Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Ofisi ya Waziri Mkuu

Hon. George Boniface Simbachawene

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kibakwe

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Ofisi ya Waziri Mkuu

MHE. GEORGE B. SIMBACHAWENE: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa nichukue nafasi hii kumpongeza sana Mheshimiwa Waziri Mkuu kwa ahotuba yake nzuri sana na niwapongeze pia Mawaziri Mheshimiwa Jenista na wasaidizi wake wanafanya kazi nzuri sana tunawaona na tunawatia moyo endeleeni hivyo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nchi yoyote ile duniani inaongozwa kwa dira na kwa sisi Tanzania dira yetu ni ya 2025 na kwa sasa tunatekeleza dira ya miaka mitano na katika miaka mitano tumekuwa tukitoa hapo kila mwaka tunatoa kipande na tunatekeleza. Kwa sasa tuna Mpango wa Maendeleo wa Taifa wa 2018/2019, nichukue nafasi hii kupongeza sana, nimeona orodha ya miradi ya kimkakati. Niipongeze sana Serikali ya Awamu ya Tano kwamba, miradi hii kwa kweli, iko barabarani na iko sambamba kabisa na vision yetu ya 2025.

Mheshimiwa Mwenyekiti, duniani kokote kule na hasa kwenye nchi ambazo zimeendelea na zilizopata uhuru karibia na sisi Tanzania, nyingi sana zimepiga hatua na shabaha zao kufikiwa kwa sababu ya maamuzi ya dhati. Sisi hapa udhati wetu wa maamuzi, napata mashaka. Wakati standard gauge leo inajengwa wengine wanasema hiyo haina umuhimu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wakati tunajenga barabara na miundombinu inayounganisha, hapa tulikuwa hatuna barabara kwa mfano ya kutoka Iringa kupitia Dodoma kwenda mpaka Babati sasa tunaungana na Arusha; na hiyo nayo haina maana, lakini watu wanapita humo humo haina maana. Wakati wanafunzi wanalipiwa gharama kubwa sana na Serikali karibu kila mwezi shilingi bilioni 22 na ushee hilo nalo linaonekana halina maana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo, sidhani kama ni sahihi sana kwa sababu kama tutasema kila jambo tunabeza, kila jambo jema linabezwa, basi maana yake ni kwamba hatujui tunakokwenda.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, rai yangu Mheshimiwa Waziri Mkuu ni kwamba, hebu wakati mwingine tuzungumze kama Watanzania na pengine masuala haya ya dira yafundishwe hata kwenye shule za msingi, kwenye sekondari, kwenye vyuo vikuu yafundishwe kwa sababu hata ukimwambia Mtanzania hapa anayemaliza degree ya chuo kikuu kwamba hivi dira yetu sisi mpaka tunapofika mwaka 2025 tunataka tuwe tumefika wapi, unaposema suala la uchumi wa kati wengine hatuelewani, ama kwa makusudi, lakini nadhani iko haja ya kusisitiza watu kupata elimu hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nchi nyingi ambazo zimepiga hatua kwa shabaha zao walizoziweka hazikuwa legelege na kuwa na mawazo ambayo yanasigana kama sisi. Wakati jambo zuri ndege zinashuka hapa, ndege tatu zimefika tunasubiri hizo mbili zije, tayari wameanza kusema ndege ni za nini? Sasa unashindwa kuelewa hivi wanajua tunakokwenda? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, huwezi kujenga uchumi bila kuwa na national carrier, uchumi wa kisasa unajengwa kwa njia za usafirishaji. Kwa hiyo, nisihi sana kwamba, si ajabu hata humu Wabunge wengine wenzetu hawajui tunakwenda wapi na ndio maana wanavuta kamba tunakotaka kuelekea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nisihi kwamba kama tunataka kuwa Japan, kama tunataka kuwa kama China, ni lazima tuweke dira. Wenzetu Wachina juzi wameamua kuwa na Rais wao wa maisha. Uamuzi ule usifikiri ni wa kitoto ni uamuzi wa watu waliofikiri sana. Wameona kwamba Xi Jinping amekuja na ku-address kwa hotuba zake tatu tu. Ameeleza msingi wa vision yao wanayoitaka. Na sisi leo tunaye Magufuli ambaye anatupeleka kwa vitendo kwa kuangalia tunataka kuelekea wapi, lakini wako watu wanabeza. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Xi Jinping kwa hotuba tatu analibadilisha Taifa lenye watu wengi duniani la China, kumwamini kwamba anastahili kuwa Rais wa maisha, lakini sisi Magufuli anayetenda haya tunayoyaona makubwa tunasema hatuelewi anataka kutupeleka wapi. Kwa hiyo, niseme tu rai yangu, Mheshimiwa Waziri Mkuu nchi hii ni yetu wote ni Watanzania, lakini pale yanapofanyika mambo mazuri ni lazima wote tuunge mkono kama Watanzania tusikatishane tamaa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mnafanya kazi nzuri na kubwa sana, mnafanya kazi ya kujitolea kweli kweli lazima tuwapongeze. Mheshimiwa Waziri Mkuu nakupongeza wewe binafsi kwa kazi nzuri unayofanya. Imani yangu ni kwamba watanzania hawa ni vizuri sasa tukawaeleza tunayoona picha ya tunakokwenda.