Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Ofisi ya Waziri Mkuu

Hon. Rukia Ahmed Kassim

Sex

Female

Party

CUF

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Ofisi ya Waziri Mkuu

MHE. RUKIA AHMED KASSIM: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante na mimi kuweza kunipa nafasi hii ili niweze kuchangia katika hotuba hii ya Mheshimiwa Waziri Mkuu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi naanza na ukurasa wa 12; Serikali kuhamia Dodoma. Hili ni jambo jema sana Mheshimiwa Rais kuamua kama sasa kweli Serikali ihamie Dodoma, lakini nahisi bado Manispaa ya Dodoma haijajielewa kama Rais katoa amri hii kuwa Serikali ihamie Dodoma. Hivi ninavyosimama hapa hakuna stand ya magari, mabasi yanahangaikahangaika tu, wameondolewa hapo wamepelekwa Kilimo Kwanza, huko Kilimo Kwanza ni eneo la Jeshi ambalo wameliazima.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hivi kama kweli Serikali imeamua kuhamia Dodoma wao bado hawajaliona hili na wakaanza kutayarisha kuwa hili ni eneo la ku-park na basi na eneo lingine waweke kwa ajili ya magari madogo madogo? Hiace zinarandaranda tu hapo barabarani, lakini hawana parking za kukaa wala za kuweza kuchukua abiria. Hili ni tatizo, kwa hiyo naiomba Serikali waieleze Manispaa na wajielewe kwamba Serikali sasa imehamia Dodoma. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia kuna viukuta hivi vya road reserve, hivi vimekuja mpaka kufikia nadhani Kilimo Kwanza, hapa katika mji havipo, lakini kuna viwanja ambavyo bado ni vitupu na wenyewe watajenga, kwa hiyo kama hawakuviweka mapema watu wakijenga wataingia katika eneo la road reserve baadae itabidi kuvunjwe. Kwa hiyo, mimi nawashauri wajipange na wajielewe na waweze kuweka vitu kama hivyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna mitaro ya majitaka; bado haijarekebishwa vizuri. Tunayaona maji yanasambaasambaa hovyo tu. Tatizo hili limejitokeza Dar es Salaam, Dar es Salaam wakati mji ule ulikuwa na watu wachache mitaro ya majitaka ilikuwa inakidhi haja kwa idadi ya watu waliokuwepo kwa wakati ule, lakini hivi sasa kama hawakuwaza kuliweka mapema na wakajua kwamba huu utakuwa ni mji wakaanza kutayarisha mitaro hiyo ili ikidhi haja ya watu watakapokuwa wengi, italeta shida. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna eneo hili la mji hapo ambapo kuna vichochoro vile, kuna barabara za mitaa, zile barabara ni nyembamba mno utafikiria ulimi wa paka, hawajarekebisha, watu wanavunja majumba ya zamani wanajenga, lakini bado hawajaweka ile mitaa iongezeke, yaani walau gari ziweze kipishana. Kwa hiyo, mimi naishauri Serikali, mtu yeyote ambaye atajenga sasa katika eneo la mji kwanza ianze sheria kuwa ajenge ghorofa na waache nafasi ambayo itasaidia magari yaweze kupishana katika ile mitaa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, uwanja wa ndege, uwanja uliopo hapa ni aibu, ule si uwanja, sijui hata ni kitu gani, useme ni uwanja wa volleyball au sijui useme kitu gani. Serikali imepanga kujenga uwanja Msalato, kwa hiyo, mimi naishauri Serikali waanze kujenga ule uwanja Msalato ili aibu hii iondoke. Wakianza kujenga uwanja kwa sababu sasa hivi mji umeanza kukua kuna Mabalozi wamehamia hapa, kuna maafisa chungu nzima wa Serikali wako hapa, sisi Wabunge tuko hapa, lakini uwanja uliopo ni mdogo, ndege kubwa haziwezi kutua, kwa hiyo hii ni aibu. Mimi naishauri Serikali waanze kujenga uwanja wa Msalato ili tatizo hili liondoke.

