Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2016 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018

Hon. Edward Franz Mwalongo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Njombe Mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2016 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018

MHE. EDWARD F. MWALONGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante wa kunipa nafasi. Nami nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu, mwingi wa rehema, mpaji wa yote kwa kutujalia afya njema mchana wa leo na tunaendelea kuijadili Bajeti yetu ya Mwaka wa Fedha wa 2017/2018.

Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote, niseme nampongeza sana Mheshimiwa Waziri na Wizara ya Fedha na Mipango kwa ujumla. Vile vile nawapongeza Mawaziri wote na Serikali yetu kwa ujumla kwa kazi nzuri wanazoendelea kufanya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nami nichukue nafasi hii kumpongeza sana Mheshimiwa Rais kwa kazi nzuri anayoifanya kwa ajili ya nchi yetu na kwa manufaa ya Watanzania wote. Leo tumepata taarifa kwamba amekutana na Profesa John ambaye ndio Mkurugenzi wa Barrick, amefika na wamekubaliana kwamba tukae chini tuongee na Kampuni ya Barrick imekubali kutulipa Watanzania sehemu ya fedha ambayo tunaidai na tutarekebisha mikataba kuifanya nchi yetu ipate manufaa makubwa sana kwenye machimbo ya madini mbalimbali ambayo tunayo hapa nchini. Mheshimiwa Rais amesimamia kwa niaba yetu wote Watanzania. Tuna wajibu wa kumpongeza na kumwombea ili aendelee na kazi hiyo vizuri, tuweze kunufaika kama Watanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikijikita kwenye bajeti iliyopo mbele yetu, nianze na suala la maji. Kuna miradi ya maji kwa kweli inasuasua sana. Kama ahadi ya Mheshimiwa Rais inavyosema, ni kumtua ndoo mwanamke wa Tanzania, lakini kwa mwendo huu tunaokwenda, sidhani kama tutafanikiwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika miradi ya maji iliyopo katika Jimbo la Njombe Mjini, upo mradi wa maji ambao tumeambiwa kwamba tutapata fedha kutoka Serikali ya India, ni mkopo. Sasa hivi ni mwaka mzima, hakuna hata dalili ya hiyo fedha kupatikana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumeambiwa kwamba documents na mikataba yote iko ofisini kwa Mheshimiwa Waziri wa Fedha na Mipango, kwa taratibu za nchi na nchi. Hebu tuombe sasa basi hiyo fedha ipatikane ili Mradi huu wa Maji wa Njombe Mjini uweze kufanyika, vinginevyo wananchi wa Njombe wataendelea kuteseka sana na kuona kwamba Serikali haiwajali. Mji wa Njombe jinsi ulivyo, umezungukwa na mito pande zote mbili; ni jambo la kusikitisha sana kwamba tunapokuwa Njombe tunakosa maji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, siyo hiyo tu, miradi ya maji ya Njombe inasuasua sana na kinachofanya isuesue; na nimeshalalamika sana hapa Bungeni, inawezekana kabisa kwamba ndani ya Halmashauri ya Mji wa Njombe kuna shida ya wataalam. Tunaomba sana Wizara ya Maji na Umwagiliaji ikishirikiana na Wizara ya Fedha na Mipango waone namna gani wanaweza kutusaidia tupate wataalam wa kutosha waweze kusaidia hii miradi iweze kwenda ukiwemo Miradi Rugenge na Igogwe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikiacha Miradi ya Maji ya Njombe nije suala la Liganga na Mchuchuma. Suala hili kwa kweli linasikitisha sana. Ni mradi ambao ni miaka mingi sana tumekuwa tukiuongelea. Wapo watu mpaka sasa wanazeeka wanaacha Liganga na Mchuchuma.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa bahati mbaya sana ukizungumza habari ya Liganga na Mchuchuma, watu wanafikiri ni vitu ambavyo viko hapo hapo pamoja. Ni kwamba Liganga na Mchuchuma viko sehemu mbili tofauti na vina umbali zaidi ya kilometa 80. Kutoka Liganga kwenda Mchuchuma pana kilometa 80, lakini kinachotakiwa kuchimbwa ni chuma kilichopo Liganga na kuna makaa ya mawe yaliyopo Mchuchuma. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama tunataka kuvuna chuma hivi ni kweli makaa ya mawe ya Mchuchuma yatatumika yote kwenye chuma? Kama makaa haya yana matumizi mengine, basi makaa yaanze kutoka. Hivi makaa yanahitaji process gani? Kwa sababu tunachojua sisi, kwa
mfano ukienda kule Ruvuma wanakochimba makaa ya mawe, kiko kile kijiko kinachimba na crusher, vitu viwili tu; na magari yanasomba yanasafirisha makaa. Tuombe na sisi yale makaa yaanze kutoka tuanze kupata manufaa yake. Vinginevyo tuambiwe kwamba makaa ya Mchuchuma yanatosha kwa ajili ya kiwanda cha Liganga tu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, dalili ya mvua ni mawingu. Tunapotaka kuchimba chuma cha Liganga na tunapotaka kuchimba makaa haya ya Mchuchuma yatasafiri kwa barabara. Barabara ya Itoni – Manda ni ya vumbi na ipo kwenye ilani iliyopita na ipo kwenye ilani hii. Tumeambiwa itaanza kutengenezwa kwa kiwango cha lami.

