Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Ofisi ya Waziri Mkuu

Hon. Dr. Jasson Samson Rweikiza

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Bukoba Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

3

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Ofisi ya Waziri Mkuu

MHE. JASSON S. RWEIKIZA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kunipa nafasi kuchangia asubuhi ya leo. Awali ya yote naomba nichukue nafasi hii nimpongeze sana Mheshimiwa Waziri Mkuu kwa hotuba yake ya jana ambayo imesheheni mambo makubwa yanayofanywa na Serikali ya Awamu ya Tano. Yeye mwenyewe Waziri Mkuu anafanya kazi nzuri ya kusimamia Serikali kuzunguka nchi nzima na kufanya kazi vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nimpongeze Mheshimiwa Rais Magufuli kwa kazi nzuri sana ya Serikali yake. Serikali inafanya kazi nzuri sana, kila mtu humu ni shahidi kazi inayofanyika kubwa sana. Kujenga reli ya kisasa ya kimataifa ya umeme, ndege zimenunuliwa zinakuja, barabara zinajengwa, madini hata kesho wanafungua ukuta mkubwa pale Mererani kuzuia wizi wa madini, sekta ya umeme, sekta mbalimbali zinashughulikiwa na zinapiga hatua kubwa sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikisema hivyo bado kuna nafasi ya kufanya vizuri zaidi na nimesimama hapa kuchangia maeneo mawili, maji na kilimo. Katika maji vijijini kila Mbunge anaposimama hapa hasa Wabunge wa vijijini wanazungumzia maji vijijini, bado kuna tatizo kwenye maji vijijini. Niombe sana lile wazo tulilokwishalisema humu ndani, la kuanzisha Wakala wa Maji vijijini lianzishwe mara moja. Tuanzishe wakala wa maji vijijini. Maji vijijini bado ni changamoto kubwa, wananchi vijijini wana changamoto kubwa sana ya kupata maji salama na safi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwangu kule kuna maeneo mengi ambayo ukiona maji wanayotumia wananchi utashangaa na kuogopa. Wanatembea kilometa tatu, kilomita nne kupata maji hayo, hayo maji yenyewe yanafanana na chai ya maziwa, ndio wanayotumia, ndio wanayokunywa, ndio wanayopikia. Sasa tukianzisha Wakala wa Maji tutapambana na hali hii tutaweza kupata maji mazuri kwa wananchi wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niliposimama juzi hapa kuzungumzia maji lilikuwa swali nikajibiwa kwamba tayari kuna pesa kwenye mfuko wa maji zaidi ya shilingi bilioni 160. Sasa kama kuna fedha lakini hazitumiki na yenyewe haina tija. Wakala aanze, hiyo fedha bilioni 160 ianze kutumika katika vijiji vyetu. Wakala aanze, atafute fedha, ajenge miradi ya maji vijiji. Kila Halmashauri ilikuwa na miradi 10 ya maji, mingi ya hii haijakamilika, asilimia kubwa haijakamilika hakuna fedha, Wakala wa Maji uanzishwe kusudi tupate ufumbuzi wa tatizo la maji vijijini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tulitoa mfano kwamba REA imekuwa na mafanikio makubwa na REA ni Wakala wa Umeme Vijijini. Tuwe na Wakala wa Maji Vijijini tupate kufumbua tatizo la maji. Kule kwangu kwa mfano kata ya Ruhunga maeneo ya Rugaze kule Vijiji vya Rugaze, Kibirizi, Rubweya, Kyamolaile kuna sehemu nyingine nyingi, maji ni changamoto kubwa sana na ufumbuzi ni huo tu tupate Wakala wa Maji atafute fedha, kwenye bajeti kwenye vyanzo vingine, misaada na mikopo kutoka nje, kusudi tatizo la maji liweze kupata ufumbuzi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili ninalotaka kuzungumzia ni kilimo, ukisoma Ilani ya CCM ya mwaka 2015, kuna makambi ya kilimo. Ukienda Dar es Salaam au miji mingine lakini Dar es Salaam hasa kuna vijana wengi sana maeneo ya mbalimbali Buguruni pale, Ubungo ukienda Mwenge, ukienda Tandale, Mbagala, Temeke, kila maeneo kuna vijana wengi sana ambao hawana kazi wanayofanya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vijana wale wanauza pipi, wanauza kandambili, wanauza vitambaa vya mikononi na vijana wenye nguvu vijana wenye miaka 25, miaka 30, miaka 18 wanauza pipi, hawana kazi ya kufanya. Ukiwaambia waende kulima mashambani hawatakwenda kwa sababu jembe la mkono ni tatizo, wanaogopa jembe la mkono na wana haki ya kuliogopa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niliwahi kusema ndio maana ikaingia kwenye Ilani ya Chama cha Mapinduzi ya Uchaguzi wa mwaka 2015 kwamba tuanzishe kambi za kilimo za vijana. Maeneo mengi Tanzania yana rutuba, maeneo mengi ya Morogoro kule Kilosa, Mvomero, ukienda Rukwa, ukienda Kigoma hata Dodoma hapa shida ni maji tu. Maeneo yana rutuba sana na maeneo makubwa ambayo hayajalimwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilisema vijana wapelekwe kule ukisema kila kambi vijana 100, ukawapa trekta moja au mbili ya mkopo au power tiller kadhaa na msimamizi wa kuwasimamia bwana shamba ambaye amesomea hayo mambo ya kilimo kidogo, wakaanza kulima alizeti, wakaanza kulima maharage, mahindi, pamba na mazao mengine ya muda mfupi na ya muda mrefu, hawa vijana baada ya miezi sita watakuwa matajiri. Baada ya miezi sita kwa trekta moja au mbili nchi hii itakuwa na chakula kingi sana shida ya chakula itakwisha, Tanzania itakuwa tajiri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilikuwa Bungeni humu miaka mitatu iliyopita nikaona Naibu Waziri mmoja anaenda kwa Waziri wa Kilimo wakati huo, anamwambia amepata maombi ya nchi nafikiri ilikuwa Ghana au Nigeria, wanaomba kununua chakula, akamjibu chakula hakipo kwa sababu kimeshauzwa Kenya, ile reserve ya chakula imekwisha. Sasa tungelima chakula kwa njia hii ya makambi ya vijana ambao ni wengi sana ardhi ipo tungepata mafanikio makubwa sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna nchi ambazo hazilimi nchi za jangwa kama huku kaskazini au Uarabuni hawalimi wale lakini wanakula na wana fedha nyingi sana. Tulime kwa wingi sana kwa vijana hawa kwa kutumia trekta na power tiller na vifaa vingine, tupate mazao mengi sana, tupate ufumbuzi kwanza kwa ajira kwa vijana hawa na ufumbuzi wa kukuza uchumi wa Taifa letu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tusifanye makosa ambayo tuliyofanya huko nyuma miaka ya 1974 tulipoanzisha vijiji vya ujamaa tufanye kwa mpango mkakati mzuri. Moja, tunapoanzisha mkakati huu wa Makambi ya Kilimo kwenye Wizara husika kama ni ya Kilimo kama ni ya Masoko au kwingineko Serikalini, kuwe na vitengo maalum vya kutafuta masoko ya mazao haya nje. Huko Dafur Sudan huko, nchi za jangwani huko ambako hawalimi, nchi za Uarabuni huko, kuwe na mkakati maalum wa kutafuta masoko ya kuuza hayo mahindi, maharage, alizeti, korosho na mengine, kuwa aggressive kuuza mazao haya kwa bei nzuri na kwa wakati ili vijana hawa wapate fedha wanayohitaji ambayo wameifanyia kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama nilivyosema hapo mwanzo, kilimo hiki kiratibiwe vizuri kuwe na Bwana shamba au Bibi shamba na researchers officers ambao watasaidia vijana hawa katika kulima kisasa, kutumia pembejeo, mbolea na madawa na kadhalika. Tusitegemee mvua, tusitegemee mvua, nchi hii maeneo mengi ina mvua mara mbili kwa mwaka. Hata pale ambako penye mvua moja kama Dodoma kuna mabwawa ambayo ukizuia ukapiga tuta pale mbele unazuia maji mengi sana huku nyuma, unamwagilia mwaka mzima au angalau miezi nane kwa mwaka wapate tija ya kilimo ambacho nakizungumzia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hii itaondoa kilimo ambacho tumekizoea cha mkulima mmoja mmoja ambacho ni vigumu kumhudumia mkulima mmoja mmoja kumpelekea pembejeo, mbolea, madawa ni vigumu sana. Wakiwa kikundi cha 100 au 200 ni rahisi kuwahudumia na huduma ikawa nzuri ya kupeleka pembejeo na kuondoa mazao ukapeleka kwenye soko. Nchi zote duniani zilizoendelea Marekani, Ulaya wameendelea kwa kilimo. Tu-modernize kilimo chetu kwa vijana hawa wakapata ajira na nchi itapata neema kubwa sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunapozungumzia viwanda, uchumi wa viwanda, viwanda vingi vinategemea kilimo, kama mahindi, pamba na kahawa ambavyo baadaye unaweza kuvi-process. Kwa hiyo, baadhi ya viwanda tena vingi vitatumia mazao haya haya kuongezea uchumi wa viwanda katika nchi yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa nafasi hii.