Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Ofisi ya Waziri Mkuu

Hon. Justin Joseph Monko

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Singida Kaskazini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Ofisi ya Waziri Mkuu

MHE. JUSTIN J. MONKO: Mheshimiwa mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa na mimi nafasi ya kuweza kuchangia Hotuba ya Mheshimiwa Waziri Mkuu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza niipongeze Serikali ya Awamu ya Tano kwa namna inavyoshughulika na masuala ya wananchi kupitia bajeti zake na kupitia watendaji wake wote kwa ujumla. Kwa sababu ya muda wangu mfupi nitajaribu tu kueleza niliyoyaona katika bajeti hiyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze na suala la kilimo; bado kuna tatizo kubwa kwamba tuna uwekezaji mdogo saa wa kilimo. Tunayo maeneo makubwa, mazuri ambayo yanafaa kwa kilimo, tunayo mabonde mazuri ambayo yanafaa katika kilimo cha umwagiliaji, lakini tunachokifanya sasa hivi ni kufanya umwagiliaji kwenye bahari, kumwagilia maji kweye mito, lakini kilimo cha umwagiliaji bado hakijawa na tija katika nchi yetu.

Kwa hiyo, niiombe sana Serikali ijaribu kuwekeza hatuwezi kwenda kwenye hatua ya viwanda ambayo tunazungumza na tumesisitiza kwamba viwanda vyenyewe lazima viwe ni viwanda ambavyo vitatokana na malighafi za ndani. Malighafi hizo ni za kilimo na tumekuwa na uwekezaji mdogo sna katika sekta ya kilimo.

Katika masuala ya elimu, katika hotuba ya Waziri Mkuu tumeona katika masuala ya elimu kwa kweli udahili wa wanafunzi umeongezeka kwa asilimia zaidi ya 35, lakini miundombinu yetu katika shule za msingi hata katika sekondari kwa kweli ina changamoto kubwa. Zipo shule nyingi katika Jimbo langu zina matatizo. Iko shule moja ya Mikuyu ina madarasa mawili, ina choo ambacho ni cha muda, lakini ina darasa kuanzia chekechea mpaka darasa la sita na haina hata ofisi ya walimu, lakini shule hii imesajiliwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini iko shule nyingine ambayo iko Mighanji katika Kata ya Ngimu. Shule hii ina wanafunzi wengi, wako wanafunzi wanasoma wanatoka zaidi ya kilometa 11 kwenda kwenye hiyo shule. Wananchi wa vitongoji vya Ngaramtoni wamejitolea kujenga shule lakini bado haijapata usajili. Wanayo madarasa manne lakini sasa hivi imeshindwa kusajiliwa kwa sababu haina lipu, haina sakafu na bado tumeacha watoto wetu wale wadogo wanaendelea kutembea kwa zaidi ya kilometa 10.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tatizo hili ni kubwa ukichanganya na tatizo la upungufu wa walimu, kwa kweli limeleta shida sasa katika Jimbo langu na ndiyo mtaona hata matokeo yaliyopita kwa kweli Jimbo letu limefanya vibaya sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie pia shule za sekondari. Tunayo matatizo ya maabara, maabara nyingi katika Jimbo langu hazijakamilika na nilipotembelea katika Jimbo lile nimeona nyingi zinahitaji fedha karibu shilingi milioni 90 kumalizia. Ni nyingi na suala hili sasa hivi katika bajeti ya Halmashauri yenye makusanyo ya ndani ya shilingi bilioni 1.3 haiwezi kufanya jambo lolote. Kwa hiyo, niiombe sana Serikali ifanye mkakati wa makusudi katika kuhakikisha kwamba inasaidia kumalizia ujenzi wa hizi maabara zetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini niangalie katika suala la afya. Suaa la afya katika Jimbo langi la Singida Kaskazini poa ni tatizo kubwa. Nina vijiji 84 lakini tuna zahanati 32 tu. Vituo vya afya vilivyopo ni viwili, Kituo cha Mgori na Kituo cha Ilongero. Vituo hivi havitoi huduma ya upasuaji. Kwa bahati mbaya sana vituo vyote viwili havijapata fedha za ukarabati kama ambavyo katika halmashauri nyingine zimepata.

Kwa hiyo, niiombe sana Serikali ifanye haraka kwa sababu Halmashauri hii haina hata hospitali ya wilaya tunategemea Hospitali ya Mtinko ambayo ni hospitali ya mission na wananchi wanapata matatizo sana katika masuala ya matibabu. Viko vijiji vinafuata matibabu kwa zaidi ya kilometa 40. Kiko Kijiji cha Mkulu ambacho makao makuu yake ya kijiji ni kilometa 26. Viko vitongoji vitatu ambavyo viko Mkulu, lakini kijiji chenyewe ni cha Nduamuhanga kiko kilometa 26; na huko ndiko ili zahanati.

Ukitoka hapo ni lazima ukatize kwenye pori, kwenye hifadhi au upite katika Wilaya ya Chemba. Tunahitaji kwa kweli kupata msaada kwa sababu wananchi wale wanahitaji kupata msaada wa haraka ili kusudi waweze kuepukana na matatizo na kuokoa maisha ya wananchi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nije katika suala la barabara. Jimbo la Singida Kaskazini lina mtandao wa barabara wa kilometa 772.39...

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. JUSTIN J. MONKO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante, lakini kinachosikitisha barabara hizo zimejengwa kwa kiwango cha changarawe kwa asilimia 8 tu, yaani kilometa 68 kati ya hizo 774.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niiombe sana Serikali iweze kutenga fedha katika bajeti hii inayokuja kuhakikisha kwamba Jimbo hili linasaidiwa. Hatuwezi kuendelea kuwa na barabara za udongo kwa zaidi ya asilimia 91 katika karne hii. Ahsante sana, naunga mkono hoja.