Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi kwa mwaka wa fedha 2016/2017.

Hon. Jerome Dismas Bwanausi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Lulindi

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi kwa mwaka wa fedha 2016/2017.

MHE. JEROME D. BWANAUSI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nichukue fursa hii kukushukuru kunipa nafasi na mimi ili ukayasikie tena mambo ya korosho.
Kwanza nianze kwa kumpongeza sana Mheshimiwa Waziri, lakini pia Naibu wake na Katibu Mkuu wa Wizara ya Kilimo na Watendaji wa Wizara kwa jinsi ambavyo mmejipanga kurudisha imani katika Wizara hii ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, tunatambua juhudi za Mheshimiwa Waziri Mwigulu ambazo anazifanya na wananchi wana imani kubwa sana kwa jinsi ambavyo ameonyesha njia na mipango thabiti ya kuhakikisha kwamba wakulima na wavuvi wanaanza kuneemeka kwa kupata kipato kizuri. (Kicheko/Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze na sakata la korosho Masasi. Mheshimiwa Waziri, mimi niendelee kukushukuru na ninamshukuru sana Mrajisi, namshukuru sana Katibu Mkuu wa Wizara, ndugu yangu Turuka kwa kuanza kulichukulia kwa umakini mkubwa suala la sakata la korosho katika Wilaya Masasi. Mheshimiwa Waziri, sakata hili ambalo wewe mwenyewe umeahidi kwenda kulisikiliza kule, takriban zaidi ya shilingi bilioni tatu, wakulima wale hawajuwi watazipata lini. Mchezo huu wa kuwadhalilisha wakulima na kuwanyima haki zao haujaanza leo. Ni wa miaka mingi, lakini mwaka huu Mheshimiwa Waziri wamekufuru kuchukuwa hizo fedha. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, naamini kwa umakini wa Serikali ya Awamu hii ya Tano, inayoongozwa na Rais Dkt. John Pombe Magufuli, ambaye amesema Serikali hii ni ya kuwajali wanyonge na watu ambao wako kule chini, ninao uhakika kabisa kwamba Serikali itaingilia kati suala hili na kuhakikisha wakulima wale wote ambao wanaelekea kudhulumiwa wanalipwa stahili zao inavyostahili! (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, tumelipokea sana kwa shangwe kubwa tamko la Waziri Mkuu juu ya kupunguza zile tozo, lakini nataka kutoa angalizo, wananchi wamefurahi sana kuona jinsi ambavyo korosho sasa zitaweza kuuzwa kwenye maghala yao. Kama hatukujipanga vizuri kuhakikisha bodi inaweka watalaam wa korosho kule katika kila ghala kuangalia ubora wa korosho kwa kuziweka katika grade zinazostahili na kuhakikisha zinawekwa vizuri, tutajikuta baadaye tunakwama katika suala zima la soko la korosho. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, ni imani yangu katika miezi hii michache iliyobaki, Bodi ya Korosho kwa kushirikiana na Mfuko, lakini pia kwa kushirikiana na Wizara, ijipange vizuri. Umebaki muda mfupi, tujipange vizuri ili azma ya Serikali ya kumfanya mkulima wa korosho apate bei nzuri mwaka huu iweze kutimia. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda sana Wizara hii ijielekeze sana katika kuhakikisha kwamba Mfuko wa Wakulima wa Korosho unajielekeza kutumia zaidi kwa ajili ya shughuli za maendeleo ya korosho kuliko matumizi ya kawaida. Ingewezekana kabisa, bodi kwa kushirikiana na Mfuko ikaongeza fedha kwenye ruzuku ya mbolea na kuwafanya wakulima wengi zaidi wapate punguzo la bei ya pembejeo kuliko ilivyo sasa. Na mimi naomba sana Mfuko wa Wakulima wa Korosho ni lazima ufanye kazi yake kwa uwazi zaidi kuliko ilivyo sasa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, fedha zinazotolewa kupelekwa kwenye Mfuko wa Wakulima wa Korosho ambayo inatokana na export levy ni fedha nyingi sana, lakini sijuwi kama Serikali inaziangaliaje fedha zile tunazozipeleka kule kwa maana ya kuzikagua, lakini kuhakikisha kwamba matumizi yasiyo ya lazima yanaepukwa ili ule Mfuko ufanye kazi yake ipasavyo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nielekee kwenye suala zima la kilimo katika Bonde la Mto Ruvuma. Kama kuna maji ambayo hatuyatumii mpaka yanaelekea baharini ni maji ya Mto Ruvuma. Yale maji tungeweza kuyatumia kwa kilimo kwa kushirikiana na Wizara ya Maji na Umwagiliaji ili bonde lile litumike kwa ajili ya uzalishaji wa mazao ya chakula, lakini yale maji yote yanatiririka kwenye bahari na wala hatuna mpango wala scheme kubwa ya kuhakikisha kwamba maji yale tunayatumia. Naomba sana Mheshimiwa Waziri katika mipango yako hebu tujaribu kuangalia uwezekano huo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nizungumzie kuhusu Maafisa Ugani. Katika kipindi changu cha siasa nimefanya kazi kwenye ngazi za chini, kuanzia chini kabisa; Mwenyekiti wa Mtaa, Diwani, Meya hadi sasa. Nilichobaini ni kwamba Maafisa Ugani wengi tunawalipa mishahara bila kufanya kazi. Ni lazima wale Maafisa Ugani tunaowapeleka kwenye Kata, Maafisa Kilimo na Maafisa Mifugo, waonyeshe mpango wa kazi. Unamkuta wakati mwingine baadhi ya maeneo, siku Mheshimiwa Mbunge unakwenda ndiyo na yeye anajitambulisha mbele ya wananchi. Wananchi hawamjui! (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, ni lazima Wizara isimamie kuhakikisha wale Maafisa Ugani kule chini kwa kweli wanafanya kazi, lakini kuwe na utarabu hata wa kwenda kuwakagua shughuli gani ambazo wanazifanya za kila siku katika maeneo yao. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hakika wananchi wangependa sana kuendelea na mfumo huu ambao hivi sasa upo wa pembejeo za ruzuku. Naiomba Wizara, kama haijajipanga vizuri, utaratibu huu wa kusambaza pembejeo za kilimo kwa maana ya ruzuku usitishwe mpaka mtakapojipanga vizuri! Hakuna sababu Serikali inapeleka fedha kwa ajili ya kuwapa wachache wanaoweza kutumia zile fedha kwa njia za udanganyifu! Hakuna sababu! (Makifi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, mawakala wengi sio waaminifu hata kidogo! Wenyewe wanashirikiana na baadhi ya wachache ambao sio waaminifu katika vijiji kusaini kwamba wamepokea mbegu pamoja, ambapo hawakufanya hivyo, yaani hawapokei! Wanakwenda kuziuza tena zile pembejeo! (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, narudia. Wizara ya Kilimo kama haijajipanga vizuri kwa muda huu mfupi kabla ya msimu ujao wa kilimo, iache, isubiri mwakani ikijipanga vizuri! (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri aliahidi kuja Masasi. Naomba katika mahitimisho yake atuthibitishie Wanamasasi kwamba lini tunakwenda ili kukutana na wananchi wale ili tuwaondelee matatizo waliyonayo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, naomba kuunga mkono hoja. Ahsante sana!