Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jamii Kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2017 pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Masuala ya UKIMWI kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2017

Hon. Nuru Awadh Bafadhili

Sex

Female

Party

CUF

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jamii Kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2017 pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Masuala ya UKIMWI kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2017

MHE. NURU A. BAFADHILI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Awali ya yote napenda kumshukuru Mwenyezi Mungu kuniwezesha kuwa hapa kwa muda huu na kuweza kuchangia hoja iliyopo mbele yetu.

Vilevile napenda kukishukuru chama changu, Chama cha Wananchi (CUF) kinachoongozwa na Profesa Ibrahim Haruna Lipumba kwa kuweza kuniteua kuweza kuwakilisha wananchi. (Makofi)

Mheshimiwa Mweyekiti, nitajikita kwanza kwenye masuala ya elimu. Kwa kweli elimu yetu ni nzuri, lakini kuna matatizo katika elimu. Matatizo yaliyopo ni kwamba mtoto mwenye njaa hafundishiki. Watoto wetu hawafanyi vizuri katika masomo kwa sababu ya njaa kutokana na hali duni ya uchumi. Kwa hiyo, tunaiomba Serikali, ihakikishe inafanya utaratibu angalau wanafunzi wetu wa shule zetu waweze kupata angalau mlo mmoja kwa siku ili waweze kuhudhuria vizuri masomo. Kuna baadhi ya wanafunzi wanashindwa kwenda shuleni, wanakuwa watoro kutokana na ukosefu wa vyakula majumbani kwao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, kama Serikali italitilia mkazo hilo, itawezekana na wanafunzi wetu wakaweza kufanya vizuri katika masomo yao. Kwani sisi tuliposoma pia, tulikuwa tunakwenda shule lakini tunapata milo miwili. Saa 4.00 tunapata uji wa bulga na mchana tunapata chakula ambacho kilikuwa ni mlo uliokamilika. Basi hata kama Serikali itakuwa haina uwezo wa kufanya milo miwili, basi angalau huo mlo mmoja ili mwanafunzi aweze kukaa darasani na kumsikila Mwalimu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitazungumzia kuhusu suala zima la afya. Kwa kweli katika Wizara hii ya Afya kuna matatizo mengi sana. Kwa mfano katika hospitali yangu ya Rufaa ya Tanga, kuna matatizo ya Daktari Bingwa wa Wanawake, yaani Daktari Bingwa wa Akinamama, Daktari Bingwa wa Koo na Masikio. Kwa hiyo, wenye matatizo hayo ya koo, sikio wanashindwa kupata huduma nzuri kutokana na ukosefu wa daktari.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vile vile kuna tatizo la watumishi katika kada zote. Kwa hiyo, Wizara iangalie katika mgawanyo huo wa Watumishi wa kada zote na Hospitali yetu ya Rufaa ya Tanga iangaliwe ili waweze kupata huduma nzuri na zilizo bora zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitazungumzia vilevile kuhusu UKIMWI. Hili ni janga la kitaifa kwa kweli na vijana wetu ndio wanaoathirika zaidi na UKIMWI. Vijana wa umri kuanzia miaka 15 mpaka 24 ndio wanaoathirika zaidi na UKIMWI. Kuna vishawishi vingi kwa vijana hawa na wakati mwingine kuna wazee wengine wanawafuata wasichana wadogo wadogo eti wanadai kuwa wake zao majumbani wamechuja. Kwa hiyo, wanawafuata watoto wadogo na wengine tayari wanaume wale wazee au vijana wakubwa wameathirika, kwa hiyo, wanawaambukiza watoto wetu au vijana wetu wadogo maradhi ambayo hayana tiba. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna mila potofu ambazo zinachangia pia kuambukiza au kuenea gonjwa hili la UKIMWI, mfano kuna mila nyingine mwanamke anapokuwa na mimba, mchumba anachumbiwa akiwa ndani ya tumbo, haijulikani kama kutazaliwa mwanamke au mwanaume. Kwa hiyo, atakapozaliwa mwanaume siyo wake, lakini akizaliwa mwanamke ndiyo atakuwa ni wa kwake. Kwa hiyo, pia hizi ndoa za utotoni zinachangia katika kueneza gonjwa hili la UKIMWI.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile kuna mila za kurithi wajane. Utakuta mke akifiwa na mume wake anarithiwa au wakati mwingine na vile vile mume anarithiwa na mke mwingine. Kwa hiyo, hii inaleta matatizo kwa sababu hajulikani mmojawapo kati ya hao waliokufa amekufa kwa ugonjwa gani?

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, tunaiomba Serikali hili lipigiwe kelele zaidi, lakini vilevile sisi kama wazazi, tuwafundishe watoto wetu maadili mazuri. Kwa kweli kuna wazazi ambao wanajifanya wao kila wakati wako busy, wako kazini tu, hawawaangalii watoto wao nyumbani. Kwa hiyo, maadili yanaporomoka na baada ya maadili kuporomoka, utakuta watoto wanaharibikiwa. (Makofi)

Kwa hiyo, sisi kama wazazi, tuhakikishe tunafuatilia nyendo zote za watoto wetu kwa sababu sisi kama Wabunge nadhani wazazi wetu walitufuatilia tukaenda shuleni tukasoma mpaka leo tumefikia kupata nafasi hii ya kuwawakilisha wananchi wetu. Kwa hiyo, sisi kama wazazi aidha wanaume au wanawake, tuhakikishe tunakwenda vizuri katika kutengeneza maadili katika nyumba zetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hilo hilo kuhusu UKIMWI. Kuna mila nyingine wanatumia vifaa ambavyo havichemshwi. Kwa mfano, watu wanapotahiriwa, wanapokeketwa, wanaotogwa masikio sijui na pua na nini, unaona vitu vile havichemshwi wala haviko katika usalama, kwa hiyo, hivi pia vilevile vinachangia katika kueneza gonjwa hili la UKIMWI.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile tunaiomba Serikali ihakikishe inaongeza bajeti kwa ajili ya kununua dawa za waathirika wa ugonjwa wa UKIMWI...

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzunguzaji)

MHE. NURU A. BAFADHILI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante.