Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jamii Kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2017 pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Masuala ya UKIMWI kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2017

Hon. Edward Franz Mwalongo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Njombe Mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jamii Kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2017 pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Masuala ya UKIMWI kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2017

MHE. EDWARD F. MWALONGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi ili nami niweze kutoa mchango wangu katika hizi taarifa za hizi Kamati mbili. Kwanza kabisa, niwapongeze Wenyeviti wa Kamati jinsi walivyowasilisha kwa umahiri lakini niwapongeze vilevile wanakamati wote walioshiriki kuchakata taarifa hizo mpaka hapo zilipofikia, tunawapongeza sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze na suala la upungufu wa walimu kwenye shule hasa hasa za msingi. Tatizo hili ni kubwa sana na Serikali inachelewa sana kuajiri. Ukitaka kuona Taifa linajimudu ama linaenda vizuri kwa maana ya misingi yake inajitetea vizuri na linaangalia mbele kwamba litafika wapi ni kusimamia elimu. Tunapokuwa hatupeleki walimu shuleni maana yake hili Taifa linaenda kuwa mfu kesho. Watoto hawa wanakosa walimu, wenyewe kama watoto hawawezi kulalamika, lakini matokeo yake tutayakuta huko mbele ya safari kwamba tutakuja kuwa na Taifa ambalo linajiwajibisha kabisa lenyewe kwa sababu watoto hawa watakuwa wamekosa elimu na maarifa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, juzi juzi umetokea mgao wa walimu na tulivyojaribu kufuatilia tuliambiwa ni fidia ya walimu wenye vyeti batili. Mimi katika Halmashauri yangu Mji wa Njombe sikupata mwalimu hata mmoja wakati wenye vyeti batili walikuwa 12, hapa nifanyeje, si nione kama kuna upendeleo? Kama jibu ni vyeti batili, sijapata walimu na mimi wenye vyeti batili walikuwa 12. Kwa hiyo, tukienda kwa utaratibu huo kama ni kweli ni vyeti batili tunagawa tugawe kwa usawa. (Makofi)

Naomba niiambie Serikali kwamba Halmashauri ya Mji Njombe ni jina tu, lakini yenyewe ina kata 13 na kata moja tu ndiyo mji lakini kata nyingine ni vijijini, kwa hiyo, tuichukulie kwa kigezo hicho. Leo hii Halmashauri ya Mji Njombe ina upungufu wa walimu 454, hivi hapa tutatoa elimu kwa hawa watoto, si tunawapeleka tu wakacheze shuleni mwisho wa siku wanatoka hawajapata elimu yoyote. Naomba sana hili liangaliwe kwa sababu elimu ni suala muhimu sana, tukicheza na elimu maana yake ndiyo tunaliua Taifa taratibu. Sisi tunaweza tukawa hatuoni kwa sababu sisi tumepata elimu, lakini kipo kizazi ambacho tunakilea sasa ambacho kinahitaji kupata elimu. (Makofi)

