Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jamii Kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2017 pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Masuala ya UKIMWI kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2017

Hon. Dr. Adelardus Lubango Kilangi

Sex

Male

Party

Ex-Officio

Constituent

None

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jamii Kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2017 pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Masuala ya UKIMWI kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2017

MWANASHERIA MKUU WA SERIKALI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwa kukushukuru kwa kunipa nafasi ya kuongea lakini kwa sababu ndiyo nafungua mdomo wangu kwa mara ya kwanza katika Bunge hili Tukufu, basi nianze kwanza kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kutujalia uhai. Nimshukuru pia Mheshimiwa Rais kwa kuniteua kuwa Mwanasheria Mkuu wa Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuwashukuru na kuwapongeza Mheshimiwa Spika, Naibu Spika Mwenyekiti na Wenyeviti wote. Naomba kuwashukuru na kuwapongeza Wabunge wote na hata Watanzania wote ambao wako nyuma yetu (Makofi).

Mheshimiwa Mwenyekiti, wakati wa kuchangia taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jamii yalizuka masuala kama mawili hivi matatu ya kisheria yaliyohitaji ufafanuzi wa Mwanasheria Mkuu wa Serikali. Swali la kwanza lilitoka kwa Mheshimiwa Abdallah Mtolea aliyependa kufahamu uhalali wa Mheshimiwa Rais kumpatia msamaha Nguza Viking maarufu kama Babu Seya pamoja na Johnson Nguza maarufu kama Papii Kocha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, utoaji wa msamaha kwa wafungwa upo kwa namna mbili kisheria; namna ya kwanza ni msamaha wa Rais ambao unatolewa chini ya Ibara ya 45 ya Katiba. Hata hivyo, nieleze hii inaitwa prerogative of mercy ni kama Kiswahili chake nimeshindwa kukipata kwa haraka, lakini ni kama mamlaka ya kutoa msamaha au huruma. Sasa mamlaka haya yanaongozwa na sheria itwayo Presidential Affairs Act na kifungu husika ni kifungu cha tatu (3) (Makofi).

Mheshimiwa Mwenyekiti, namna ya pili ya utoaji wa msamaha ni kupitia Bodi ya Parole huu unaitwa msamaha wa Parole. Aina hii inaongozwa na sheria itwayo The Parole Boards Act na kifungu husika ni kifungu cha nne (4) cha sheria hiyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, msamaha uliotolewa na Mheshimiwa Rais kwa Nguza Viking pamoja na Jonson ni ule wa aina ya kwanza na ambao unaongozwa na hiyo sheria niliyoitaja ya Presidential Affairs Act.

Mheshimiwa Mwenyekiti, palikuwa pia na maswali kutoka kwa Mheshimiwa Suzan Lyimo ni maswali mawili. La kwanza, aliuliza kama ni halali na inakubaliwa kisheria kwa Serikali kukata rufaa dhidi ya uamuzi kuhusiana na Sheria ya Ndoa baada ya miaka miwili kupita.

Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili, ni kwamba kwa Serikali kukata rufaa dhidi ya maamuzi ya kesi hiyo je, inakubaliana na ndoa za utotoni. Kesi aliyokuwa anaizungumzia ni miscellaneous civil cause No. 5 ya 2016.

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali lake la kwanza kama ni halali kukata rufaa baada ya miaka miwili kupita ni suala la procedure na kwa vyovyote vile swali hili linaweza likajitokeza rufaa itakapokuwa inasikilizwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, ndiyo hilo kwamba kwa Serikali kukata rufaa dhidi ya kesi hiyo inakubaliana na ndoa za utotoni. Ni wazi Serikali ilivyokata rufaa imetoa sababu na sababu hizi zitakuwa ni sehemu ya vitu vinavyobishaniwa ile rufaa itakapoanza kusikilizwa. Kanuni ya 64(1)(c) ya Kanuni za Kudumu za Bunge inakataza kuzungumzia jambo lolote linalosubiri uamuzi wa Mahakama na kwa hiyo hatuwezi kulizungumzia hapa. Ahsante sana.