Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Azimio la Bunge la Kuridhia Makubaliano ya Paris chini ya Mkataba wa Umoja wa Mataifa kuhusu Mabadiliko ya Tabianchi

Hon. Amb Dr. Diodorus Buberwa Kamala

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Nkenge

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Azimio la Bunge la Kuridhia Makubaliano ya Paris chini ya Mkataba wa Umoja wa Mataifa kuhusu Mabadiliko ya Tabianchi

MHE. BALOZI DKT. DIODORUS B. KAMALA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa fursa ya kuchangia mada hii muhimu iliyo mbele yetu. Naomba nianze kwa kusema kwamba naunga mkono hoja iliyo mbele yetu na naunga mkono hoja hii kwa kutumia hoja ndogo saba.

Mheshimiwa Naibu Spika, hoja ya kwanza kwanini naunga mkono hoja hii, naunga mkono hoja hii kwa sababu itatuwezesha Tanzania kunufaika na shilingi trilioni 195 ambazo tutaweza kuzipata kwa sababu tu ya kuridhia mkataba huu. Kwa nini nasema tutanufaika na sehemu ya fedha hizi? Fedha hizi trilioni 195 zimetengwa kupitia makubaliano ya Nchi za ACP pamoja na Jumuiya ya Ulaya ni bilioni 70 sasa ukiziweka kwa fedha za Kitanzania zinakuja kwenye trilioni 195 na fedha hizi zinaelekezwa kwa nchi 78 kimsingi kwa sababu nchi wanachama wa ACP ni 79, lakini Cuba yeye ni mwanachama mtazamaji, kwa hiyo, yeye hatanufaika hata na shilingi moja.

Kwa hiyo, ukigawa fedha hizi kwa nchi zote za ACP ni fedha nyingi sana na fedha hizi zinalenga kuelekezwa kwenye Global Climate Change Alliance ambayo inalenga katika kutekeleza huo mkataba wa Paris. Lakini pia ni fedha ambazo zitatusaidia sana katika kupambana na mazingira ukizingatia ukweli kwamba rasilimali siku zote huwa hazitoshelezi, kwa hiyo, kila fursa inayojitokeza ya kukuwezesha kupata rasilimali lazima tuichangamkie kwa hiyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja hii kwa sababu najua kwamba tutaweza kunufaika na fedha hizi lakini nina uhakika kabisa kwamba Wizara imejipanga, wameanzisha mfuko wa kutafuta fedha za kupambaa na mazingira na najua mipango ambayo tayari wameshaiweka ya kuhakikisha wanapata fedha na ndiyo maana nalishawishi hata Bunge hili katika bajeti ijayo basi tutenge fedha za kuweka kwenye huo mfuko wa mazingira ili waweze kuandaa miradi mizuri ya kuweza kunufaika na fedha hizi na fedha nyinginezo. Kwa hiyo, hiyo ni hoja ya kwanza kwa nini naunga mkono hoja hii. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini hoja ya pili, ukiangalia mazungumzo yaliyokuwepo kuhusiana na masuala ya mazingira nakumbuka pale Brussels tulikuwa na mazungumzo ya muda mrefu kuhusu mkataba huu maana mkataba huu ulizungumzwa maeneo mbalimbali duniani. Ulizungumzwa New York, ulizungumzwa Brussels, ulizungumzwa Beijing hata Tanzania mlizungumza wakati huo sikuwepo nilikuwa Brussels lakini tulipokuwa Brussels tulizungumza pia. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo moja kubwa ambalo lilichukua muda mrefu kuzungumza na kukubaliana ni kukubaliana kwamba ili kupambana na mabadiliko ya tabianchi, kila nchi itabidi ichangie kulingana inavyoharibu mazingira lakini pia kwa kuzingatia uwezo wake wa kiuchumi. Hoja hii nchi zilizoendelea hazikuitaka sana lakini kwa mara ya kwanza katika dunia hii, nchi za ACP zikaungana na nchi za Ulaya ili kuwa na msimamo wa pamoja wa kwamba katika uharibifu wa mazingira basi kama wewe unaharibu zaidi utatakiwa uchangie zaidi katika kupambana na tabianchi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ni hoja iliyotuchukua muda mrefu lakini nashukuru hatimaye hoja hiyo ilipita na ilipoenda UN mataifa yote yakakubaliana na ndio maana tunaita kifungu namba mbili katika mkataba huu kinachosema mataifa yote duniani yatawajibika kupambana na mazingira kulingana na jinsi anavyochangia, ukichangia kuchafua zaidi basi uchangie zaidi katika kupambana na hayo mazingira kwa hiyo, ndio maana nasema naunga mkono hoja hii kwa sababu ni hoja muhimu inatoa fursa hata kwa mataifa ambayo yanachafua zaidi yaweze kuchangia zaidi katika kupambana na mazingira.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine ambalo ni kwanini naunga mkono haja hii ukiangalia kifungu namba tano kinasema nchi zinazoendelea zitaendelea kusaidiwa kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi. Sasa ukisema nchi zinazoendelea na nchi nyingine zenye uchumi kama wa sisi ni kwamba sisi tunachangia kidogo katika kuharibu mazingira, lakini kifungu hiki kinatuhakikishia kwamba tutaendelea kusaidiwa katika kupambana na mazingira.

