Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Ofisi ya Waziri Mkuu

Hon. Nuru Awadh Bafadhili

Sex

Female

Party

CUF

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Ofisi ya Waziri Mkuu

MHE. NURU A. BAFADHILI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi hii. Awali ya yote, napenda kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kuniwezesha kusimama hapa nikiwa katika afya nzuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kutokana na bajeti hii nitazungumzia kuhusu elimu na afya. Nikianzia na suala zima la elimu, hivi karibuni tulimsikia Rais Mstaafu wa Awamu ya Tatu, Mheshimiwa Benjamini William Mkapa, akilalamikia ufaulu mdogo wa wanafunzi wetu katika shule zetu za Serikali. Ni kweli wanafunzi wetu katika shule za Serikali wanapata elimu lakini haifanani na wanafunzi wa shule za binafsi. Kwa sababu shule za sekondari za Serikali utakuta darasa moja lina wanafunzi 45, 50 mpaka 60; ni sekondari nayo hiyo. Shule za binafsi utakuta labda form one wako 20, form two wako 25, lakini hawazidi 40 na Walimu wapo wa kutosha ambao wanawafundisha wale wanafunzi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kitaaluma mimi ni mwalimu. Mwalimu unatakiwa katika muda wa dakika 40 unazopewa, uzungukie wanafunzi wote wa darasani kwako ili ujue kosa lake; amefanya nini katika kazi uliyompa au anahitaji msaada gani? Sasa utakuta darasa lina wanafunzi 70 au 80, utawazungukiaje? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, Serikali iangalie pia uwiano wa wanafunzi katika madarasa yetu. Walimu wanafanya kazi, wanajitahidi, lakini madarasa yanajaa wanafunzi kiasi ambacho msaada unakuwa ni mdogo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile Serikali iwaangalie sana wanafunzi wetu. Kila siku mimi natamka, nasema, “mwanafunzi mwenye njaa, hafundishiki.” Kuna wanafunzi wengine, pengine amekula saa 11.00; asubuhi hajala chochote anaambiwa aende shule. Kwa kweli mwanafunzi yule kwake itakuwa ni vigumu sana kusoma.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wenzetu kule shule za watu binafsi, au wenzetu Wazungu wanasema za private, utakuta wanafika kule saa 4.00 kuna kantini, mzazi kampa mtoto wake pesa, anajinunulia chakula. Mchana vilevile anajinunulia chakula. Sisi watoto wetu, anaondoka nyumbani pengine hata uji hakunywa asubuhi na hata senti 20 au Sh.50/= za kwenda kumuwezesha kununua chochote cha kutafuna, hakupewa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa akili itakuwa kwenye kusoma au atawaza njaa? Mara nyingi wanafunzi wa namna ile, utakuta hawashiki lolote katika akili zao, kwa sababu anawaza nikitoka hapa nitakwenda kula nini? Kwa hiyo, Serikali ifanye utaratibu wa kuwawezesha angalau wapate uji. Saa 4.00 mwanafunzi akipata uji, atajua kuwa nikifika shuleni nitapata uji, nitakunywa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile napenda kuzungumzia kuhusu Walimu. Walimu kweli wanafanya kazi, lakini kuna maneno. Sisi tulipoanza kazi ya Ualimu tuliambiwa Ualimu ni wito kama Shehe, Padri, Sister au Askofu. Imani ile sisi ilituingia. Sasa hivi tuna Walimu wenye matatizo. Mwalimu amekwenda shule, asubuhi tayari ameshalewa. Hivi mwanafunzi atakwenda kusoma nini kwa Mwalimu yule ambaye amelewa? Au Mwalimu usiku anakwenda kwenye mabaa mwingine anajiuza. Mpaka wanafunzi wanafikia kumdharau Mwalimu darasani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, Serikali ihakikishe kuwe na utaratibu maalum au kuwe na circular maalum inayowafanya Walimu wawe wanaiheshimu ile kazi ya Ualimu, kama sisi tulivyoambiwa kuwa Ualimu ni wito. Ndiyo maana viongozi wengi hapa ni Walimu kwa sababu walikuwa na nidhamu nzuri sana. Kwa hiyo, tuwaangalie.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile tuangalie stahiki za Walimu. Kuna Mwalimu anapandishwa daraja lakini anaweza kukaa miaka miwili hajapewa pesa zake. Kwa hiyo, Walimu nao wanachoka, ndio wanafanya kazi vilevile wanavyotaka. