Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Ofisi ya Waziri Mkuu

Hon. Jitu Vrajlal Soni

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Babati Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Ofisi ya Waziri Mkuu

MHE. JITU V. SONI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Kwanza nichukue fursa hii kumshukuru Mwenyezi Mungu pia naomba niipongeze Serikali hasa Waziri Mkuu kwa kazi nzuri wanayofanya kwa kufanya uratibu mbalimbali na kuhakikisha kwamba shughuli zote za Serikali zinaenda. Kuna maeneo mbalimbali ambapo ningependa kushauri na naamini kabisa ushauri utazingatiwa kama ilivyokuwa siku zote unazingatiwa ili shughuli ya maendeleo iende vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nilikuwa naomba kwanza suala hili la budget process ya kwetu tuangalie namna Serikali iangalie nasi tuendelee kushauri tubadilishe mfumo wetu wa budget circle kwa sababu mengi tunayozungumza leo tayari ceiling zimeshawekwa na maeneo mengi watu wameshapanga bajeti zao, kufumua na kuiandaa upya inakuwa ni ngumu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ingekuwa ni vizuri sisi tungekuwa tunajadili mambo mengi, nini kipande nini kishuke, mabadiliko gani yaje yawe yanafanyika kuanzia mwezi wa Nane mpaka mwezi wa kumi na moja ili watu wanapoandaa bajeti zao basi shughuli hizi zote ziweze kuendana na budget circle na kama kuna mabadiliko tuweze kwenda.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia tuwe na mfumo, kwanza tujue kabisa mapato yetu ni shilingi ngapi ili kutokana na yale makusanyo ndiyo tupange matumizi yake. Hapo tukiweza kufanya ninaamini kabisa hili suala la kusema fedha hazijatosha, hazijaenda kule kutokana na hii cash budget itakuwa tatizo hilo tumeondokana nalo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine, naomba niipongeze kwanza Sheria ya Manunuzi tumeifanyia mabadiliko mara kadhaa na inaenda vizuri, tumeona mafanikio makubwa katika sekta kwa kutumia force account katika sekta ya elimu, afya. Hata hivyo, bado hiyo hiyo Sheria ya Manunuzi inatumika vibaya na fedha zote tunazokusanya bado matumizi ni mabaya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano, tukienda kwenye manunuzi ambapo tunaendelea kutoa tender na wale wanaopokea zile tender bado bei zao ziko juu. Kwa mfano, ukienda TEMESA, TEMESA ni chaka moja ambapo mahali manunuzi yale bado ni tatizo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, fedha nyingi za Serikali zinapotea pale TEMESA, TBA na taasisi nyingi za Serikali ambazo zinatoa huduma, unakuta gharama zao ni kubwa kuliko ya private sector na pesa zetu nyingi zinapotea huko.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine ni suala la kwenye viwanda. Naomba kwamba tuna sera nzuri tunaelekea kwenye uchumi wa viwanda lakini tusipoangalia kwa undani tukafanya uchambuzi wa kina kwamba gharama za uzalishaji ambazo zinakuwa ni kubwa kuliko bei ya bidhaa ambayo inatoka nje, bado hatutaweza kuwa nchi ya viwanda na utakuta bado tutakuwa tunaagiza vitu kutoka nje. Sehemu kubwa inatokana na utitiri wa masuala ya tozo, ushuru, ada na kodi. Hayo yakifanyiwa kazi nina uhakika kwamba viwanda vyetu vya ndani vinaweza vikafanya vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niendelee kuipongeza Serikali haswa kwa upande wa miundombinu; huko Babati Madaraja yameendelea kujengwa. Daraja la Magara, daraja la Mtogiheri na madaraja mengine yamejengwa vijijini ambayo hata barabara za trunk roads hayapo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika suala la barabara ningeomba Serikali iangalie upya suala la mgao wa fedha zile ambazo zinaenda TANROAD na ambazo zinaenda TARURA. Ningeshauri kwamba tuwe fifty fifty kwa sababu TARURA ndiyo ina kilometa nyingi za barabara na hiyo ingefanya barabara za vijijini pia ifanye kazi vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia naomba kwenye suala la elimu hasa elimu stadi. Katika Bunge lililopita tuliweza kupitisha hapa sheria ambayo ilichukua skills development levy ile asilimia nne tukagawa mbili kwa mbili. Mbili zikaenda kwenye Bodi ya Mikopo kwa dharura kwa muda wa mwaka mmoja, lakini naona kwamba sasa bado imeendelea kubaki huko.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ningeomba ile pesa yote asilimia nne irudi iende sasa kwenye ufundi stadi, VETA kwa sababu VETA yetu pia inataka mabadiliko makubwa. Leo tukitaka uchumi wa viwanda, viwanda vyote siku hizi ni mambo ya ICT na tusipobadilika na mfumo huo kwa kufundisha vijana wetu masuala ya ICT bado wale watakaokuwa wanapata mafunzo pale itakuwa hawajafikia hatua nzuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine ni suala la maji. Naomba Serikali ijitahidi kuhakikisha kwamba Wakala wa Maji Vijijini ianzishwe mapema ili miradi ya maji iweze kwenda vizuri. Pia pesa ambayo inatengwa kutokana na ile shilingi hamsini tuliyoweka, basi yote ile iende kwa ajili ya maji vijijini, lakini tunaomba kwenye bajeti hii basi Serikali ifikirie kuongeza shilingi hamsini nyingine iwe mia ili Mfuko wa Maji uweze kutuna wananchi vijijini waweze kupata maji. Niihakikishie Serikali wananchi wote hawatajali kupanda kwa gharama zingine ili wananchi wenzao wa vijijini waendelee kupata maji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna suala lingine la upande wa Kilimo. Naiomba Serikali sasa ijitahidi kuhakikisha kwamba Benki ya Kilimo iwezeshwe ule mtaji ambao waliahidi kwamba itawezeshwa ili wakulima waweze kukopa kule na suala la utafiti pia tuwe na fedha za kutosha kuhakikisha kwamba tafiti mbalimbali zinaendelea kufanyika, kile chombo ambacho tumeanzisha Tanzania Agricultural Research Institute iweze kuanza kazi yake mara moja na fedha zake ziweze kupatikana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine ambalo ni muhimu sana leo hii fedha za OC zinaenda vizuri ambazo zinajumuisha mishahara na gharama zingine za kawaida, lakini fedha za maendeleo zinaenda kutokana na pesa inavyopatikana. Ningeomba kwamba kama kuna uwezekano tuangalie kama tunaweza kupanga kwa uwiano kwamba fedha asilimia fulani zikienda za OC basi na za maendeleo ziwe zinaenda zinafanana. Nasema hivi kwa sababu kama OC imeenda asilimia 100 na za maendeleo imeenda asilimia 10 wanaenda kusimamia nini kwa sababu ile fedha tunaendelea kupoteza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo zote ziendane na kama tunaona kwamba hatuna fedha za kutosha kwa maendeleo kwa miradi yote, basi tuweke vipaumbele mwaka huu itakuwa Wizara kadhaa tunawekeza fedha huko zote halafu OC kwenye hizo Wizara ambazo hazipati fedha za maendeleo tupunguze kabisa zote ziende kwenye suala la maendeleo ili value for money iweze kuonekana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine ambalo ningeomba Serikali huko ndani ya Serikali suala la PPP bado halijaeleweka vizuri. Ningeomba kwanza papatikane elimu ya kutosha na semina mbalimbali kwa Wabunge, lakini pia kwa Watumishi wote ili tukikaa pamoja vizuri naamini kwamba suala hili la PPP inaweza kutusaidia