Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Ofisi ya Waziri Mkuu

Hon. Oran Manase Njeza

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbeya Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Ofisi ya Waziri Mkuu

MHE. ORAN M. NJEZA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa hii nafasi na mimi naomba nianze kwanza kwa kumpongeza Mheshimiwa Rais kwa kazi kubwa anayoifanya hasa kwenye miundombinu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mtizamo tu wa kawaida ujenzi wa reli ya kati watu wanaweza kufikiri ni kitu kidogo sana kwa Standard Gauge au ujenzi wa viwanja vya ndege na ununuzi wa ndege. Hiki ni kitu kikubwa kwa heshima ya nchi yetu na kwa kweli inatu-position mahali pazuri sana na branding yake kwa nchi yetu nafikiri inatuweka mahali pazuri sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nimshukuru Waziri Mkuu kwa kazi kubwa anayoifanya pamoja na timu yake. Amefanya kazi nzuri sana na anaendelea kufanya kazi nzuri sana na amefanya ziara Mbeya. Alipofanya ziara Mbeya pamoja na mambo mengine alitembelea kuna meli tatu zimejengwa pale kwenye Ziwa Nyasa. Aliona ni namna gani Watanzania wana uwezo mkubwa, meli mbili zimekamilika na zimeshaanza kazi na zimejengwa na Watanzania. Kwa kweli, namshukuru sana Mheshimiwa Waziri Mkuu ulichokifanya siku ile ni kitu kikubwa sana na kimeleta hata impact kwa majirani zetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile naomba niwapongeze Mawaziri wote, wamejitahidi wamefanya ziara kwenye majimbo yetu na ziara zake matokeo yake ni mazuri sana. Wote walipokuja kwenye Jimbo langu wameacha matokeo mazuri sana. Sasa naomba nianzie kwenye
miundombinu ambayo ndiyo Serikali yetu imejikita kwa kiasi kikubwa sasa hivi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ujenzi wa reli ya kati wa Standard Gauge ni kitu kimekuja kwa wakati muafaka, pia na uboreshaji wa bandari umekuja kwa wakati muafaka. Kwa sababu hivi vyote vinaifanya Tanzania iwe ni njia kuu kwa ajili ya kibiashara kwenda kwenye masoko ya kidunia. Napendekeza pamoja na ujenzi wa reli na uboreshaji wa reli ya kati, ningeomba vilevile Serikali ije na mkakati ni namna gani itaifufua TAZARA.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nalisema hilo kwa maksudi kabisa nilikuwa naangalia wenzetu majirani wanafanya nini leo hii. Nilikuwa naiangalia Msumbiji inafanya nini. Msumbiji ilikuwa katika dimbwi la vita. Usalama ulikuwa mdogo sana. Kwa hiyo, nchi jirani hazikutegemea sana zile bandari zake. Leo hii Msumbiji wanaboresha reli na bandari inaitwa Nakala. Hiyo Nakala ambayo itakuwa ni kati ya bandari kubwa katika ukanda wetu huu wa Indian Ocean itapitia katikati ya Malawi na vilevile inaenda kwenye Jimbo linaitwa Tete ambalo jimbo la Tete ni ndani ya Msumbiji hiyo na ni jirani sana na Zambia na ni jirani sana na Zimbabwe.

Sasa sisi kwa biashara yetu ya bandari ambayo kwa kiasi kikubwa nina imani zaidi ya asilimia 75 kwa ajili ya soko la nje inategemea sana sana border post yetu ya Tunduma, kwa ajili ya Zambia, Malawi, Congo na kwa kiasi kidogo Zimbabwe. Sasa hawa wenzetu hili soko tayari wameshaliangalia na wameshaanza ujenzi kuna project pale ya dola bilioni tano ambayo katika hizo bilioni 300 zinatoka ADB (African Development Bank), sasa ikikamilika hiyo je, sisi biashara yetu ya bandari kwa ajili ya nchi hizi za Zimbabwe, Zambia, Malawi na Congo itaathirika namna gani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilikuwa naiomba Serikali iweke mkakati wa kuiboresha TAZARA. Kuna umuhimu sana wa kuiboresha TAZARA, kama bandari ina asilimia 75 inazitegemea hizi nchi ambazo leo hii nchi zote hizi zinaangaliwa na wenzetu wa Afrika Kusini, Angola na sasa
hivi Msumbiji tutakuwa tumejiweka wapi kwenye soko la usafirishaji. Kwa hiyo, naomba Wizara itakapokuja Wizara husika, ijaribu kuangalia ni namna gani itaboresha TAZARA lakini vilevile ni namna gani tujenge bandari kavu Mbeya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hiyo bandari kavu kwa sababu kuna kilomita pale 120 za kwenda ziwa Nyasa, nazo tuangalie kwa ajili ya ushindani ili reli ile itoke Mbeya kwenda ziwa Nyasa kwa ajili ya ushindani ambao wameuonyesha hawa wenzetu wa Msumbiji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia kwenye viwanja vya ndege, kuna Wabunge wengi wameongelea uwekezaji na ujenzi wa uwanja wa ndege wa Songwe. Ni kweli ni miaka mingi bajeti zimekuwa zikitengwa lakini mpaka leo uwanja hauna taa za kuongozea ndege, uwanja hauna uzio.

