Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Ofisi ya Waziri Mkuu

Hon. Dr. Haji Hussein Mponda

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Malinyi

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Ofisi ya Waziri Mkuu

MHE. DKT. HADJI H. MPONDA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kunipa nafasi kuchangia hotuba ya Waziri Mkuu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mojawapo ya malalamiko katika nchi hii ni mipaka na migogoro ambayo inaendelea katika vijiji vinavyopakana na hifadhi au mapori tengefu au mapori ya akiba. Naomba nianze kwa kumpongeza Waziri Mkuu kwa busara zake na kuwa msikivu zoezi hili katika bonde la Kilombero limekamilika Wilaya ya Malinyi na zoezi hili lilifanywa kwa kuwashirikisha wananchi. Pamoja na kukamilika zoezi hili yameacha kilio, imeacha kero, imeacha malalamiko kwa wananchi hawa. Naomba ieleweke zoezi hili limefanyika baada ya mabadiliko ya Sheria ya Wanyamapori ambayo yalifanyika mwaka 2009.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sheria hiyo ya wanyamapori kabla ya 2009 wananchi walikuwa wanaruhusu matumizi ya binadamu katika mapori tengefu likiwemo Bonde la Kilombero. Sasa ilivyobadilika sheria ile wananchi hawa kihalali kabasa vijiji karibuni 16 na vitongoji vyake kama 25 vinaishi kihalali kule katika maeneo yale. Sasa sheria imebadilika inawakataza, sasa hapo ndio umeanza mgogoro, lakini busara ambazo ametumia Waziri Mkuu ni kwamba ametuma wataalam, wajadili na wapitie mipaka ile.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lile zoezi limekamilika kama ninavyosema bado malalamiko yako pale kwa sababu pamoja imetambulika ile mipaka, lakini mashamba ya wananchi, wananchi wa Wilaya ya Malinyi na Wilaya ya Ulanga kilio chao kikubwa mashamba walikuwa wanalima maeneo yale hasa maeneo ya buffer zone sasa wamezuiliwa hawawezi kulima tena.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa nini maana yake? Kwa hiyo, kuwazuia kulima maeneo yale tayari tunatengeneza mazingira magumu na tujue kwamba mpunga ambao unapatikana Ifakara au mchele unaitwa Kilombero asilimia 80 ya mchele ule unatoka Malinyi. Sasa kitendo cha kuwazuia wananchi hawa wasilime maeneo yale tayari tumetengeneza mazingira ambayo ni njaa ambayo itatokana na kukataza kulima maeneo yale.

Nikuombe Mheshimiwa Waziri Mkuu ulimtuma Waziri wako wa Maliasili na Utalii amekuja maeneo yale, ameona na mimi namshukuru Waziri Dkt. Kiwangalla ametumia busara zake, ameona hali halisi ameunda tume ya watu 21 ambayo itafanya kazi ndani ya mwezi mmoja kuona nini changamoto wananchi wale ili kama mazingira yanaruhusu basi maeneo yale waruhusiwe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo letu lenyewe tunaliomba wala sio kubwa sana ni katikati ya kilometa mbili mpaka kilometa tano kutoka nje ya mipaka ya kijiji, vinginevyo kama atazuia wananchi wale basi kilio kitakuwa kikubwa sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili Serikali imeeleza hapa ukosefu wa pembejeo kuna changamoto mbalimbali zimesababisha na ukosefu huu. Naomba nielezee kwenye Wilaya ya Malinyi. Mwaka huu wananchi Wilaya ya Malinyi wameshindwa kulima mahindi kwa sababu ya sumu ya panya haikupatikana kwa wakati muafaka na taarifa tayari ilishatolewa kwa sababu tataizo hili limejitokeza miaka mitatu mfululizo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naiomba Serikali unapofikia wakati wa kuweka hizi bajeti waangalie msimu upi ambao unatakiwa kupeleka hizi pembejeo, vinginevyo kilio hiki kitaendelea. Kwa mfano, mwaka huu watu hawatalima mahindi kwa sababu ya hizo sumu za panya hazikufika kwa wakati muafaka. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, la mwisho Serikali mwaka 2010 waliingia mkataba wa mkopo na Serikali ya India wamekopa karibuni milioni 40 za Kimarekani toka Serikali ya India na mradi huo ulikuwa kuwezesha matrekta ya SUMA JKT, lakini mpaka ilivyofikia mwaka 2015 matrekta yale yalikuwa na matatizo ya urejeshaji wa mikopo ile na ndani ya miaka mitano ni asilimia 40 tu ya madeni 46 ndio yamerejeshwa. Sasa mwaka 2017 Serikali mmeanza mradi mwingine tena mradi mwingine wa kuunganisha matrekta pale Kibaha, matrekta aina ya…

(Hapa kengele ililia kuashiria kuisha muda wa Mzungumzaji)