Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Azimio la Bunge la Kumpongeza Mheshimiwa Dokta John Pombe Joseph Magufuli, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa hatua anazochukua kukabiliana na Upotevu wa Mapato ya Serikali katika Sekta ya Madini

Hon. Japhet Ngailonga Hasunga (CPA)

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Vwawa

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Azimio la Bunge la Kumpongeza Mheshimiwa Dokta John Pombe Joseph Magufuli, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa hatua anazochukua kukabiliana na Upotevu wa Mapato ya Serikali katika Sekta ya Madini

MHE. JAPHET N. HASUNGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nashukuru kwa kupata hii nafasi na nalipongeza Bunge kwa kuja na hili Azimio ambalo ni muhimu sana katika kumpongeza Rais. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwenye macho haambiwi tazama na mwenye masikio lazima asikie. Rais amechukua hatua nyingi, Rais amethubutu kuzuia makinikia yasiende nje, Rais amezuia kusafirisha madini yote nje, hizo ni hatua za dhati kabisa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nchi yetu hii ni tajiri sana, tuna madini mengi sana labda nizungumzie kwenye Jimbo langu la Vwawa na Mkoa wa Songwe na Mbeya kuna madini mengi. Kwa mfano, kuna niobium pale kwenye Gereza la Songwe ni madini yanayoweza kutumika kutengeneza injini za ndege, ni madini pekee yamegunduliwa yapo Tanzania. Kuna gesi na kila aina ya madini, tuna makaa ya mawe kule Magamba ambayo hayapo yoyote katika Afrika ni makaa bora, tuna makaa ya mawe kule Kiwira, tuna madini ya dhahabu kule Chunya kuna ugunduzi wa kila aina ya madini.

Kwa sababu Botswana mwaka 2006 ilichukua hatua kama hizo na haikushtakiwa. Utajiri ni wa kwetu, madini ni ya kwetu lazima hatua zichukuliwe. Marais waliotangulia walithubutu kuchukua hatua lakini wale wasaidizi wao hawakuwaunga mkono na ndiyo maana sisi tunasema Marais walifanya kazi nzuri lakini watendaji wasaidizi hawakutekeleza majukumu yao, lazima hawa hatua zichukuliwe. Marais walifanya kazi nzuri na Rais huyu wa Awamu ya Tano hatua anazozichukua lazima ziungwe mkono na kila mtu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi nashukuru nimeona baadhi ya Wapinzani wanasema ile Miswada mibovu mibovu ambayo ina matatizo iletwe, ni kweli ndiyo tunachosema zile sheria zote mbovu mbovu, mikataba ya kila namna ambayo ina matatizo iletwe hapa Bungeni, tuipitie upya kwa uwazi ili iweze kuleta maendeleo ya nchi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nadhani hili ni suala la msingi sana ili nchi yetu iweze kunufaika na rasilimali za madini ambazo ni nyingi sana katika nchi hii. Nchi haistahili kuwa maskini kwa utajiri uliopo ambao tumepewa na Mwenyezi Mungu. Tuna almasi, dhahabu, nikel, uranium na kila aina ya madini, kwa nini tuwe maskini? Lazima tukae chini kama watu tuliokwenda shule tuone ni nini cha kufanya ili nchi yetu iweze kufaidika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nampongeza sana Rais na naomba Wabunge wote tumuunge mkono, tupambane ili nchi hii iweze kuleta maendeleo ya kweli.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa nafasi hii, ahsante sana.