Mheshimiwa Mwenyekiti, watu wa manispaa tunawaomba, sisi watu tunaokaa Area D, Area D sasa hivi imekuwa ni kisiwa. Ukitaka kwenda Area D mpaka uzunguke Mji wote wa Dodoma ndiyo uweze kufika. Kwa hiyo, mimi nawasauri angalau mle kandokando ya ule uwanja watutengenezee japo kijinjia kidogo magari yaweze kupita, wanaokwenda Area D isiwe kama ni watu wanaokwenda katika mji mwingine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kutoka hapo najielekeza sasa katika vyama vya siasa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimemsikia Mheshimiwa Mohamed Mchengerwa, Mwenyekiti wa Kamati ya Katiba na Sheria akimshauri Msajili wa Vyama vya Siasa vyama ambavyo vinakiuka maadili na Sheria ya Vyama vya Siasa vifutwe. Jambo hili si jema na ninaomba lisije likatokea katika nchi yetu, kwa sababu unapokifutia chama usajili ni kuwafanya wale walio na chama sasa,kwa sababu chama kile sio cha viongozi, chama ni cha wananchi wote; unapounda chama hata mkiwa ni wachache mmeunda kile chama lakini ni sawa na kujenga msikiti au kanisa, utalijenga baadae likikamilika muumini yeyote anayekwenda kusali pale tayari ana haki. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo hivi vyama vya siasa sio vya viongozi, ni vyama vya wananchi, vitakapofutwa itabidi wale wanaofanya siasa sasa watakapokosa pa kufanyia watakwenda kufanya katika misikiti, kwenye nyumba za ibada, makanisa, hii itakuwa ni shida kubwa na italeta tatizo kubwa katika nchi. Mimi namshauri Msajili kama ni mlezi wa vyama chama kinapotokea matatizo awaite na awashauri na si kuwafutia usajili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nimemsikia Mheshimiwa Mchengerwa akisema katika hotuba ya Kamati yake kumshauri Msajili wa Vyama vya Siasa aendelee kutatua matatizo kusaidia kusuluhisha tatizo lililopo katika Chama cha Wananchi (CUF). Mimi ni Mbunge kupitia CUF, nakiri kweli kuna matatizo katika Chama cha Wananchi (CUF) ambayo yamesababisha hata sisi wenyewe humu ndani hatuelewani, ni bora mtu wa chama kingine unamuona ni mwema zaidi kwako kuliko yule wa chama chako, hili ni tatizo. Na tunamuomba Msajili aendelee kutushauri na kutupatanisha kwa sababu mwisho wa yote haya ni matatizo kwetu. (Makofi)

T A A R I F A . . .

MHE. RUKIA AHMED KASSIM: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza mimi hayo maneno yake ya kisimani siyataki, nataka aongee maneno ya Kibunge. Msajili ana haki, Msajili ndiye mlezi wa vyama kwa mujibu wa sheria na Katiba ya nchi hii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna Sheria Na. 5 ya mwaka 1992, Sheria ya Vyama vya Siasa, inampa mamlaka Msajili kuvishauri na pia kushughulikia vyama vya siasa. Kwa hiyo yeye ikiwa anasema Msajili kashtakiwa, kashtakiwa na nani na kwa sheria gani? Mimi nadhani hayo maneno ya kisimani akayasemee Kilwa, si humu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niendelee. Atakapoweza kutatua tatizo hili litatusaidia lakini inaonekana kuna baadhi ya watu hawataki, lakini mimi naona tu hawajajijua kwa sababu kama wanajijua, Profesa ndiye Mwenyekiti wa Chama cha Wananchi (CUF) na ndiye mwenye mamlaka ya kuweza kuteua na ku… (Makofi)

T A A R I F A . . .

MHE. RUKIA AHMED KASSIM: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo mimi nasema huyo ni comedy katika siasa. Na ninamuomba u-comedy wake akaufanyie kule Konde, si katika Bunge. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Profesa ni Mwenyekiti kwa mujibu wa Katiba ya Chama cha Wananchi (CUF). Kama wao wanasema kwamba Profesa alijiuzulu anapojiuzulu Mwenyekiti au Katibu Mkuu au Makamu Mwenyekiti kwa mujibu wa Katiba ya CUF mpaka mamlaka iliyomchagua ikubali, iridhie kujiuzulu kwake, kikao hicho hakikufanyika na Profesa alirudia nafasi yake kama Mwenyekiti.

Mheshimiwa Mwneyekiti, kwa hiyo, namuomba kama ni Mbunge kupitia Chama cha Wananchi (CUF) amheshimu na ajue kwamba ni Mwenyekiti wake, na akiendelea na huo utumbo kuna Kamati imeundwa ambayo ni ya maadili ambayo mimi ni mjumbe wake, tutamshughulikia.