Lakini sababu nyingine kwa nini naunga mkono hoja hii ukiangalia sehemu ya pili, kifungu cha 4(2) kinasema nchi zinazoendelea ziendelee kukabiliana na hatua za kupambana na mabadiliko ya tabianchi.

Mheshimiwa Naibu Spika, hakuna mabadiliko ambayo hakuna mkataba ambao utasaini tu usiokupa wajibu, ni kwamba makubaliano haya tuna wajibu wa kufanya ni upi. Wajibu wa kufanya ni kuendelea kuwa na mikakati na kuonyesha dhamira ya kuendelea kupambana na mazingira ndiyo maana tunapopitisha tunatoa ridhaa maana yake tunakubali kama Bunge kwamba tutaendelea kusaidia Wizara yetu ya Mazingira na Masuala ya Muungano kuiwezesha kuendelea kupambana na mazingira hiyo ndio maana yangu.

Mheshimiwa Naibu Spika, na ukiangalia mwenendo wa bajeti Wizara imekuwa ikpatiwa kila mwaka unaona kwamba ilikuwa si fedha zinazotosheleza mahitaji yao yote basi kwa kupitisha kifungu hiki ninakuwa nina uhakika kwamba sasa tunaenda kutenga fedha za kutosha kwa Wizara ya muungano na masuala ya mazingira ili kuweza kusaidia masuala mbalimbali. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja iliyo mbele yetu kwa sababu hata mataifa makubwa kama Marekani na Japan sitawataja baadhi ya viongozi kwa sababu kidiplomasia si vizuri kumtaja mtu, wapo waliosema hawatakubaliana na masuala ya Paris Agreement, lakini naomba kulithibitishia Bunge hili kwamba mataifa yote makubwa mnayoyajua yaliyokuwa yanaonesha hayatakubaliana na kupambana na mazingira tayari yameweka sahihi na tayari yameridhia, sasa wale waliokuwa na wasiwasi waliojaribu kuonesha kwamba hawatakubali, wameshakubali sioni sababu kwa nini sisi tusiridhie kwa sababu sisi ni wanuifaika wakubwa wa makubaliano hayo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuridhia maana yake tutaweza kunufaika na Global Environmental Facility, Adaptation Fund, pamoja na Green Climate Fund na mengineyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini la mwisho hoja ya saba kwa nini hoja iliyo mbele yetu ni muhimu tukiridhia maana yake tunaiambia dunia kwamba tutaendelea kupambana na mazingira, miradi mizuri kama ya Kihansi tutaendelea nayo kuna mradi mzuri sana unaendelea kutekelezwa chini ya ofisi ya Makamu wa Rais mradi kama Ruaha Mkuu, kutunza Ruaha Mkuu kwa sababu tunazungumzia Green Stiegler’s Gorge huwezi ukazungumzia Stiegler’s Gorge wakati unaendelea kuharibu mazingira, lakini tunaposema tunasaini, tunaiambia dunia kwamba tutatunza hata mazingira, lakini tutaendelea kutoa elimu, tutaendelea kutunza vyanzo vya maji, pale Ocean Road kuna mradi mkubwa wa kutunza mazingira na zaidi ya nchi 10 kutoka dunia nzima zinakuja pale kuangalia Tanzania tunafanyaje kutunza mazingira kwa hiyo, ni mfano wa kuigwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa sababu hizo saba naunga mkono hoja iliyo mbele yetu kwa asilimia mia moja.