Mheshimiwa Mwenyekiti, fedha iliyopatikana ni kuanzia kipande cha kilometa 60 kuanzia Mawengi mpaka Lusitu. Sasa kipande hiki ni kidogo sana, sehemu kubwa ya barabara itakuwa bado ya vumbi. Kama kweli hiki chuma kitatoka, maana yake kutakuwa na malori yanayosafirisha chuma kwa sababu tumeambiwa uzalishaji ni tani milioni moja kwa mwaka. Ukifanya hesabu ya kawaida tu kwamba lory libebe tani 30, ni malori 76 kwa siku yatabeba chuma. Kweli malori 76 yatapita barabara ya vumbi? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, sisi Wananjombe tunaona kabisa kwamba hatutendewi haki na hatuambiwi ukweli. Tunaambiwa tu kwa kuridhishwa kwamba huu ni mradi wa kielelezo, lakini hakuna cha kielelezo wala cha nini. Sasa tunasema tunataka kazi hii ianze, kama haianzi, basi habari ya kwamba Mchuchuma na Liganga ni mradi wa kielelezo, ifutwe na isiwepo, tuseme kabisa kwamba hii tumeiacha kwa sababu ni deposit ya miaka ijayo, karne ijayo na vizazi vijavyo. Ieleweke hivyo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara sisi tunaihitaji, kwa sababu ukiacha Mchuchuma na Liganga, tunahitaji kusafirisha mazao. Chakula kingi kinatoka Ukanda wa Ludewa; viazi vinatoka Ukanda wa Ludewa, vije kwenye masoko yanayotakiwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara ya Njombe – Ludewa inatakiwa iwe ya lami ili tusafirishe mazao. Kwa sababu tunaona katika nchi hii, sehemu nyingine zimetengenezwa barabara za lami, nasi tunahitaji barabara ya lami. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine, ndugu yangu Mheshimiwa Hongoli pale amelizungumzia. Sisi Njombe miti na mbao ni zao kama mazao mengine. Sasa figisufigisu na mizengwe inayowekwa kwenye mbao inatukatisha tamaa. Kwa sababu mkulima wa kawaida ana uwezo wa kuvuna miti yake na kuiuza sokoni. Vinginevyo, tuambiwe kuanzia sasa ni marufuku wakulima kuvuna miti yao; na maana yake ni marufuku wasipande miti.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mtu anapanda miti, anapasua; akifika barabarani anaulizwa mashine ya EFD kwenye mbao. Jamani, hebu Serikali ifanye kazi, muwe mnajua na mazao ya wananchi wenu, kwa sababu mbao ni mazao ya kawaida. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiacha hiyo, kuna kitu kinaitwa TP (Transit Pass). Sheria inasema, Transit Pass unadaiwa unapovuka Wilaya. Ndani ya Wilaya ya Njombe watu wanadaiwa Transit Pass; ukibeba kuni, Transit Pass; ukibeba mabanzi, Transit Pass; sasa inasikitisha sana kwamba wananchi hawa wanapanda miti; sehemu kubwa ya nchi hii haina miti.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wananchi wa Njombe kupanda miti ni maisha ya kawaida humhimizi mtu. Sasa bado wanakuja kupata adhabu kwenye kuvuna. Kama tunataka twende pamoja tutunze mazingira na mkumbuke kwamba ukanda ule una vyanzo vingi sana vya maji, basi tusaidiane. Kitu kama Transit Pass naomba Serikali itoe ufafanuzi kwamba Transit Pass ikatwe nje ya Wilaya. Kwa mfano, kama unasafirisha mbao kwenda nje ya Wilaya uwe na Transit Pass, mabanzi yasiwe na Transit Pass, kuni zisiwe na Transit Pass ili wananchi wale waone kupanda miti kwao ni sehemu ya maisha ya kawaida na waweze kuona neema. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, liko suala la vijana. Vijana wa Kitanzania tumewasahau jumla! Ni jambo la kusikitisha sana! Kama tunataka kujenga Taifa bora lenye vijana wanaoweza kufanya kazi na kuitetea nchi hii, ni lazima tuweke mikakati muhimu sana na kabambe kwa ajili ya vijana. Vijana wa Tanzania wale tu wanaomaliza Kidato cha Nne kwa mwaka ni vijana 400,000 kwa matokeo ya waliofanya mtihani wa Form Four mwaka 2016. Waliochaguliwa kwenda Kidato cha Tano wapo 99,000. Vijana zaidi ya 300,000 wamebaki. Hakuna mpango wowote wa Kitaifa kuwasaidia. Kichaka tunachojificha ni asilimia 10 ya Halmashauri. Hivi are we serious? Vijana hawa watasaidiwa na asilimia 10 ya Halmashauri?

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni lazima Serikali iseme upya kwamba vijana hawa tuwafanyie nini? Kama Wizara ya Fedha na Mipango mnataka fedha, tengenezeni walipakodi. Hawa ndio vijana walipakodi, wapewe maarifa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimekuwa nikishauri hapa Bungeni, tuanzishe makambi kabambe kabisa ya shughuli za vijana, tuwawezeshe vijana kwa mkakati maalum ili vijana hawa waweze kuwa na kipato. Wakishakuwa na kipato watakuwa walipa kodi, lakini tunapowaacha hivi vijana 300,000 na mwakani 300,000 na mwaka mwingine 300,000, tunakuwa na vijana wazururaji, walalamishi, vijana ambao tutashindwa kuishi… (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa mzungumzaji)