Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Sheria Ndogo na Kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2017, Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Katiba na Sheria Kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2017 pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala na Serikali za Mitaa Kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2017

Hon. Jenista Joackim Mhagama

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Peramiho

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Sheria Ndogo na Kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2017, Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Katiba na Sheria Kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2017 pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala na Serikali za Mitaa Kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2017

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA WAZIRI MKUU, SERA, BUNGE, KAZI, AJIRA, VIJANA NA WENYE ULEMAVU: Mheshimiwa Mwenyekiti nakushukuru, na mimi nianze kwa kuwapongeza sana hasa Kamati mbili, Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Katiba na Sheria, lakini vilevile kwenye muktadha wa mjadala wetu wa leo niwapongeze pia Kamati ya Sheria Ndogo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninawapongeza sana Wajumbe wa Kamati hizi mbili kwa kweli wamefanya kazi kubwa sana katika kuishauri Serikali na wametekeleza majukumu yao sawasawa. Kwa hiyo kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri Mkuu naomba niwapongeze sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ziko hoja kadhaa zimejitokeza katika Kamati hizi zote ambazo zimesoma taarifa na mimi nianze kwanza kwa kuunga mkono hoja ya Kamati hizo zote mbili ambazo zinairuhusu Ofisi ya Waziri Mkuu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niseme jambo la kwanza limezungumzwa suala kuhusu Baraza la Vijana. Ninaomba nichukue nafasi hii nitoe taarifa kwenye Bunge lako Tukufu, wote tunakumbuka mwaka 2015 tulipitisha Sheria ya Kuunda Baraza la Taifa la Vijana katika nchi yetu ya Tanzania. Lengo letu kubwa lilikuwa ni kuwaunganisha vijana wote wawe pamoja, kuondoa itikadi zao za kisiasa na kuwafanya wawe wazalendo kwa nchi yao ya Tanzania. Vilevile kuwafanya vijana wa Taifa hili la Tanzania waelewe umuhimu wao wa kuwepo katika nchi yetu ya Tanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaomba niwaambie Waheshimiwa Wabunge, baada ya sheria ile kupita, tayari kanuni za kuanzisha Baraza hili zimeshakamilika. Hata wewe Mheshimiwa Mwenyekiti wa Kikao cha leo nakumbuka Ofisi ya Waziri Mkuu ilishakuja mbele ya Kamati yako ili kupitia kanuni zile na kuziweka sawa sawa na sasa muda si mrefu, uundwajiwa wa Baraza la Taifa la Vijana utaanza kupitia ngazi mbalimbali kama sheria inavyosema.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nichukue nafasi hii kuwaomba Waheshimiwa Wabunge vijana wote, tutakapofika nafasi hiyo sasa ya uundaji wa Baraza la Vijana la Taifa watoe ushirikiano kwa Serikali kusudi kazi hii iweze kufanyika vizuri. Kwa hiyo, katika suala hilo tunakwenda vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Kamati ya Sheria Ndogo imetuelekeza Serikali na kwa kweli tumekuwa Ofisi ya Waziri Mkuu tukitekeleza jukumu la kisheria la kuweka mezani sheria ndogo zote ambazo zimekuwa zikiandaliwa na kupitishwa na mamlaka mbalimbali za Serikali ikiwemo Wizara mbalimbali. Tumekuwa tukipokea maoni ya jumla yanayohusiana na sheria hizo ndogo zote katika nchi yetu ya Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Kamati