Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2016 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018

Hon. Augustino Manyanda Masele

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbogwe

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2016 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018

MHE. AUGUSTINO M. MASELE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nami nichukue fursa hii kumshukuru Mwenyezi Mungu na kukushukuru wewe Mwenyekiti wetu kwa kunipatia nafasi siku ya leo nami niweze kuchangia hotuba ya bajeti ya mwaka 2017/2018 kama ilivyowasilishwa na Waziri wetu Dkt. Philip Mpango.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Taifa letu la Tanzania limekuwa ni Taifa la mfano katika dunia hii. Taifa letu limejitoa muhanga katika kuwakomboa Waafrika wenzetu katika nyanja za kiuchumi na kisiasa. Sisi kama Taifa tumetumia utajiri wetu kuhakikisha kwamba wenzetu wanajikomboa. Sasa wakati umefika na wakati wenyewe unamweka mbele Rais wetu Dkt. John Magufuli kuvipigana upya vita vya uchumi, ndiyo maana ameamua sasa kuhakikisha kwamba madini na rasilimali zetu zote zinanufaisha Watanzania wote.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwa kusema neno moja kwamba Mwenyezi Mungu ametujalia sana na ametupenda akatupatia rasilimali nyingi na hasa nijikite katika suala zima la vyanzo vya nishati ya umeme. Nishati ya umeme ndiyo msingi wa mambo mengi iwe kilimo, iwe ujenzi, iwe kila kitu ukiwa na umeme wa uhakika utajenga viwanda na ukiwa na umeme wa uhakika utafanikiwa katika mambo mengi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa maana hiyo Mungu katupa gesi, Mungu katupa maji, tunao upepo, tunalo jua la kutosha. Hivyo, niombe Serikali ihakikishe tu kwamba kwa kweli suala zima la uzalishaji wa umeme kutokana na vyanzo vyote hivyo ikiwemo makaa ya mawe yatumike katika kuhakikisha kwamba umeme unapatikana kwa wakati na kwa wingi unaostahili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia niipongeze Serikali yangu kwa kuhakikisha kwamba tunaanza mara moja ujenzi wa Reli ya Kati kwa standard gauge. Kuwepo kwa usafiri wa reli ya kati ambao uko katika standard gauge ni ukombozi wa aina yake katika Taifa letu la nchi jirani za Afrika Mashariki na Afrika ya Kati.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kitabu hiki cha bajeti cha Mheshimiwa Mpango nizungumzie habari ya Bandari ya Dar es Salaam. Bandari ya Dar es Salaam imekuwa na changamoto mbalimbali ikiwemo ile changamoto ya kodi ya ongezeko la thamani kwa usafiri wa bidhaa zinazokwenda nchi za nje.

Mheshimiwa Waziri amesema inakuwa sasa inachajiwa asilimia sifuri ya VAT, yapo malalamiko pia kwa upande wa mawakala wa meli zinazoleta mizigo katika Bandari ya Dar es Salaam nao wanalo lalamiko linalofanana na hili kwamba VAT inatozwa kwa mawakala hawa na hawa mawakala wanapochajiwa wanaweka hiyo chaji kwenye wamiliki wa zile meli, kwa maana hiyo gharama za uendeshaji katika Bandari ya Dar es Salaam zinaonekana kwamba ziko juu zaidi na wenye meli wanakuwa wana-opt kwenda kwenye bandari zingine za jirani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimshauri Mheshimiwa Waziri kwamba na hao mawakala wa meli katika Bandari ya Dar es Salaam na wenyewe wachajiwe kiwango cha asilimia sifuri ili kuhakikisha kwamba hizo meli zisije zikawa zinaelekezwa upande mwingine. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunapozunguzia habari ya ujenzi wa viwanda ni pamoja na viwanda vya mbolea ambavyo tumehaidiwa kwamba kwa sababu tumepata gesi hapa Tanzania na kwa maana hiyo Mtwara na Lindi tungeweza kupatiwa viwanda vya mbolea. Kwa bahati mbaya sana sioni hapa kwamba hizi jitihada za kuweza kujenga hivi viwanda vya mbolea ambavyo vingeweza kukuza kilimo chetu katika Taifa hili vimewekwa katika sehemu gani. Nimwombe Mheshimiwa Waziri aliangalie jambo hili kwa jicho la pekee kwa sababu kilimo ni uti wa mgongo wa Taifa hili na Watanzania walio wengi wameajiriwa katika sekta hii muhimu ya kilimo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimalizie tu kwa kuiomba Serikali katika Wizara ya Nishati na Madini, katika Jimbo la Mbogwe tunao wawekezaji ambao wamekuwa wanafanya utafiti kwa muda mrefu katika eneo la Nyakafuru, naomba mara moja kwa kweli na hawa watu wamulikwe ili kuhakikisha kwamba madini yaliyopo katika Wilaya yetu yanawanufaisha wananchi wa Wilaya ya Mbogwe. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikushukuru kwa kunipa nafasi ya kuweza kuchangia na kwa mara nyingine naunga mkono hoja. Ahsante sana kwa kunisikiliza.