na tukapata mafanikio makubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ambalo ni muhimu ni kuhakikisha kwamba tunakuwa na mifumo mbalimbali kwa mfano kwenye madini. Kwenye Sekta ya Madini ningependekeza niwapongeze Serikali kwa kazi nzuri iliyofanyika, lakini pia kile kituo cha Arusha ambacho kinatoa mafunzo kwa kufundisha watu wa kuchakata madini kutengeneza jewellery na vito, basi fedha za kutosha ziwekezwe ili tuweze kuzalisha wataalam wa humu ndani nchini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine la mwisho, ni kwenye masuala ya maafa. Ningeomba Serikali pia tujipange, maeneo mengi haya maafa yangeweze tukaepukana nayo kwa kupanga. Tukiwa na master plan ambayo hasa Miji yetu na katika maeneo ambayo yanakuwa sasa miji midogo tuwe na master plan ili tuweze kuepuka masuala mbalimbali ya maafa. Pia katika maeneo yote ambapo yanatokea mafuriko tuhakikishe kwamba Serikali tujipange na tujue chanzo cha mafuriko ni nini tuweze kuzuia yale mafuriko ili tusitumie fedha nyingi kwenye masuala ya maafa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia ningeomba Taasisi zote za Serikali kwa mfano Fire, watu wa Traffic wakusanye mapato yao yote kwa njia ya kielektroniki na hiyo itaziba mianya hii ya pesa ambazo zinaendelea kupotea na tukipata fedha nyingi Mfuko wa Serikali ukiwa umetuna vizuri nina uhakika kabisa kwamba fedha za maendeleo pia zitakuwa zinatoka na tunaweza kwenda vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, la muhimu, tuendelee kuangalia suala hilo la Sheria ya Manunuzi na pia suala hilo la viwanda namna ya kukaa pamoja na kuhakikisha kwamba sera yetu inakaa vizuri, lakini pia gharama zote za uzalishaji wote tuzielewe. Tukiwa tunaelewa kwa pamoja naamini kabisa kwamba bidhaa zote ambazo tunaagiza kutoka nje, hasa za kilimo na bidhaa zingine za mifugo nyama, samaki hizo zote ambazo tunaweza kuzalisha nchini tungewekeza basi huko tuzalishe bidhaa zote, sisi ndio tuwe tunapaleka nje na exports ziwe kubwa kuliko imports hasa kwa vitu ambavyo vinawezekana ndani ya nchi hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naamini kabisa kwamba Mheshimiwa Waziri Mkuu pamoja na timu yake ya Mawaziri, Naibu Mawaziri, lakini pia Watendaji wote huko Serikalini wanaweza kujipanga na haya yote ambayo tunashauri wakafanikisha kwamba tuweze kupanga na mambo yakaenda vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine ambalo naomba ni suala zima la migogoro ya ardhi, Tume mbalimbali zimeundwa, naomba haswa kwa mfano kule Babati, migogoro ya ardhi kwa hifadhi zile mbili za Tarangire na Manyara, Vijiji vya Hayamango, Gedamar, Gedejabong lakini pia Vilimavitatu migogoro ile na yale mashamba ya Kiru tufike mwisho.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baadhi ya migogoro ile ina miaka zaidi ya 25, hivyo tumalize ili watu waishi kwa amani, wafanye kazi ya maendeleo kwa sababu tayari nishati imefika katika maeneo mengi, barabara zimeboreshwa na wapo tayari kufanya kazi, kitu kinachozuia ni hiyo migogoro michache ambapo tukiweza kuwekeza suala zima ya maendeleo huko tutakuwa tunaenda vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba suala zima la uratibu pia katika ofisi ya Mheshimiwa Waziri Mkuu, suala zima la kusaidia watu wenye ulemavu na wenye mahitaji maalum kwamba Mfuko ule wa UKIMWI utafutiwe chanzo cha kudumu cha…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa mzungumzaji)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante na naunga mkono hoja.