Mheshimwia Mwenyekiti, tumeambiwa watahamisha walimu kutoka sekondari, zoezi hilo linakwenda polepole mno utafikiri kwamba wanaofanya hilo zoezi sijui hawalijui au hawana uhakika au hawajiamini. Haioneshi kabisa kwamba hili zoezi ni la haraka kwa sababu kuna shida ya walimu mashuleni hasa ukizingatia sasa hivi limetolewa tamko la marufuku kuchangisha mashuleni. Madarasa ya awali na baadhi ya madarasa walikuwepo walimu wanajitolea lakini wazazi walikuwa wanachangia sasa hiyo kitu tumeambiwa ni marufuku, hivi hatma ya hawa watoto itakuwaje.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wakati mwingine matamko ya Serikali yanatia shaka kwa sababu unakuja kuona kwamba yalikuwepo madarasa ya awali katika maeneo mbalimbali ambayo yalikuwa yanakwenda vizuri kabisa na wananchi walikuwa wanalipa ada kwa ajili ya watoto wao, Serikali ikasema darasa lolote lile la awali lazima liwe chini ya shule ya msingi, ni marufuku kuwa na darasa la awali nje ya shule ya msingi. Watoto wale wamepelekwa kule shule ya msingi hakuna walimu, wameondoka mahali ambapo kuna walimu, hivi nia hasa ya Serikali ni nini, kwamba watoto wapate elimu au ni mtizamo ambao mimi nauona kwa upande fulani una kama wivu au chuki kwamba hawa wenye shule za watoto wananufaika kwa hiyo tuwanyang’anye hawa watoto tuwapeleke shuleni. Mmewanyang’anya watoto mmewapeleka shuleni, shuleni kule wale watoto hawana walimu, matokeo yake mnawaathiri watoto hawa. Kwa sababu watoto hawawezi kulalamika hamuwezi kuona madhara yake, lakini tutambue sisi wote ni Watanzania leo sisi tunawawakilisha wananchi, lakini hawa Watanzania wa kesho wanakosa huduma. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ziko ramani zinatoka Wizara ya Elimu zinaitwa MESS Makao Makuu kitu kama hicho zinapelekwa mashuleni kwa ajili ya ujenzi wa shule. Tumepiga kelele sana humu ndani juu ya suala la watoto wa kike kujisitiri. Maelezo yanasema kila shule iwe na mahali maalum pa watoto wa kike kujisitiri Serikali hiyo hiyo inaleta ramani haina chumba cha kujisitiri. Sasa hayo maelezo anapewa nani na anatekeleza nani? Hebu tuangalie tunapotoa maelezo tuhakikishe kwamba maelekezo haya yanakwenda kujibu ile kiu ambayo wananchi na wawakilishi wao wanahitaji wapewe huduma. Kama Serikali haiwezi kwa sasa kuwapa watoto hawa taulo za kujisitiri basi hata iwajee chumba maalum. Maelekezo yanasema hivyo, lakini utekelezaji unakwenda kinyume. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini lipo jambo lingine, uko mkanganyiko kati ya taasisi mbili za Serikali, iko Idara ya Wakaguzi wa Elimu lakini iko Idara inashughulika na usalama mahali pa kazi. Wananchi wanajenga darasa ile idara inakuja kusema darasa hili halina mwanga wa kutosha wakati Wakaguzi wa Elimu wamekagua na wamepitisha hilo darasa, sasa hapo wananchi wafanye nini? Kwa hiyo, nafikiri Idara hizi za Serikali zijaribu kuona ni namna gani zinaweza kushirikiana ili kusudi wananchi wakifanya shughuli ikikamilika iwe imekamilika. Siyo Idara hii ya Serikali inaseme shughuli hii haina sifa, shughuli hii ina sifa. Kwa hiyo, naomba Idara za Serikali ziwasiliane katika hilo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ni elimu ya ufundi. Sasa hivi tunakwenda kwenye Tanzania ya Viwanda, ndugu zangu Wabunge humu ndani nawaambieni hivi viwanda tunavyohamasisha vijengwe tunakwenda kulifanya hili Taifa kuwa la watwana kwa sababu vijana wetu hawana ujuzi, sasa ni nani atakayefanya kazi kwenye hizo taasisi? Tunasema VETA wakati inakwenda mwendo wa konokono hakuna mfano wake, hawana vifaa wala walimu, VETA wana mitaala ya miaka 70 iliyopita wanafundisha sijui calibrator, wanafundisha vitu vya ajabu ajabu ambayo havipo kwenye ulimwengu wa sasa wa utendaji hasa hawa ndiyo wanatakiwa kwenda kufanya kazi kwenye viwanda vinavyojengwa na tunafahamu viwanda vinavyokuja ni vya teknolojia ya kisasa. Kwa hiyo, tunakwenda kuwapeleka Watanzania mahali ambapo watakuwa wafagia uwanja, wapakia mizigo, ndiyo kazi wanazokwenda kufanya. Kama kweli tunahamasisha viwanda sisi kama Watanzania tuwapange vizuri vijana wetu wapate elimu nzuri ya kuweza kuajirika huko kwenye viwanda vyenye teknolojia ya kisasa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie suala la UKIMWI. Tafiti za UKIMWI zinanitatanisha sana, mimi ni Mbunge wa Njombe Mjini na ukiangalia kwenye taarifa za Serikali Njombe ndiyo tunaambiwa sisi tunaongoza kwa UKIMWI katika nchi hii, lakini hizi data ni za lini kwa sababu mimi hapa nahisi kuna kuonewa. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa za miaka kumi mpaka leo ndiyo zinatumika kwamba Mkoa unaoongoza kwa UKIMWI Tanzania ni Njombe, siyo kweli tutendeane haki. Kama mnataka kutoa utafiti wa kisasa na wa kitaalam fanyeni utafiti kila mwaka.

T A A R I F A . . .

MHE. EDWARD F. MWALONGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niendelee.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, mimi nina mashaka sana na takwimu hizi za Serikali juu ya suala la UKIMWI. Hata hivyo, kama kweli Serikali inatuona kweli sisi watu wa Njombe ndiyo tunaongoza kwa UKIMWI mbona haitusaidii kupunguza UKIMWI? Zana zile za kujikinga hatuletewi…

T A A R I F A . . .

MHE. EDWARD F. MWALONGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa hizi za Serikali sawa tunakubaliana nazo kimsingi, lakini ukitokea ukame hapa, wale wanaokuwa wamefiwa na ng’ombe huko, Serikali inawapa ng’ombe; ikitokea njaa watu wanapelekewa misaada ya chakula. Sisi tuna UKIMWI, kwa nini hatusaidiwi? Kama sisi tuna UKIMWI, tupeni hiyo misaada basi tuione. (Kicheko/Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaichotaka Serikali ioneshe kweli kwamba Njombe wanateketea. Njombe ikiteketea, maana yake Watanzania watokosa chips, ndio wakulima wa viazi hao, watakosa maparachichi, mtakosa ma- housegirl mnaokuja kuwachukua Njombe na sisi tumepiga marufuku. Kwa sababu hawa watoto wetu mnawachukua kwa ajili ya kufanya kazi za ndani, nao ni sehemu ya kuchangia UKIMWI Njombe. Mnawaacha kwenye majumba yenu, hawana ulinzi wala uangalizi, wanaambukizwa UKIMWI wanarudhishwa vijijini kule, wanaenda kupaka vijana vijijini. Kwa hiyo, nawaomba sana, msije tena Njombe kuchukua ma-housegirl, tumekataa. (Kicheko/Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, yangu kwa leo ni hayo.
Ahsante sana.