Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jamii Kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2017 pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Masuala ya UKIMWI kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2017

Hon. George Malima Lubeleje

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mpwapwa

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jamii Kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2017 pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Masuala ya UKIMWI kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2017

MHE. GEORGE M. LUBELEJE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi ili na mimi niweze kuchangia hoja hii ya Kamati hizi mbili. Kwanza niwapongeze sana Wenyeviti wa Kamati na Kamati kwa kazi nzuri sana wanayofanya kwa sababu kama Kamati ya Maendeleo ya Jamii majukumu yao ni mengi na sekta zao ni nyingi sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitaanza na suala la sekta ya afya. Sekta ya afya ina changamoto nyingi sana, sasa hivi wananchi wanajenga zahanati na vituo vya afya. Sasa unavyosema jengo la zahanati, kituo cha afya au hospitali ya Wilaya siyo jengo tu, ni dawa pamoja na watumishi. Hata hivyo, pamoja na kwamba katika bajeti hii tumetenga shilingi bilioni 251 kwa ajili ya kununua dawa, vifaa tiba pamoja na vitendanishi lakini bado kuna upungufu mkubwa sana wa dawa katika hospitali zetu za wilaya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, namwomba Mheshimiwa Waziri atembelee Hospitali za Mikoa, Wilaya na Vituo vya Afya hasa vijijini ndiyo kabisa maana linakwenda sanduku moja, idadi ya watu ni 2,000 mpaka 3,000, dawa hazitoshi. Naomba viongozi wetu wa Wizara ya Afya mnapotamka kwamba hakuna upungufu wa dawa kabisa, hospitali zetu zote zina dawa za kutosha, hapana, upo upungufu mkubwa sana wa dawa. Pamoja na hii bajeti kuongezwa, lakini tujitahidi kuongeza fedha za kutosha tununue dawa za kutosha ili wananchi wetu wapate huduma. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mpaka leo hii unakwenda katika hospitali, mganga anamwandikia mgonjwa dawa anakwenda kununua duka la mtu binafsi, bado wapo na haipendezi kabisa. Tulishauri kwamba MSD wajenge maduka katika baadhi ya Hospitali za Wilaya ili dawa zinazokosekana kwenye pharmacy ya hospitali basi zipatikane pale. Kwa sababu bei ya dawa katika maduka ya watu binafsi ni kubwa zaidi kuliko haya maduka yetu ya MSD. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili, ni sekta ya elimu. Wizara ya Elimu imeanzisha kidato cha tano na cha sita katika baadhi ya shule kwenye wilaya zetu. Hata hivyo, kuna changamoto kubwa sana ya mabweni, mabwalo, na chakula. Hizi shule zimeanzishwa form five na six lakini wameachiwa wananchi ndiyo wanaojenga. Siyo vibaya wananchi wakajenga madarasa, mabwalo na hosteli lakini tunaomba Serikali isaidie vifaa vya kukamilisha majengo haya, ni shida sana, vijana wanasoma katika mazingira magumu. Maana form five na six vijana wale hawatoki mazingira ya pale pale bali Mikoa yote ya Tanzania. Kwa mfano, tuna Shule ya Sekondari ya Wasichana Mazae, mazingira yake ni magumu sana. Tumejenga hosteli na mimi Mbunge nilitoa mifuko 200 kwa ajili ya kujenga hosteli, lakini mazingira ni magumu. Kwa hiyo, naomba Serikali isaidie vifaa vya kukamilisha majengo yale. Wananchi tunawahamasisha, wako tayari wanajenga lakini vifaa vya kukamilisha majengo hayo hatuna. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, bajeti ya chakula ni kidogo sana. Mwanafunzi mmoja anapata hela ya chakula kwa siku shilingi 1,500 kwa asubuhi, mchana na jioni kwa hizi shule za bweni. Hivi kweli unaweza kula breakfast, lunch na dinner kwa shilingi 1,500? Haiwezekani. Kwa hiyo, naomba waongeze fedha za chakula kwa siku angalau iwe shilingi 2,500, hii inaweza kuwatosha wanafunzi lakini siyo shilingi 1,500.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nishauri kwa kuwa Halmashauri zetu za Wilaya zina shule za msingi pamoja na sekondari kidato cha kwanza mpaka kidato cha nne, naomba Wizara ya Elimu mngewapokea form five na six muwapunguzie majukumu Serikali za Mitaa maana wana majukumu kweli. Toka elimu ya msingi, darara la kwanza mpaka darasa la kumi na mbili halafu mnaongezea tena kitado cha tano na kidato cha sita, yote Halmashauri ya Wilaya. Nashauri form five na six Wizara ya Elimu yenyewe ishughulikie hizi shule.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la lingine ni kuhusu suala la UKIMWI. Ushauri wangu ni kwamba Serikali inatenga fedha nyingi sana na wafadhili wanaleta fedha nyingi sana kwa ajili ya mapambano dhidi ya UKIMWI na fedha hizi zinapelekwa katika Halmashauri zetu za Wilaya lakini zisimamiwe basi ziwahudumie waathirika wa UKIMWI wenyewe. Sasa hivi wananchi wanaelewa UKIMWI ni nini lakini fedha nyingi sana zinakwenda kwenye semina makongamano wale waathirika kabisa wa UKIMWI hawafaidiki. Kwa hiyo, nashauri wale waratibu wa UKIMWI kwa kila Halmashauri wakipata hizi fedha wahakikishe walengwa ndiyo wanafaidika na hizi fedha, siyo kuanzisha semina na mambo mengine. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema haya, kwanza nikushukuru kwa kunipa nafasi lakini la pili nipongeze sana hizi Kamati mbili kwa kazi na taarifa nzuri sana. Naunga mkono kwa asilimia mia moja. Ahsante sana.