Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Ofisi ya Waziri Mkuu

Hon. Omary Tebweta Mgumba

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Morogoro Kusini Mashariki

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Ofisi ya Waziri Mkuu

MHE. OMARY T. MGUMBA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana kwa kunipa nafasi ili nitoe mchango wangu katika hili. Niipongeze Serikali na Waziri Mkuu kwa hotuba yake nzuri ambayo ina mwelekeo mzuri wa bajeti yetu ya 2018/2019. Kwa sababu ya muda naomba niongelee jambo moja tu na mengine nitaongelea kwenye Wizara zinazofuata.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niipongeze sana Serikali ya Awamu ya Tano hasa Rais wetu Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli kwa uthubutu alioufanya ambapo Marais waliopita walikuwa hawajaufanya pamoja na kazi nzuri waliyoifanya kwa kutekeleza mradi wa Stiegler’s Gorge ambao unakwenda kutuhakikishia umeme wa uhakika zaidi ya megawatts 2,100 ndani ya muda mfupi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hili jambo siyo dogo, hili suala lilianza tangu miaka ya 60, Mwalimu Nyerere ilikuwa ni ndoto zake kulitekeleza, lakini kutokana na vikwazo mbalimbali wale wasioitakia mema Tanzania ndiyo waliokuwa wanaukwamisha mradi huu usitekelezeke. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mradi huu una manufaa makubwa sana. Pamoja na uzalishaji huo wa umeme megawatts 2,100 lakini pia utatoa ajira kwenye uvuvi. Hili bwawa litakuwa ni sehemu ya utalii, liko bwawa karibu na mbuga yetu ya Selou lakini pia kutakuwa na heka zaidi ya 85,000 ambazo zitakuwa ni za kilimo cha umwagiliaji. Utaona ni namna gani unaona huu mradi una fursa nyingi na faida kubwa ambayo inakwenda kutekelezwa na Serikali hii ya Awamu ya Tano. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia huu mradi utaboresha huduma za jamii. Nitoe mfano kwenye Jimbo langu la Morogoro Kusini Mashariki. Kupitia mradi huu, barabara ya Ubenazomozi – Ngerengere - Tununguo – Mvuha
- Kisaki - Stiegler’s Rufiji yote itatengenezwa kwa kiwango cha lami. Unataka mafanikio gani zaidi ya haya? Niipongeze sana Serikali kwa kuliona hili, lakini hasa Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli kwa kuthubutu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pengine watu hawaelewi miongoni mwa sababu ya kuanzishwa NEMC na mambo mengine haya ilikuwa ni kuzuia miradi kama hii ya Stiegler’s na Kidunda kwa sababu walikuwa wanaona ni miradi ya kielelezo, inakwenda kuwakomboa Watanzania kwenye njia ya umeme pamoja na maji, wakatuwekea vikwazo chungu nzima tusiitekeleze.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niliwahi kutoa mfano humu ndani Mradi wa Bwawa la Kidunda andiko lake la kwanza lilikuwa tangu mwaka 1955, andiko la pili 1962, andiko la tatu 1982 baada ya Wajapan kushinda ile tenda ya kutengeneza ule mradi ndiyo pale Wajerumani wakatuletea mradi huu wa mazingira, nani asiyejua? Leo tumepata Rais anakwenda kutekeleza yale bila kusikia lolote kwa maslahi ya Watanzania halafu tunaubeza. Niwaunge mkono, tuko nyuma yenu na kwa kusema haya naamini kabisa Serikali itapaa na Watanzania tutakwenda mbele zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kwa kusema haya niwaambie, haina maana Serikali imeachana na miradi ya gesi. Nawapa mfano mmoja, Rais tumemwona kama miezi miwili iliyopita alienda kuzindua Mradi wa Umeme Kinyerezi II zaidi ya megawatts 168. Huu ni mradi wa gesi inatumika ile ile ya Mtwara haijasimama.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kinachofanyika ni kuchanganya hii yote, mradi wa maji na mradi wa gesi ukizingatia umeme unaozalishwa kwa maji una gharama nafuu zaidi. Megawatts moja katika kuzalisha umeme wa gesi ni zaidi ya milioni 1.2 USD wakati mradi wa kuzalisha maji megawatts moja tunatumia zaidi ya milioni 1.0 USD maana yake ni nini? Huu mradi ambao ni wa kuzalisha kwa maji una gharama nafuu kuliko wa gesi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na hayo Serikali haijaacha. Niwaambie suala la gesi ni la utafiti unaendelea mpaka leo, tuna neema tumeshagundua futi za ujazo zaidi ya trilioni 57…

(Hapa kengele ililia kuashiria kuisha kwa muda wa Mzungumzaji)