Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2016 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018

Hon. Shabani Omari Shekilindi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Lushoto

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2016 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018

MHE. SHAABANI O. SHEKILINDI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Kwanza kabisa nimshukuru Mwenyezi Mungu ambaye ameniwezesha mimi kusimama kwenye Bunge lako Tukufu ili niweze kuchangia hoja ambayo ipo mbele yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa nianze kumpongeza Waziri wa Fedha na Naibu wake kwa hotuba nzuri ambayo siku ile ya kusoma hotuba Watanzania wote naamini walikuwa kwenye luninga na kwenye redio kusikiliza hotuba na walifurahi mno. Kwa hiyo, hotuba hii kwa kweli imejibu kiu ya Watanzania hususan wale wa hali ya chini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimpongeze Rais wangu, Mheshimiwa Dokta John Pombe Magufuli kwa kazi anayoifanya kwani sisi katika upande wetu wa dini unasema kwamba Mwenyezi Mungu anapomchagua mtu wake anamtuma Jibril. Jibril anapeleka majibu kwa Mwenyezi Mungu kwamba Mwenyezi Mungu nimeleta jina la Joseph John Pombe Magufuli kwamba huyu ndiyo anakubalika kwa watu, Mwenyezi Mungu anaidhinisha. Mwenyezi Mungu anapoidhinisha anatuma malaika, malaika wanakuja kwetu sasa kusambaza kwenye mioyo ya wananchi kwamba mchagueni John Pombe Magufuli huyu ndiyo Rais wa kweli. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, hii ni tunu ambayo tumepewa na Mwenyezi Mungu ambaye hamuungi mkono Rais wetu kwa juhudi hizi anazozifanya, basi apimwe akili kwa sababu naamini kabisa huu ni ujumbe wa Mwenyezi Mungu, ameletwa na Mungu huyu. Kwa hiyo, kama mtu hatamuunga mkono tunaita ni kizazi cha shetani. Mara nyingi viongozi wazuri wanapofanya kazi vizuri basi wale ambao ni mlolongo wa shetani huwa wanapinga. Kwa hiyo, usione watu wanapinga ujue ni mlolongo wa shetani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa niendelee kuchangia, kwanza nimpongeze Mheshimiwa Mpango na timu yake kwa ujumla hasa kwa kutoa hii tozo ya Road Licence. Hata hivyo, nimuombe tu sasa kwamba amekula ng’ombe mzima amebakisha mkia, kuna hii fire extinguisher na sticker zake ni kodi kandamizi ambayo kwa kweli naomba aiangalie na ikiwezekana nayo iondoke. Kwa sababu yeye mwenyewe naamini anakiri kwamba gari ikipata ajali ule mtungi wewe abiria, dereva au turnboy huwezi kuamka na kuzima gari ile au hao watu wanaokata sticker hizi za fire extinguisher hawawezi kuzunguka barabarani na kukuta gari inaungua na wakazima sijawahi kuwaona. Kwa hiyo, naona hii ni kodi kandamizi itolewe. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hilo, kuna hawa vijana wetu wa bodaboda wameamua kujiajiri na hili ni kundi kubwa sana, nao ikiwezekana hii SUMATRA itoke. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, sasa niende kwenye suala zima la viwanda. Nashukuru kwenye hotuba ya Waziri ameainisha mikoa ya viwanda ikiwemo Tanga lakini cha kushangaza Mheshimiwa Mpango kwenye hotuba yake anasema atatengeneza viwanda vipya wakati Tanga kuna viwanda vimekufa mfano Kiwanda cha Chuma, Kiwanda cha Afritex na Kiwanda cha Foma.

Mheshimiwa Mwenyekiti, halafu kuna Kiwanda cha Chai cha Mponde hakifanyi kazi na hapa lazima niseme, tumeongea vya kutosha, kiwanda kile hakina tatizo lolote ni kizima kabisa, kinaendelea tu kulipiwa bili za umeme. Wananchi, wakulima wa Mponde wanapata tabu sana. Imefikia hatua sasa hata ule mlo mmoja kwa siku hawaupati, hawapeleki watoto wao shule, hawana ada, hata bili ya umeme wameshindwa kulipa. Kwa hiyo, nimwombe Waziri Mpango kwa unyenyekevu na heshima kubwa aliyokuwa nayo atenge hata shilingi bilioni nne akafungue kiwanda kile ili tuweze kuokoa maisha ya wananchi wale. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niende kwenye suala zima la maji. MWewe ni shahidi wakati unaniona nimevaa mabuti niko kwenye barabara ya Soni – Mombo - Lushoto, kumenyesha mvua nyingi mno. Nashindwa kuelewa nimeshaongea sana mbele ya Bunge lako Tukufu kwamba Wizara sasa ipeleke wataalam wa kutujengea mabwawa ili yatumike kwa ajili ya kilimo cha umwagiliaji cha mboga mboga na kuwapa wananchi maji. Vilevile mabwawa haya yatazuia uharibifu wakati wa mafuriko hata kama yatashuka, yatashuka kidogo sana. Niiombe Serikali hebu itenge fedha za kutosha ili ipeleke vijijini ili wananchi wa vijijini waweze kupata maji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na hayo, hizi fedha zinazoenda Halmashauri kwa ajili ya maji naomba sasa mfumo ubadilishwe. Kuna watu wanaitwa DCCA wapewe kazi hawa au kuundwe Mamlaka ya Maji Vijijini, naamini hawa wataenda sawia kabisa na kuboresha huduma na kwenda kwa kasi zaidi ili wananchi waweze kupata maji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara zangu zimeharibika mno. Nimeomba kwa muda mrefu sana barabara ya kutoka Mlalo - Ngwelo – Mlola – Makanya - Milingano - Mashewa ipandishwe hadhi lakini mpaka sasa hivi bado haijapandishwa. Nimwombe Waziri Mheshimiwa Mpango ikiwezekana barabara ile sasa ipandishwe hadhi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama unavyojua barabara yetu ile inashuka matope na mawe, inafunikwa kutokana na mafuriko, kwa hiyo, ningeomba sasa tupate barabara mbadala. Kuna barabara inaanzia Dochi - Ngulwi - Mombo kilometa 16 tu, niiombe Serikali yangu tukufu, sikivu iweze kunisaidia barabara ile ili wananchi wangu wa Lushoto wasiishi kisiwani. Pamoja na hayo, Rais wa Awamu ya Nne aliahidi kilometa nne, nizikumbushie kwa Waziri Mheshimiwa Mpango aweze kutupa hizo kilometa ili tuweze kutengeneza Mji wetu wa Lushoto. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna suala la vituo vya afya, wananchi wangu nimewahamasisha wamejenga vituo vya afya zaidi ya vinne, vimefikia hatua ya lenta lakini kama ilivyo ada Serikali imesema kwamba wananchi wakijenga ikifikia hatua ya lenta basi Serikali inachukua. Kwa hiyo, niombe Serikali sasa nimeshafikisha hatua ya lenta hebu wanipe pesa ili niweze kumalizia vituo vile ili wananchi wangu waweze kupata huduma ya afya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, usambazaji umeme vijijini. Nishukuru Serikali ya Awamu ya Tano ina kasi sana ya kusambaza umeme vijini lakini imetoa vijiji vichache sana. Niiombe sasa Serikali yangu, sisi tumeshaahidi kule kwamba jamani umeme unakuja kama Ilani ya chama inavyosema, sasa unapopata vijiji hata 10 havizidi sijui tutawajibu nini wananchi wale.

Mheshimiwa Mwenyekiti, milioni 50…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa mzungumzaji)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante na naunga mkono hoja.