ya hatari, utakuta Wilaya ina vyama 20, 40, SACCOS pamoja na Vyama vya Wakulima, lakini Afisa Ushirika utamkuta mmoja au wawili. Inakuwa ni ngumu! Ni kazi kubwa kwa Maafisa Ushirika kuhakikisha kwamba vyama vile vinakwenda kama inavyokusudiwa na kama sheria inavyotaka. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ombi langu, commission ipewe nguvu, iwe na watumishi wa kutosha mpaka Wilayani ili waweze kusimamia Vyama vya Ushirika vizuri viweze kuwasaidia wakulima wao. Tunajua bila ushirika maeneo mengi kwa kweli inakuwa ni tatizo kubwa ingawa wenzangu wameeleza, ushirika ni jumuiya ya hiari, kwa hiyo, wanaushirika wenyewe wafanye yale yanayotakiwa ili kuhakikisha ushirika unaboreshwa kama inavyoeleweka. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na hilo jambo la ushirika, kuna jambo la mikopo. Nashukuru ndugu yangu ameeleza kuomba kupeleka Benki ya Kilimo katika Mkoa wa Ruvuma.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Ruvuma ni eneo mojawapo ambayo wanazalisha sana mahindi, lakini tukiangalia suala la mikopo hali siyo nzuri kwenye Benki zetu za kawaida. Riba inakuwa kubwa haimwezeshi mkulima kukopa na kupata return ya kuweza kurudisha faida na yeye mwenyewe kupata chakula kwa ajili ya maisha yake na familia yake ilivyo.
Tunaomba sana suala la benki lifanyiwe hima kuhakikisha kwamba Benki za Kilimo zinakwenda mikoani ili kuweza kuwasaidia wakulima walio wengi kwa kupata mikopo iliyokuwa nafuu ili waweze kuendeleza kilimo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la mwisho ni suala la uhifadhi wa chakula, ni aibu! Nimesema nimekuwa kwenye sekta ya kilimo kwa muda wa miaka nane. Ukienda vijijini maghala ya kuhifadhia mazao hakuna na ndiyo maana utakuta sehemu kubwa iliyopo tunazalisha vizuri lakini uhifadhi wa mazao unakuwa ni tatizo. (Makofi)
Kuhusu ile programu ambayo ilikuwepo miaka ya nyuma ya kuhakikisha kwamba kila kijiji kinapata ghala la kisasa, basi naomba Mheshimiwa Waziri utakapokuja, atuhakikishie angalau vijiji vile ambavyo vinaonekana uzalishaji wa mazao ni mkubwa waanzishiwe miradi ya kujenga maghala kwa ajili ya kuhifadhi mazao yao. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuunga mkono hoja, kwa hayo machache, nashukuru sana kwa kuniruhusu kuchangia mawili, matatu, ahsante sana.