Mheshimiwa Mwenekiti, leo hii bidhaa kama maua, bidhaa kama viazi, bidhaa mbalimbali za matunda zinatoka Mbeya kupelekwa kiwanja cha ndege cha Dar es Salaam kwa sababu hatuna taa kwenye uwanja wa ndege wa Songwe. Naiomba Serikali itoe hizo hela haraka kwa sababu kwa kiasi kikubwa kwanza ukiangalia hata abiria wengi wanatoka nchi zetu hizi za jirani. Tunapata pesa nyingi za kigeni, lakini vilevile tuna-potential ya ku-export vitu vingi kwa kutumia..., ndege kubwa zinahitaji kutua moja kwa moja kwenye uwanja ule, huwezi ukatumia ndege kubwa ukasema itue kwanza Dar es Salaam ndiyo ije Mbeya. Wenyewe wanataka wakichukua mzigo aende moja kwa moja New York au aende moja kwa moja Russia.

Kwa hiyo, tunaomba ule ukamilishaji wa ule ujenzi na kwa vile ilishatoka kwenye bajeti sioni kama kuna tatizo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine ni la uzio, ni muhimu sana kujenga uzio kwa ajili ya usalama. Tumeona kiwanja cha ndege cha Mwanza juzi hapa binadamu amehatarisha abiria na ndege na hilo linaweza kuja kutokea kwenye kiwanja cha Songwe kwa vile pembezoni mle watu
wanafuga ng’ombe, ng’ombe wana tabia ya kufukuzana. Sasa fikiria ng’ombe wanafukuzana halafu ndege ndiyo inatua, sijui hiyo hatari nani ataibeba.

Naomba sana Wizara itakapokuja hapa iseme ni namna gani katika hivi viwanja ambavyo ni potential. Potential kwanza ni vya mpakani, lakini vilevile ni soko kubwa pia ni viwanja vikubwa tuvimalizie ili biashara na tuweze kupata bei nzuri, tuweze kupata pesa nyingi za kigeni. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, la mwisho ni suala la kilimo. Suala la kilimo kila mmoja kaongea kabisa uchumi wetu kwa kiasi kikubwa unategemea kilimo na kweli haipingiki. Lakini nilikuwa najaribu kusoma makala mbalimbali ambazo zinaonyesha ni namna gani kuna hatari ya upungufu mkubwa wa chakula mwaka 2030 mpaka 2050. Tanzania tumejiandaa vipi kwa hilo. Wenzetu ukisoma wamejiandaa sana, wana- invest sana ili waweze kukabiliana na hii hali na hiyo sisi tunaiweza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunapoongelea kuhusu maji ni namna gani maji yatusaidie kwenye umwagiliaji, ni namna gani maji ya mvua tuweze kuyavuna, bila hivyo mwaka 2030 target ya wenzetu kwa kweli itatumaliza na Tanzania kwenye ongezeko la watu inaonekana speed yetu ni kubwa, tunaongezeka kwa haraka, lakini uzalishaji wa chakula ni mdogo sana. Kwa hiyo, naiomba Wizara ije na mkakati ni namna gani imejipanga kuhakikisha kuwa mazao ya chakula hayaitwi tu mazao ya chakula, nayo yawe katika orodha ya mazao ya biashara. Hii ya kusema kuna kahawa, cocoa, korosho ndio mazao ya bishara nafikiri ni mfumo wa kizamani, kwa sababu ni mazao ambayo tulikuwa tunategemea fedha za kigeni. Lakini kibiashara leo viazi, mahindi, maharage kwa kiasi kikubwa nafaka ndiyo wakulima wanategemea kwa kiasi kikubwa kama mazao ya biashara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na hilo nafikiri tusije tukafanya makosa ya kuzuia haya mazao tena kuuzwa nchi za nje. Leo hii Kenya mahindi kwa kiasi kikubwa wananunua kutoka Uganda. Sasa ukiangalia Uganda wanazalisha mahindi? Mahindi yanayozalishwa Uganda ni tani kama milioni mbili na laki nane tu, lakini Tanzania tunazalisha karibu tani milioni sita.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana, naunga mkono hoja.