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa nizungumzie kuhusu suala la afya. Nitazungumzia kuhusu hospitali yangu ya Mkoa ya Rufaa ya Tanga, Bombo. Kwa kweli ile hospitali inapokea wagonjwa kutoka sehemu mbalimbali, lakini ile hospitali ina tatizo moja; Hospitali ya Bombo haina lifti ya kuwapandisha wagonjwa katika jengo la Galanos.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wagonjwa inabidi wapandishwe kwa kutumia mabaunsa. Kuna watu maalum wenye miili mikubwa wamekaa pale, unawalipa ndio wanakupandishia mgonjwa wako juu ili aende wodini akalazwe. Kwa hiyo, Serikali iangalie jinsi gani itaitengeneza ile lifti ya Hospitali ya Bombo ukizingatia hospitali ile ndiyo Hospitali yetu ya Rufaa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile napenda kuzungumzia kuhusu Hospitali ya Wilaya. Sisi kama Wilaya ya Tanga nasema hatuna Hospitali ya Wilaya. Hospitali ya Wilaya huwezi kuifananisha na Kituo cha Afya kimoja kinaitwa Makorora, kingine kinaitwa Ngamiani, kingine kinaitwa Pongwe katika Kata ya Pongwe. Vile vituo huwezi kuvilinganisha na hospitali yetu ya Wilaya. Nimeitembelea ile Hospitali ya Wilaya, nimekuta vile vyumba ni kama mabweni ya wanafunzi wa sekondari, yaani kabisa haikujengwa kihospitali ya Wilaya. Ni ili mradi tuambiwe Tanga tuna Hospitali ya Wilaya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Hospitali hiyo ya Wilaya haikuzingatia miundombinu ya walemavu. Kuna ghorofa ya kupanda huko juu. Sasa mlemavu akiambiwa apande juu, atapanda vipi? Hospitali hiyo ya Wilaya pia hatuna ambulance ya Wilaya. Kwa hiyo, watu wa Tanga Hospitali ya Wilaya pia tunategemea pia hivyo Vituo vya Afya na vilevile tunategemea Hospitali ya Rufaa ya Bombo. Kwa hiyo, naiomba Serikali ihakikishe Tanga na sisi tunapata hospitali yetu ya Wilaya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Hospitali ya Wilaya iliyojengwa, inaelekea kama ilijengwa kwa mshtuko sijui; imejengwa labda kisiasa au vipi, kwa sababu tulikuwa na kiwanja chetu cha hospitali kiko sehemu za Mwakibila Kata ya Tangasisi. Miaka kati ya 2007 mpaka 2010, kiwanja kile kiliuziwa mwekezaji. Mwekezaji yeye hakujenga chochote, badala yake kikahamishwa kiwanja kilichokuwa kijengwe hospitali kikapelekwa hiyo sehemu ambayo inaitwa Masiwanishamba, lakini miundombinu ya kwenda huko Masiwanishamba pia hakuna.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Hospitali hiyo hiyo tunayoambiwa ni Hospitali ya Wilaya, ikifika saa 9.30 hospitali inafungwa. Ina maana wagonjwa wanaambiwa wasiugue tena hapo mpaka kesho tena saa moja na nusu, kunakuwa hakuna tena huduma ya hospitali. Kwa hiyo, naiomba Serikali itusaidie hilo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, labda nizungumzie suala zima la kuhusu madawa ya kulevya. Kama tulivyoona kwenye vitabu vyetu tulivyopewa kuhusu masuala mazima ya dawa za kulevya, ni dhahiri kwamba vijana wengi wanaotumia dawa za kulevya wakipelekwa kwenye Sober House wanatulia vizuri wanakuwa wazuri, lakini wanaporudi tu kwenye maeneo yao na akikutana na wale wengine, wanarudia tena kazi yao. Kwa hiyo, inakuwa ni kama kumpigia mbuzi gitaa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa naiomba Serikali kama itawezekana ihakikishe tujengewe Sober Houses kwa ajili ya vijana wetu wale ambao wameathirika na dawa za kulevya. Pia katika hizo Sober Houses tuhakikishe wakifika kule at least wanapata mafunzo mbalimbali ya kazi za mikono. Kuna mwingine atafundishwa labda useremala, mwingine atafundishwa kushona cherehani, kwa hiyo, akirudi huku uraiani anaweza akaajirika pengine akipewa nyezo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nina uhakika hii Serikali ni sikivu. Kwa hiyo, tuhakikishe wale tunaowapeleka katika Sober Houses, tuhakikishe tunawapatia mafunzo maalum. Siyo tu yale mafunzo ya kuwazuia wasile unga, lakini wapate mafunzo ya kuhakikisha kwamba wanapata mafunzo ya kazi za mikono ili akirudi aende akajitegemee mwenyewe katika maisha yake anayoishi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, labda nizungumzie kuhusu rushwa sasa. Hii rushwa yaani imekuwa kama ni donda ndugu, kwa sababu mtu anaambiwa kabisa hapa hatupokei rushwa, lakini ukimaliza anakwambia unaniondoaje...

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa mungumzaji)