Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Ofisi ya Waziri Mkuu

Hon. Peter Ambrose Lijualikali

Sex

Male

Party

CHADEMA

Constituent

Kilombero

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Ofisi ya Waziri Mkuu

MHE. PETER A. LIJUALIKALI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa nafasi. Awali ya yote, nitoe pole kwa familia ya Diwani, Marehemu Godfrey Luena ambaye aliuawa kwa kupigwa mapanga nyumbani kwake. Natoa pole lakini nataka niiambie familia yake kwamba Luena hajafa, Luena anaishi. Kile ambacho alikiamini kitaishi, ambacho alikipigania kitaishi hakitafika kwake Kilombero. Tunamheshimu Luena kwa kazi aliyoifanya na tunaamini kazi yake haitapotea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa bahati mbaya sana hekima ya upinzani wa nchi hii ni upumbavu kwa Serikali ya CCM. Kwa bahati mbaya sana, hekima yetu ni upumbavu; hekima yetu ni tafsiri kwamba ni waoga. Ni bahati mbaya, lakini hekima yetu haitalala, itafanya kazi siku zote ingawa inaonekana ni upumbavu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo katika Taifa letu kuna jambo ambalo kwa kweli linaniuma sana. Nichukue mfano tu, watu wana-post kwenye mitandao kwamba Mheshimiwa fulani anaumwa au anakaribia hivi, watu wanasema bora aende, bora afe, tumechoka. Kama sisi ni watu wazima wenye akili timamu, wenye upendo wa Taifa letu, unapokuwa na Taifa ambalo kiongozi mkubwa wa Taifa anaumwa halafu wananchi wanasema bora afe; hii inatoa tafsiri mbaya kwa Taifa. Taswira ya nchi yetu inaharibika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaposema haya maneno kwamba kuna shida, huu ni upumbavu. Tunaposema kuna uonevu katika nchi hii, kwa sababu tumesema, tunaonekana sisi ni waoga.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hakuna mtu ambaye hajui hapa, Bunge lililopita Mheshimiwa Nape na wenzake walisema usalama wa nchi ni mbovu, Kamati ya Bunge iundwe, ile Kamati ikafanya kazi kubwa, ikaenda huko, mpaka leo majibu hakuna. Kwa nini hamna majibu? Hekima hii ni upumbavu kwenu. Mnadhani kuwa mambo ni mazuri?

KUHUSU UTARATIBU . . .

MHE. PETER A. LIJUALIKALI: Mheshimiwa Mwenyekiti, mama yangu, nimwambie kwamba lengo langu haikuwa kumuudhi mtu yeyote kati yenu, ama yeyote aliyepo humu ndani, siyo lengo langu. Nami sijafundishwa kumuudhi mtu yeyote. Nimejaribu kutumia labda neno ambalo naweza nikaeleweka, ila kama limekuudhi, nisamehe. Naamini kwamba umenielewa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, haiwezekani watu wazima tumekaa wote hapa, tunaona kabisa viashiria vya nchi kuharibika, tunajifanya hatuoni. Ninyi ndio wazee wetu. Tulitegemea muwe wa kwanza kuona haya mambo kwamba yanaharibika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano, tunahubiri mshikamano, umoja na upendo; na mwenzangu Mheshimiwa Mwakyembe alikuja kwenye Kamati, akasema sasa hivi tuna mpango tulete sijui kampeni ya uzalendo kwanza. Unawezaje kuwa na uzalendo kwenye Taifa ambalo Diwani wangu anauawa, kiongozi wangu wa chama anafanyiwa uhuni, mpaka leo kimya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, utaona mfano, haya magazeti, jambo hilo hilo likiandikwa kwa ajili ya Mheshimiwa Mbowe kwa maneno hayo hayo, Serikali inakaa kimya; Mheshimiwa Waziri anaona raha, anatulia. Jambo hilo hilo, neno hilo hilo likiandikwa kwa kiongozi wa Serikali, gazeti linafungiwa. Huu umoja unatoka wapi? Huu upendo mnaotaka kuhubiri unatoka wapi? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nchi yetu jambo baya; hata hii sheria wanayosema ya mtandaoni, watu wote ambao wamekamatwa nayo ni watu ambao wanaaminika wanaongea jambo ama wame-post kitu ambacho kinakwenda kinyume na Serikali, lakini jambo hilo hilo mtu wa CCM aki-post, husikii shida yoyote. Sasa tutajidanganya hapa; amani, amani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sikia niwaambieni, nchi zozote zile ambazo mambo yameharibika, haikuanza tu siku mambo yakaharibika, mambo yanaanza hivi. Wazee mpo hapa mnaona mambo yanaharibika kwa sababu mnadhani mtakuwapo milele, mnaacha mambo yaende. Mtaharibu nchi yetu ninyi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mengi yamesemwa. Niongelee sasa kuhusu elimu. Taifa lolote lazima likitaka maendeleo liwekeze kwa watu. Investment ya nchi ya kwanza ni kwenye aina ya watu inayotengeneza Taifa. Hii nitasema siyo kwamba nafurahia, Taifa ambalo tunazindua ndege watu wanakwenda kukimbilia kupanda eti kupiga picha. Come on! Hii nchi gani? Yaani Watanzania tumekuwa, yaani, khaa! Haya bwana. (Kicheko)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia bajeti, asilimia 70 ya fedha ambazo zimeingia kwenye elimu ni fedha za wafadhili. Fedha zetu za walipa kodi hazijaingia kwenye elimu. Maana yake ni kwamba Taifa letu halijawekeza kwenye elimu. Kama Taifa haliwekezi kwenye elimu, tunawekeza kwenye Bombadier na vitu vingine, its okay. Tutakuwa na Bombadier, tutakuwa na standard gauge, vitu vizuri vizuri vitakuwa vinaonekana, lakini vina-bring impact gani kwa watu wetu?