Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Ofisi ya Waziri Mkuu

Hon. Juma Kombo Hamad

Sex

Male

Party

CUF

Constituent

Wingwi

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Ofisi ya Waziri Mkuu

MHE. JUMA KOMBO HAMAD: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nikupe pole na nimwombe Mwenyezi Mungu akujalie uendelee kuwa na afya njema.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la demokrasia na utawala bora na haki za binadamu nchini mwetu linapotea kila siku. Leo Tanzania, wananchi wanatekwa na kuuawa, wanasiasa na wanaharakati pia wanahujumiwa na Tanzania hata waandishi wa habari na vyombo vya habari hawako salama. Hali hii haileti afya kwa Taifa. Tunaiomba sana Serikali na Wizara ya Mambo ya Ndani, usalama kwa wananchi ni jambo muhimu kwa mustakabali wa amani ya Taifa letu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hivi tunavyozungumza kuna vijana sita Pemba wametekwa na wa watatu kati yao hadi sasa hawajulikani walipo. Vijana hawa wametekwa Pemba Jimbo la Mtambwe na hadi sasa vijana watatu hawajaonekana nao ni Thuwein Nasor Hemed (30), Khamis Abdallah Mattar (25), Khadid Khamis Hassan (30). Tunaomba Serikali itupe jibu, je vijana hawa wapo wapi?

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la sukari ya Zanzibar kuzuiwa kuuzwa Tanzania Bara sio haki na ni uonevu mkubwa Zanzibar na maendeleo ya Wanzanzibari, jambo hili halileti afya kwa Muungano wetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la kodi hasa katika Bandari ya Dar es Salaam ni tatizo na ni kero kubwa, mustakabali wa biashara kwa wafanyabiashara wa Zanzibar. Tunaiomba sana Serikali kulifanyia kazi suala hili ili kuleta nafuu kwa wafanyabiashara wa Zanzibar.

Mheshimiwa Mwenyekiti, msamiati wa kero za Muungano sasa imekuwa hadithi zisizo na tija kwani kila siku kero hizi zinaongezeka na kuzidi kudumaza maendeleo ya Zanzibar. Kama suala hili halikupatiwa ufumbuzi linaweza kutikisa Muungano hatimaye kuvunjika kabisa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la kuwaweka watu mahabusu kwa muda mrefu bila kuwafikisha Mahakamani sio jambo jema. Suala la Mashekhe wa Uamsho na dhuluma wanayofanyiwa sasa imekuwa haivumiliki tena. Ni lazima Serikali kutoa jibu juu ya Mashekhe hawa. Sasa ni miaka mitano wapo ndani bila kufikishwa Mahakamani, hii sio haki.

Mheshimiwa Mwenyekiti, huu ni uonevu uliovuka mipaka na uvumilivu unafika mwisho. Ahsante sana.