Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Sheria Ndogo na Kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2017, Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Katiba na Sheria Kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2017 pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala na Serikali za Mitaa Kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2017

Hon. Prof. Palamagamba John Aidan Mwaluko Kabudi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kilosa

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Sheria Ndogo na Kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2017, Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Katiba na Sheria Kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2017 pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala na Serikali za Mitaa Kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2017

WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA: Mheshimiwa Mwenyekiti, na mimi nichukue fursa hii kuzishukuru sana Kamati zote kwa taarifa nzuri walizoziwasilisha. Jukumu letu sisi ni kupokea mapendekezo yote yaliyotolewa na kamati hizo pamoja na Wabunge waliochangia.

Nichukue fursa hii kuishukuru sana Kamati ya Katiba na Sheria kwa mchango mkubwa iliyoutoa hasa wakati tulipokuwa tunakabiliwa na kupitisha sheria zile muhimu kwa ajili wa ulinzi wa rasilimali na mali zetu za asili yaani sheria ya The Natural Wealth and Resources Permanent and Sovereignity Act 2017Act No. 5 of 2017, The Natural Wealth and Resouces Contracts (Review and Re-Negotiation of Unconscionable Terms) Act No. 6 of 2017 na The Written Laws Miscellaneous Amendments Act No. 7 of 2017.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mchango wa Kamati ulikuwa mkubwa sana na ndiyo maana kama wote tunakumbuka schedule of amendment iliyoletwa na Kamati ilisaidia sana kuboresha sheria hiyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na hayo nishukuru sana mchango uliotolewa kuhusu utungaji wa kanuni. Ni kweli kabisa sheria zikitungwa zinahitaji kanuni ili ziweze kutekelezwa na moja ya sheria ambayo ilihitaji kanuni hizo ni mabadiliko ya Sheria ya Madini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimshukuru sana Mheshimiwa Rais kwa kuhimiza ukamilishaji wa Kanuni za Madini na kazi hiyo ilikamilika na nimshukuru sana Waziri wa Madini ingawa alikuwa katika likizo ya uzazi yaani maternity leave aliweza kupata nafasi ya kurudi na kuweza kuzitia saini kanuni zote tarehe 9 Januari, 2018.

Pia nimshukuru sana Katibu Mkuu Kiongozi ambaye na yeye kwa mujibu mamlaka aliyopewa chini ya Sheria ya Executive Urgency aliweza kutia sahihi amri mbili za kufuta baadhi ya mamlaka ambazo zimeondolewa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikubaliane na Mheshimiwa Daniel Mtuka, Mbunge wa Manyoni Mashariki kwamba kuna umuhimu wa kuimarisha ubora wa utungaji wa sheria ndogo na utungaji wa kanuni.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninamini kabisa mabadiliko yaliyoanza kufanyika katika ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali yataongeza ufanisi katika utungaji wa sheria na kanuni ndogo ndogo. Ni eneo ambalo linahitaji kufanyiwa kazi zaidi na nina imani chini ya Mwanasheria Mkuu mpya wa Serikali Dkt. Adelardius Lubango Kilangi tutaongeza ufanisi wa kupitia sheria na kuzifanya ziwe bora zaidi na baada ya muda mfupi mabadiliko zaidi katika Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali yatafanyika ili kuhimiza na kuimarisha ufanisi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nichukue pia nafasi hii kusema kwamba inapokuja kwenye maswali ambayo yameulizwa na Ndugu Ayoub Jaku namwomba tu kwamba maswali yake yote hayo aliyoyauliza yaje Bungeni kwa kanuni za kawaida za Bunge, kwa sababu hapa tunajielekeza katika taarifa iliyotolewa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nichukue pia nafasi hii kuishukuru Kamati kwa maelezo iliyotoa kuhusu kazi kubwa inayofanywa na mahakama. Ni kweli kabisa mahakama zinakabiliwa na upungufu wa Mahakimu na Majaji lakini Serikali iko katika hatua ya kukamilisha upekuzi wa wale wote wamependekezwa kuwa Majaji au Mahakimu ili kuhakikisha kwamba tuna Majaji au Mahakimu ambao hawana tuhuma za ufisadi, hawana tuhuma za rushwa, lakini pia ni waadilifu na wanaoweza kutekeleza majukumu yanayotakiwa kwa ufanisi na weledi zaidi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia ningependa nieleze kuhusu suala la makosa mbalimbali na faini kuwa chini. Hiyo ni moja ya changamoto na ambazo zinafanyiwa kazi na Tume ya Kurekebisha Sheria, ni kuona ni mfumo gani utumike utakaotusaidia kuhakikisha kwamba faini haziwi chini baada ya muda mfupi kutokana na thamani ya fedha ya Tanzania kushuka. Kwa hiyo, maeneo yote hayo yanafanyiwa kazi ili uhakikisha kwamba faini zitaendana na hali ya mabadiliko ya kiuchumi nchini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu suala zima la utawala wa sheria na utalawa bora. Ningependa kuwahakikishia Watanzania wote kwamba taasisi zote na mihimili yote inayohusika na utawala bora inafanya kazi inavyotakiwa. Moja ni Mahakama za Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ikiwepo Mahakama ya Rufani ina uhuru kamili, inafanya maamuzi na maamuzi yake yanaheshimiwa na nchi. Kwa hiyo Watanzania wowote au wananchi wowote ambao wanaona haki zao zimeminywa wanao uhuru kamili chini ya Katiba kwenda mahakamani na mashauri yao kuamuliwa na daima Serikali imekuwa inaheshimi maamuzi ya mahakama kwa jinsi yanavyokwenda.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora imekuwa inafanya kazi nzuri ya kuelekeza maeneo gani ya utawala bora na haki za binadamu yafanyiwe maboresho ili kuboresha zaidi. Kwa hiyo, naishukuru sana Kamati ya Katiba na Sheria kwa maoni na miongozo mbalimbali waliotoa kusaidia kuboresha hali hiyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, duniani kote daima utawala bora, utawala wa sheria na demokrasia ni mambo yanayohitaji daima kufanyiwa kazi ili kuyaboresha. Leo nimesafiri na Balozi wa nchi moja ya Ulaya na nilimkumbusha kwamba mpaka leo tunavyozunguza nchi ya Switzerland katika baadhi ya maeneo ya nchi ya Switzerland wanawake hawaruhusiwi kupiga kura na hii ni nchi ya Switzerland, lakini mpaka leo wanawake hawaruhusiwi kupiga kura, wanaopiga kura ni wanaume tu. Nchi za Ulaya mpaka leo kwa daraja lile lile na cheo kile kile mwanamke analipwa chini kuliko mwanaume.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata Wabunge, Wabunge Wanawake wanalipwa chini kuliko Wabunge Wanaume sihalalishi, lakini nataka nieleze kwamba kila nchi ina changamoto. Wabunge Wanawake hawa wangekuwa kwenye baadhi ya nchi za Ulaya wangepokea mshahara mdogo kuliko Wabunge Wanaume.

Kwa hiyo, changamoto hizi za kuboresha demokrasia daima zipo na Taifa lolote haliwezi kusema limekamilika ni lazima liendelee kuboreshwa. Kwa maana hiyo tunapokea michango yote iliyotolewa yenye lengo la kuboresha demokrasia yetu na haki za binadamu ili tuweze kuwa na hali bora zaidi bila kubeza hatua kubwa ambayo Tanzania imepiga katika demokrasia, Tanzania imepiga katika haki za binadamu, Tanzania imepiga katika usawa wa wanaume na wanawake. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya maelezo hayo naomba pia kuunga mkono hoja iliyotolewa.