ya Sheria Ndogo imefanya kazi kubwa, imepitia sheria nyingi sana ndogo katika nchi yetu ya Tanzania. Mimi niseme kama Serikali na taasisi zake itaendelea kufanya vizuri katika kutunga sheria ndogo katika nchi yetu ya Tanzania, ni kwa sababu Kamati ya Sheria Ndogo imebaini makosa na imeturekebisha katika maeneo mengi sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo nichukue nafasi hii kuliahidi Bunge lako Tukufu kwamba tutazingatia maoni na ushauri wa Kamati ya Sheria Ndogo katika kuhakikisha kwamba sheria ndogo zitakazokuwa zinatumika katika nchi yetu ya Tanzania zinaendana na sheria mama na zitakwenda kutenda haki katika kusimamia sheria mama katika nchi yetu ya Tanzania. Kwa hiyo, maagizo ya Kamati ya Sheria Ndogo tumeyapokea na tutayapeleka Serikalini kwa ajili ya utekelezaji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lilizungumzwa suala lingine kuhusu NSSF. Waheshimiwa Wabunge ninaomba niwaambie, sisi kama Serikali hatujafumba macho kuhusu suala la NSSF. Kamati ya PAC ilishasoma taarifa yake hapa ndani ya Bunge, na mimi niliwaamba kwamba pamoja na shughuli inayoendelea ndani ya Serikali ya kuimarisha NSSF, tumeimarisha Bodi na hivi juzi tumeunganisha Mifuko ya Hifadhi ya Jamii, lakini tumesema NSSF itabakia kuwa mfuko kwa ajili ya private sector na kwa ajili ya sekta isiyo rasmi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa moja kwa moja Serikali inaona jukumu kubwa la NSSF. Ninaomba niwahakikishie Waheshimiwa Wabunge tunaendelea kuyatupia macho yale yote yaliyojiri kwenye NSSF na tumeiagiza Bodi kuhakikisha kwamba inasimamia ipasavyo na inatenda haki katika kushughulikia masuala yote yaliyojitokeza kwenye NSSF. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Kwa hiyo Waheshimiwa Wabunge, jambo hili sisi tunalishughulikia vizuri na msiwe na hofu. Lengo letu ni kuhakikisha fedha za wanachama zinabaki kuwa salama, na vilevile Mfuko wa NSSF ambao uhai wake unafika mpaka mwaka 2085 uendelee kuwa mfuko ambao una maisha marefu ya kuhudumia Watanzania. Kwa hiyo, naomba Waheshimiwa Wabunge niwahakikishie kwamba tupo imara na tutafanya kazi hiyo vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, limezungumzwa suala la ajira katika nchi yetu ya Tanzania na hasa kwa ajili ya vijana. Mwaka 2014 tulifanya utafiti wa hali ya nguvukazi katika nchi yetu ya Tanzania, na tuligundua kwamba Watanzania takribani milioni 25 ndio nguvukazi ya taifa katika nchi yetu. Lakini asilimia 56 ya hao Watanzania milioni 25 ni vijana. Tulijitahidi pia kuangalia ujuzi wa hawa vijana je, unaendana na soko la ajira katika nchi yetu ya Tanzania?

Mheshimiwa Mwenyekiti, Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Katiba na Sheria inafahamu tulipokwenda kwenye Kamati tuliwaeleza baada ya utafiti huu, Ofisi ya Waziri Mkuu iliandaa programu tano za kuhakikisha tunakuza ujuzi wa vijana ili waweze kuajirika katika miradi mbalimbali kwenye nchi yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninafurahi kukuambia kwamba kwa taarifa tulizonazo sasa mwaka 2015/2016 katika nchi yetu ya Tanzania ajira ambazo zilikuwa zimetengenezwa nchini zilikuwa ni ajira 390,676. Mwaka 2016/2017 ajira zilizotengenezwa katika nchi yetu ya Tanzania zimeendelea kuongezeka mpaka kufikia ajira 421,803.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sekta inayoongoza kwa kutoa ajira kwa wingi ni sekta binafsi, sekta inayofatia ya kutoa ajira kwa wingi ni sekta ya miradi ya maendeleo. Kwa hiyo, tunajitahidi kusimamia miradi ya maendeleo ili kukuza ajira katika nchi yetu ya Tanzania. Ahsante sana.