Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Ofisi ya Waziri Mkuu

Hon. Augustino Manyanda Masele

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbogwe

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Ofisi ya Waziri Mkuu

MHE. AUGUSTINO M. MASELE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nami nachukua fursa hii kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunipatia nafasi ili kusudi na mimi niweze kuchangia hotuba hii ya bajeti ya Waziri Mkuu wetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa nipende tu kuwapa pole wananchi wangu wa Kata za Ngemo na Ushirika waliopata tatizo la kuharibikiwa nyumba zao kutokana na tetemeko lililotokea tarehe 25 Machi, 2018. Kwa maana hiyo, nipende tu kuishauri na kuiomba Serikali iendelee na utaratibu ule uliotajwa katika ukurasa wa 69 katika taarifa ya Mheshimiwa Waziri Mkuu inayohusiana na uratibu wa maafa, kwa maana ya kwamba mabadiliko ya tabianchi katika nchi yetu yamekuwa yakileta madhara kwa maana ya kwamba mpaka sasa tumejikuta mambo ambayo yalikuwa hayapatikani katika nchi yetu sasa yameanza kujitokeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaona tetemeko la ardhi lilitokea Kagera na sasa katika Wilaya ya Mbogwe tumepata tatizo hilo tarehe 25 usiku na kwa maana hiyo inaonesha kwamba huenda majanga kama haya yakaendelea kutokea. Kwa hiyo, naishauri Serikali iendelee kujiimarisha zaidi ili kwamba mambo haya yatakavyojitokeza katika kiwango ambacho siyo cha kawaida tuweze kukabiliana nayo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze mchango wangu sasa kwa kuanza kuipongeza kwanza Serikali inayoongozwa na Mheshimiwa Dkt. Pombe Joseph Magufuli akisaidiwa na Makamu wa Rais, Mheshimiwa Mama Suluhu Hassan pamoja na Waziri wetu Mkuu, Mheshimiwa Kassim Majaliwa. Serikali hii inafanya kazi nzuri, tuwe wakweli na tuache habari ya ushabiki. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kazi za Serikali hii ni zile ambazo zimekuwa zikipigiwa kelele ndani ya Bunge hili, tumeiomba sana Serikali ijenge reli kwa kiwango cha Standard Gauge, kazi hii imefanywa, upanuzi wa Bandari ya Dar es salaam Serikali inaendelea kufanya. Tumezungumzia habari ya Shirika la Ndege, watu wote humu tumekuwa tukipiga kelele, Serikali imesikia na ndege hizo imeanza kuzileta, lakini sasa naona tena watu wanaanza kugeuka kuwa vinyonga. Tunayoyazungumza humu yanapoanza kutekelezwa tunageuka tena tunaona kwamba Serikali haifanyi kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niishauri Serikali iendelee na mpango wake wa kuwaletea maendeleo Watanzania. Watanzania hawa wanapenda sana kuona kwamba nchi yao ambayo imejaliwa kuwa na rasilimali nyingi, ni nchi nzuri na ina kila kitu. Kilichokuwa kinakosekana ni namna gani ambavyo tumejipanga kuweza kuzitumia rasilimali tulizonazo hapa nchini kuweza kujikomboa kiuchumi na kuleta maendeleo kwa wananchi wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali yetu imekuwa ni Serikali sikivu, tunaona namna ambavyo Serikali inaendelea kusambaza umeme kila mahali. REA Awamu ya Tatu inaendelea vizuri, hata katika Wilaya ya Mbogwe kazi zinaendelea na wananchi wanaona kwa macho yao na siyo tu Mbogwe ni Tanzania nzima miradi hii inaendelea kufanyiwa kazi na watu wanaona. Wakati mwingine niseme tu kwamba watu wanaamua kufanya ushereheshaji, mtu anaiona kazi lakini anaamua kugeuza na kuanza kubeza. Niiombe Serikali iendelee mbele wala isigeuke nyuma. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika mwaka huu wa fedha niiombe Serikali kwa sababu ni Serikali yetu wote iendelee kuona utaratibu wa namna ya kuzisaidia Wilaya na…

(Hapa kengele ililia kuashiria kuisha kwa muda wa Mzungumzaji)